Fursa, watumiaji wa intaneti Tanzania wakifikia milioni 58.1

  • Hadi kufikia robo ya mwaka inayoishia Desemba 2025, watumiaji wa intaneti walikuwa milion 58.1 kutoka milioni 56.3 iliyorekodiwa Septemba 2025.
  • Intaneti hiyo hutumiwa zaidi na simu za janja. 
  • Hiyo inaongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na fursa za mtandaoni. 

Dar es Salaam. Idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za intaneti imeendelea kuongezeka kwa kasi na kufikia milioni 58.1 suala linalotajwa kuendelea kufungua fursa zaidi za kiuchumi.

Takwimu za mawasiliano za robo ya nne ya mwaka 2025 zilizotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zinaonesha matumizi ya huduma z aintaneti yameongezeka kwa asilimia 3.2.

Takwimu hizo zinaonyesha kuwa hadi kufikia Desemba 2025 watumiaji wa intaneti walifikia milioni 58.1 kutoka watumiaji  56.3 waliokuwepo Septemba 2025.

Idadi hiyo ni sawa na ongezeko la watumiaji milioni 1.8 ndani ya kipindi cha miezi mitatu kuanzia Septemba hadi Disemba mwaka jana.

Kwa mujibu wa TCRA, idadi hiyo inajumuisha laini zote zilizotumia huduma ya intaneti angalau mara moja katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita, bila kujali teknolojia iliyotumika kupitia njia mbalimbali, zikiwemo laini za simu za mkononi, nyaya za faiba (fiber), pamoja na teknolojia za mawimbi (wireless). 

Uchambuzi wa takwimu hizo uliofanywa na Nukta Habari kwa miaka 10 mfululizo umebaini ongezeko la watumiaji wa intaneti nchini Tanzania mwaka hadi mwaka.

Huenda ukuaji huo umechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuendelea kuimarika kwa miundombinu ya mawasiliano nchini, ikiwemo ongezeko la minara ya simu iliyofikia 10,029 kufikia mwisho wa mwaka 2024.

Aidha, intaneti inayotumia mtandao wa simu za mkononi (mobile wireless internet) imeendelea kuwa njia kuu ya upatikanaji wa huduma hiyo, ikichangia asilimia 99 ya usajili wote wa intaneti nchini. 

Mbali na ongezeko la matumizi ya intaneti, matumizi ya simu janja (smartphones) pia yameongezeka, ambapo kiwango cha upenyo wake kimefikia asilimia 41.82. 

Hata hivyo, simu za kawaida (feature phones) bado zinaendelea kutumika kwa kiwango kikubwa zaidi zikiwa na asilimia 87.11 ya matumizi.

Ni fursa iliyojificha

Wachambuzi wa uchumi wanaeleza kuwa ongezeko hilo la matumizi ya intaneti linafungua fursa mpya katika biashara, elimu, huduma za kifedha na ajira za kidijitali, huku likichochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

Akizungumza kuhusu mwenendo huo, Profesa Abel Kinyondo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amesema kuwa ongezeko la usajili wa laini zinazotumia intaneti halimaanishi moja kwa moja kuwa idadi hiyo ni sawa na watumiaji halisi, kwa kuwa mtu mmoja anaweza kuwa na laini zaidi ya moja.

Amefafanua kuwa pamoja na changamoto zilizopo, intaneti imeleta mapinduzi makubwa katika shughuli za kiuchumi kwa kurahisisha biashara, masoko na huduma za kifedha.

“Leo mtu anaweza kufanya biashara akiwa sehemu yoyote nchini bila kulazimika kusafiri. Intaneti imeongeza urahisi wa kufanya miamala, kutangaza bidhaa na kupata taarifa mbalimbali kwa haraka,” amesema Profesa Kinyondo.

Hata hivyo, ameonya kuwa matumizi ya intaneti yanaambatana na changamoto mbalimbali zikiwemo uhalifu wa mtandaoni, udanganyifu katika biashara za mtandaoni na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.

Pia amewataka vijana kutumia intaneti kwa manufaa, ikiwemo kujifunza ujuzi mpya, kufanya biashara na kutafuta maarifa, huku wakizingatia tahadhari dhidi ya matumizi yanayoweza kuhatarisha usalama wao binafsi na maadili ya jamii.

ATCL inavyopoteza mabilioni kila mwaka

Licha ya Februari 6, 2026, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa kusema kuwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) linaendelea kuimarika likionesha ukuaji chanya na kukusanya jumla ya mapato ya zaidi ya Dola za Marekani milioni 157 (sawa Sh404.5 bilioni) tangu kuimarishwa kwake upya.

Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imebaini kuwa ATCL ilipata hasara ya Sh191.19 bilioni katika mwaka wa fedha 2024/25 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kuongezeka kwa gharama za uendeshaji.

CAG Charles Kichere aliyekuwa akiwasilisha ripoti ya ukaguzi wake Machi 30, 2026 mbele ya Rais Samia Suluhu Hassan amesema hasara hiyo imeongezeka kwa asilimia 108 ndani ya kipindi cha mwaka mmoja ikiongezeka maradufu tangu kuanzishwa kwake.

“ATCL imefikisha jumla ya hasara ya Sh 748 bilioni tangu kuanzishwa kwake licha ya kuendelea kupata ruzuku za Serikali kwa ajili ya mishahara na gharama za uendeshaji,” amesema CAG Kichere.

Hii ni mara ya tatu mfululizo kwa ATCL kutajwa kuwa miongoni mwa mashirika ya umma yanayotengeza hasara nchini.

Mwaka 2022/23 ATCL lilitengeneza hasara ya Sh56.6 bilioni iliyoongezeka kutoka Sh35.2 bilioni mwaka 2021/22 kabla ya kupaa tena mwaka 2023/24 kufikia 91.7 bilioni licha ya uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali katika shirika hilo.

Kwa mujibu wa Kichere, hasara hiyo imechangiwa na mambo mbalimbali ikiwemo ongezeko la gharama za uendeshaji kuzidi ukuaji wa mapato ambapo gharama ziliongezeka kwa Sh 134 bilioni na kufikia Sh675 bilioni.

Aidha, amesema matumizi yasiyo bora ya ndege ya mizigo aina ya Boeing 767-300F yamechangia hasara hiyo, ambapo asilimia 90.4 ya safari zilikuwa za masafa mafupi na ya kati badala ya safari ndefu zenye mapato makubwa.

Kutokana na Hali hiyo ndege ilisimamishwa huku ikiendelea kugharimu shirika takribani Sh bilioni 3.5 kwa ukodishaji na bima bila kuzalisha mapato.

Pia CAG ameeleza kuwa udhaifu wa mifumo ya udhibiti umepelekea malipo ya Sh20.61 bilioni kwa mawakala bila kuthibitishwa kuwafikia abiria, pamoja na marejesho ya fedha kwa abiria ya Sh 31.7milioni yaliyofanyika bila nyaraka za kuthibitisha uhalali wake.

Bei ya maharage yaendelea kuwa kichomi Dar es Salaam 

Dar es Salaam. Bei ya maharage imeendelea kuwa tulivu nchini kutokana na kutobadilika ndani ya wiki licha ya kuendelea kwa msimu wa mvua za masika katika maeneo mbalimbali nchini. 

Kwa kawaida msimu wa mvua za masika na kipindi cha mfungo wa Ramadhan na Kwaresma kama hiki, bei za bidhaa za vyakula hupaa kutokana na kuongezeka kwa mahitaji na kupaa kwa gharama za uchukuzi kwa sababu ya athari ya mvua kwenye miundombinu. 

Uchambuzi wa bei za jumla za mazao uliofanywa na Nukta Habari umebainisha kuwa kuwa bei hizo zimeendelea kuwa thabiti katika mikoa mbalimbali, huku tofauti kubwa ikionekana kati ya bei ya juu na ya chini.

Kwa mujibu wa takwimu za mazao makuu ya biashara zilizotolewa leo Machi 4, 2026, na Wizara ya Viwanda na Biashara, bei ya jumla ya gunia la kilo 100 la maharage imeendelea kuwa Sh400,000 katika soko la Mwananyamala, jijini Dar es Salaam sawa na bei iliyorekodiwa mapema wiki hii.

Kubaki juu kwa zao hilo kwa chakula kutaendelea kuwa mzigo kwa mlaji wa mwisho, huku wafanyabiashara wakinufaika na viwango hivyo vya juu.

Hata wakati Dar es Salaam wakinunua zao hilo kwa bei ya juu, Njombe wao ndo wananunua maharage kwa bei ya jumla ya chini zaidi nchini ambapo gunia la kilo 100 linauzwa kwa Sh110,000. Bei hiyo ya Njombe ni ya chini takriban mara 4 ya ile ya Dar es Salaam na imeendelea kubaki kama ilivyokuwa mwanzoni mwa wiki.

Aidha, bei hizo hazijaonyesha mabadiliko katika mkoa wa Kigoma, ambapo zinaendelea kutumika kama zilivyokuwa Jumatatu.

Tanga waendelea kutoboa mifuko bei ya mahindi

Kununua gunia la mahindi la kilo 100 mkoani Tanga itakulazimu kulipia Sh140,000 ambayo ni mara 2 na nusu ya bei ya chini iliyorekodiwa mkoani Njombe ya Sh55,600 kwa gunia la kilo 100.

Wakati wakazi wa mkoa huo wakilia na bei hiyo, hali ni tofauti kwa wakazi wa mkoani wa Dar es Salaam ambao wananunua gunia la kilo 100 za viazi mbatata/ mviringo kwa Sh60,000 ambayo ni ahueni kwa mara 3 zaidi ya ile iliyorekodiwa mkoani Tanga ya Sh180,000.

Ufaulu kidato cha nne unavyopanda na kushuka Tanzania

  • Takwimu zinaonesha ufaulu unashuka na kuongezeka  mwaka hadi mwaka katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021.

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta) limetangaza matokeo ya mitihani ya kidato cha nne iliyofanyika Novemba, 2025, ambapo ufaulu umeongezeka kidogo kulinganisha na miaka iliyopita.

Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Dk. Said Mohamed aliyekuwa akitangaza matokeo hayo jijini Dar es Salaam leo Januari 31, 2026 amesema kuwa ufaulu wa wanafunzi kwa kidato cha nne kwa mwaka 2025 ni asilimia 92.37. 

Uchambuzi uliofanywa na Nukta Habari unaonyesha kuwa ufaulu wa kidato cha nne umekuwa ukipanda na kushuka kwa miaka tofauti katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021.

Takwimu zinaonyesha kiwango cha ufaulu kiliongezeka kwa asilimia 0.67 na kufikia asilimia 87.79 mwaka 2022 kutoka asilimia 87.30 iliyorekodiwa mwaka 2021. Hata hivyo, ufaulu huo ulishuka kwa asilimia 0.32 na kufikia asilimia 87.65 mwaka 2023.

Ongezeko thabiti la matokeo ya kidato cha nne limeonekana kuanzia mwaka 2024 ambapo ufaulu uliongezeka kwa takriban asilimia 4.72 na kufikia asilimia 92.37.

Aidha, katika kipindi cha miaka mitano wavulana ndio wanaongoza kwa kuwa na ufaulu wa juu zaidi ya wasichana wakiwa na wastani wa ufaulu wa asilimia 92.75 wakiwaacha mbali wasichana wenye wastani wa asilimia 90.71.

Sekta ya fedha inavyoimarika Tanzania

Dar es Salaam. Katika siku za hivi karibuni, sekta ya fedha nchini Tanzania imeendelea kuonesha mwelekeo chanya wa ukuaji, ikichochewa na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi, upanuzi wa taasisi za kifedha na kuimarika kwa imani ya wananchi katika mifumo rasmi ya fedha. 

Ukuaji huo umejidhihirisha kupitia ongezeko la idadi ya benki, taasisi za huduma ndogo za fedha, mawakala wa benki pamoja na rasilimali za kibenki, hali inayoashiria kuimarika kwa mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula aliyekuwa akizungumza Januari 21, 2025 katika uzinduzi maadhimisho ya kitaifa ya wiki ya huduma ya fedha, amesema hadi kufikia Septemba 2025, Tanzania ilikuwa na jumla ya benki za kibiashara 35, benki za kijamii mbili, benki za maendeleo mbili pamoja na benki tatu za huduma ndogo za fedha. 

Aidha, taasisi 2,811 za huduma ndogo za fedha pamoja na vikundi vya kijamii vya huduma ndogo za fedha 70,913 zilisajiliwa, huku taasisi mbili za ubadilishanaji wa fedha zikiongeza idadi ya watoa huduma rasmi nchini.

Aidha, Luswetula ameeleza kuwa upanuzi huo umeenda sambamba na ongezeko kubwa la mawakala wa benki nchini. Ambapo Idadi ya mawakala wa benki imeongezeka kutoka 106,176 hadi kufikia 145,430, jambo linalorahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha hadi ngazi ya jamii.

Mbali na ongezeko la taasisi, rasilimali za kibenki nazo zimeendelea kuimarika na kufikia Sh71.8 trilioni Septemba 2025, ikilinganishwa na Sh62.2 trilioni zilizorekodiwa Septemba 2024.

Aidha, katika kipindi kama hicho, amana za benki zimeongezeka hadi Sh50.2 trilioni kutoka Sh42.7 trilioni mwaka uliotangulia, hatua inayotafsiriwa kama ishara ya kuongezeka kwa imani ya wananchi katika sekta ya fedha.

Katika maelezo yake, Luswetula pia amebainisha kuwa mikopo kwa sekta binafsi imekua kwa kasi kubwa. Ikiongezeka na kufikia Sh42 trilioni mwaka 2025 kutoka Sh35 trilioni mwaka 2024, sawa na ukuaji wa asilimia 24.

Hata hivyo, pamoja na ongezeko la mikopo, amebainisha kiwango cha mikopo chechefu bado kiko katika hali inayodhibitiwa. 

“Mikopo chechefu imeongezeka kwa asilimia 2.78, kiwango ambacho bado kipo ndani ya ukomo wa kisheria wa asilimia tano,” ameeleza Luswetula.

Soko la hisa laongezeka 

Kwa upande wa sekta ndogo ya mitaji na dhamana, Luswetula amesema Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) limeendelea kukua ambapo kuonesha ukuaji idadi ya kampuni zilizosajiliwa katika soko hilo imefikia 28 huku mifuko ya uwezeshaji ikifikia 21.

Aidha, ameainisha kuwa thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji ilifikia Sh63.7 trilioni katika kipindi kilichoishia Desemba 2025.

“Jumla ya mauzo ya hisa na hati fungani katika soko la hisa la Dar es Salaam yamefikia Sh6.87 trilioni vilevile thamani ya mifuko ya uwekezaji wa pamoja ilifikia Sh4.35 trilioni katika kipindi hicho,” ameongeza Luswetula.

Fahamu mahitaji ya usingizi kwa watoto wachanga

  • Usingizi ni muhimu sana kwa ukuaji wa mwili na akili ya mtoto.

Dar es Salaam. Usingizi ni miongoni mwa mahitaji muhimu kwa binadamu, hususan watoto wachanga katika miaka miwili ya mwanzo ya maisha yao.

Tofauti na watu wazima, watoto huhitaji muda mwingi zaidi wa kulala ili kuwawezesha kukua vizuri na kuimarisha uwezo wa ubongo kufanya kazi kwa ufanisi.

Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya afya ya Stanford Medicine Children’s Health, watoto wachanga huhitaji hadi saa 17 za usingizi kwa siku, ambazo hugawanyika katika vipindi mbalimbali.

“Ratiba ya usingizi wa mtoto ni muhimu sana kwa ukuaji wake wa mwili, maendeleo ya akili (kumbukumbu, kujifunza na umakini), udhibiti wa hisia, pamoja na ujuzi wa mwendo wa mwili,” inaeleza tovuti hiyo.

Tovuti hiyo inabainisha kuwa watoto wenye umri wa kuanzia siku moja hadi miezi mitatu ya mwanzo wanahitaji kulala wastani wa saa 16 hadi 17 kwa siku, lakini mara nyingi hawalali zaidi ya saa 1 hadi 2 kwa wakati mmoja.

Aidha, watoto wenye umri wa miezi minne hadi 12 wanahitaji kulala wastani wa saa 12 hadi 16 kwa siku, huku wale wenye umri wa mwaka mmoja hadi miaka miwili wakihitaji kulala kati ya saa 11 hadi 14 kwa siku.

Tanzania kinara idadi ya Simba Afrika

Shirika la World Population Review limeitaja Tanzania kuwa na simba 14,500 idadi inayoifanya kuwa kinara wa idadi kubwa ya Simba barani Afrika.

Katika mbuga zake za kitaifa na mapori ya akiba nchini Tanzania, unaweza kuona simba jike wakiwinda alfajiri, madume wakinguruma na wengine wakiwinda au kupumzika katika vivuli vya miti.

Unaweza kujionea wanyama hao katika hifadhi mbalimbali ikiwemo Serengeti, Ngorongoro, Tarangire na Ruaha.

Hata hivyo, takwimu hizo zinatofautiana na zile zilizotolewa na IUCN pamoja na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) ambao waliripoti idadi ya simba hao kuwa 17,000.

Nchi nyingine yenye idadi kubwa ya simba ni Afrika Kusini (Simba 3,284), Botswana (Simba 3,063), Kenya (Simba 2,515) na Zambia (Simba 2,500)

Pamoja na hayo, Tawiri ilibainisha kuwa Tanzania imeongoza barani Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya wanyama wengine ikiwemo Nyati na Chui.


Fahamu faida za kutumia mifumo rasmi ya fedha

Dar es salaam: Matumizi ya mifumo rasmi ya fedha ni nguzo muhimu katika kuimarisha ustawi wa kifedha wa mtu mmoja mmoja na maendeleo ya uchumi ya Taifa kwa ujumla.

Kupitia mifumo hiyo, ikiwemo benki, taasisi za fedha zilizosajiliwa na huduma za bima wananchi hupata usalama wa fedha zao, uwazi wa miamala na ufuatiliaji sahihi wa mapato na matumizi. 

Kwa mujibu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mifumo rasmi hupunguza hatari ya wizi, upotevu wa fedha na ulaghai, huku ikirahisisha malipo ya huduma mbalimbali kama ada, kodi na mishahara kwa njia salama na za haraka.

Aidha, akiba inayowekwa kwenye mifumo rasmi inalindwa kisheria, hupata riba, na hujenga historia ya kifedha (credit history) ambayo humwezesha mhusika kupata mikopo kwa ajili ya uwekezaji, biashara au mahitaji ya kijamii.

Kwa ujumla, kutumia mifumo rasmi ya fedha ni msingi muhimu wa ukuaji endelevu wa uchumi, unaochochea uwajibikaji, ufanisi na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Follow us on TikTok

Nukta Habari

FOLLOW NOW
Subscribe to our channel

Nukta TV

SUBSCRIBE NOW
Mwenendo wa deni la serikali

Mwenendo wa deni la serikali

Nukta TV

Rais Samia: Uchumi wa nchi unapanda , lakini ukifika kwa watu hali si nzuri

Rais Samia: Uchumi wa nchi unapanda , lakini ukifika kwa watu hali si nzuri

Nukta TV

Gavana Tutuba afichua kiasi cha dhahabu kilichopo BoT thamani yake

Gavana Tutuba afichua kiasi cha dhahabu kilichopo BoT thamani yake

Nukta TV