Vyakula vya kuepuka kujilinda na ugonjwa ya figo

  • Ni pamoja na vyakula vyenye kiasi kikubwa cha protini, chumvi na kalsiamu.

Dar es Salaam. Ugonjwa wa figo ni miongoni mwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanayozidi kuongezeka duniani, yakichangia vifo vya mamilioni ya watu duniani kote.

Takwimu zinaonesha asilimia saba ya Watanzania wanaugua ugonjwa sugu wa figo, ukiwathiri zaidi wakazi wa mjini kwa asilimia 15 kulinganisha na asilimia mbili za wakazi wa vijijini.

Awali ugonjwa huu uliripotiwa zaidi kwa wazee wenye umri wa zaidi miaka 45, lakini miaka ya hivi karibuni maradhi hayo yamekuwa yakishambulia watu wa rika zote ikichangiwa zaidi na mtindo mbovu wa maisha.

Vifuatavyo ni vyakula na vinywaji ambavyo vinatakiwa kuepukwa au kupunguzwa ili kujilinda na ugonjwa wa figo.

Vyakula vyenye mafuta mengi

Ulaji uliopitiliza wa mafuta mengi, hasa yale mabaya (saturated fats), huongeza mzigo na kuzorotesha afya ya figo.

Mafuta haya hupatikana zaidi kwenye bidhaa kama siagi na samli pamoja  na aina nyingine za mafuta ya mbegu yasiyo salama.

Mratibu wa Tiba na Magonjwa Yasiyoambukiza katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Dk Omari Mwangaza, anasisitiza umuhimu wa wananchi kuzingatia aina ya mafuta wanayotumia katika mapishi yao ya kila siku.

“Mafuta mazuri ni yale yenye omega-3, omega-6 au omega-9, ikiwa mafuta yako hayana hizo yana madhara,” anaeleza Dk Mwangaza.

Omega -3 ni mafuta ambayo yanapatika kwenye vyakula kama samaki wa bahari, 0mega-6 (alizeti) na omega-9 (mzaituni na  parachichi) yakisaidia kulinda afya ya moyo na kuboresha ustawi wa mwili kwa ujumla.

Vyakula vyenye chumvi (sodium) nyingi

Madini ya sodium yana jukumu la kudhibiti kiwango cha maji mwilini. Hata hivyo, yakizidi huweza kusababisha maji kubaki mwilini na kuleta madhara kama vile kuvimba kwa mwili, shinikizo la damu, uzito kuongezeka ghafla na matatizo ya kupumua.

Vyakula vyenye sodium nyingi ni pamoja na nyama iliyohifadhiwa kwa chumvi, samaki waliokaushwa kwa chumvi, soseji na ‘bacon’ ambazo wataalamu wa afya wanazitaja kuwa chanzo cha magonjwa ya figo.

Dk Mwangaza ameshauri  kudhibiti  vyakula vya chumvi kwa sababu milli ya watu wenye asili ya kiafrika huwa na mwitikio mkubwa zaidi katika matumizi ya chumvi na sukari 

Mtaalamu huyo wa afya amewarai Watanzania kujenga tabia ya kutoongeza chumvi mezani wakati wa kula chakula.

Unywaji wa maji/vinywaji venye sukari kupitiliza

Ingawa maji ni muhimu kwa mwili, kunywa kupita kiasi kunaweza kuwa na madhara hata kwa watu wenye figo zenye afya. 

Figo hufanya kazi ya kusafisha damu na kudhibiti maji na madini mwilini, na unywaji wa maji mengi huongeza mzigo na kupunguza ufanisi wa kawaida.

Tovuti ya Medical News Today inasema kuwa mbali na madhara ya moja kwa moja katika figo, unywaji wa maji mengi unaweza kushusha kiwango cha sodiamu kwenye damu (hyponatremia),kusababisha uchovu, maumivu ya kichwa,au matatizo ya fahamu kwa muda mfupi. 

Mbali na maji, Dk Mwangaza anaeleza kuwa unywaji wa vimiminika vingine vyenye sukari ikiwemo pombe zenye sukari kupitiliza huchochea uzalishaji wa sukari isiyohitajika kwenye mwili wa binadamu jambo linaloweza kumletea mtumiaji matatizo ya figo.

@jikopointtanzania

Sukari pombe ni aina ya sukari inayojulikana kisayansi kama Sugar alcohol au polyols. Ni kundi la vitu vya kemikali vinavyofanana na sukari lakini vina muundo unaofanana kidogo na pombe (alcohol) katika kemia. Jina ‘pombe’ hapa halimaanishi pombe ya kulewesha kama Ethanol. Ni neno la kemia tu kutokana na muundo wake. Mifano ya sukari pombe Baadhi ya aina zinazojulikana ni: Xylitol Sorbitol Maltitol Erythritol Zinatumika wapi? Sukari pombe hutumiwa sana katika: vyakula vya “sugar-free” au “no added sugar” pipi vinywaji vya diet baadhi ya dawa na dawa za meno SukariPombe SugarAlcohol Polyols Lishe Afya SugarFree Sweeteners Nutrition HealthyEating DiabetesCare#wafanyabiasharatanzania #soko #love #tende

♬ original sound – JikoPoint – JikoPoint

Vyakula vyenye protini nyingi

Protini inapovunjwa vunjwa mwilini hutengeneza mabaki kama vile urea, amonia na ‘creatinine’.

Kwa mtu mwenye matatizo ya figo, mabaki haya huweza kuongezeka na kuathiri zaidi utendaji wa figo.

Hivyo ni muhimu kupunguza ulaji wa protini nyingi na kuchagua protini zinazotumiwa kwa ufanisi zaidi na mwili, kama vile mayai, samaki, nyama, kuku, maziwa na jibini.

Vyakula vyenye protini ambazo huacha mabaki mengi ni pamoja na mbogamboga, matunda, maharage, kunde, mbaazi, mahindi, mtama, karanga, mkate.

Bei ya maharage yaendelea kuwa kichomi Dar es Salaam 

Dar es Salaam. Bei ya maharage imeendelea kuwa tulivu nchini kutokana na kutobadilika ndani ya wiki licha ya kuendelea kwa msimu wa mvua za masika katika maeneo mbalimbali nchini. 

Kwa kawaida msimu wa mvua za masika na kipindi cha mfungo wa Ramadhan na Kwaresma kama hiki, bei za bidhaa za vyakula hupaa kutokana na kuongezeka kwa mahitaji na kupaa kwa gharama za uchukuzi kwa sababu ya athari ya mvua kwenye miundombinu. 

Uchambuzi wa bei za jumla za mazao uliofanywa na Nukta Habari umebainisha kuwa kuwa bei hizo zimeendelea kuwa thabiti katika mikoa mbalimbali, huku tofauti kubwa ikionekana kati ya bei ya juu na ya chini.

Kwa mujibu wa takwimu za mazao makuu ya biashara zilizotolewa leo Machi 4, 2026, na Wizara ya Viwanda na Biashara, bei ya jumla ya gunia la kilo 100 la maharage imeendelea kuwa Sh400,000 katika soko la Mwananyamala, jijini Dar es Salaam sawa na bei iliyorekodiwa mapema wiki hii.

Kubaki juu kwa zao hilo kwa chakula kutaendelea kuwa mzigo kwa mlaji wa mwisho, huku wafanyabiashara wakinufaika na viwango hivyo vya juu.

Hata wakati Dar es Salaam wakinunua zao hilo kwa bei ya juu, Njombe wao ndo wananunua maharage kwa bei ya jumla ya chini zaidi nchini ambapo gunia la kilo 100 linauzwa kwa Sh110,000. Bei hiyo ya Njombe ni ya chini takriban mara 4 ya ile ya Dar es Salaam na imeendelea kubaki kama ilivyokuwa mwanzoni mwa wiki.

Aidha, bei hizo hazijaonyesha mabadiliko katika mkoa wa Kigoma, ambapo zinaendelea kutumika kama zilivyokuwa Jumatatu.

Tanga waendelea kutoboa mifuko bei ya mahindi

Kununua gunia la mahindi la kilo 100 mkoani Tanga itakulazimu kulipia Sh140,000 ambayo ni mara 2 na nusu ya bei ya chini iliyorekodiwa mkoani Njombe ya Sh55,600 kwa gunia la kilo 100.

Wakati wakazi wa mkoa huo wakilia na bei hiyo, hali ni tofauti kwa wakazi wa mkoani wa Dar es Salaam ambao wananunua gunia la kilo 100 za viazi mbatata/ mviringo kwa Sh60,000 ambayo ni ahueni kwa mara 3 zaidi ya ile iliyorekodiwa mkoani Tanga ya Sh180,000.

Sababu zinazoweza kuathiri uwezo wa mwanamke kupata ujauzito

  • Ni pamoja na kuziba kwa mirija ya uzazi,  na mzunguko usio sahihi wa hedhi na matatizo ya homoni.

Dar es Salaam. Utasa, au hali ya kushindwa kubeba ujauzito ni miongoni mwa changamoto zinazowakumba mamilioni ya wanawake duniani kote suala linalowakosesha furaha ya kuitwa mama.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linakadiria kuwa mtu mmoja kati ya watu wazima sita wenye uwezo wa kuzaa duniani hukumbwa na changamoto ya utasa katika kipindi fulani cha maisha yao.

Daktari Bingwa wa Uzazi na Magonjwa ya Wanawake katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk Benny Kimaro, ameiambia Nukta Habari kuwa miongoni mwa sababu kubwa ya utasa ni kuwa na mzunguko usioeleweka pamoja na uwiano usio sahihi wa homoni.

Kwa mujibu wa daktari huyo, mzunguko wa hedhi wa mwanamke unapaswa kuruhusu yai kuzalishwa kila mwezi lipevuke vizuri ili liweze kukutana  na mbegu ya kiume kwa ajili ya kutungisha mimba.

Uwezo wa kushika mimba unategemea ushirikiano wa mifumo kadhaa ya mwili wa mwanamke pamoja na ubora wa mbegu za mwanaume.

“Ili ujauzito upatikane, ni lazima yai lipevuke vizuri, mirija iwe wazi, kizazi kiwe katika hali nzuri na homoni ziwe katika uwiano sahihi,” anasema Dk Kimaro.

iwapo mzunguko wa hedhi ya mwanamke hauelewiki husababisha mayai ya mwanamke kutokukomaa kwa wakati  au yasitoke kabisa suala ambalo liinachangiwa zaidi na  mvurugiko wa homoni au ugonjwa wa PCOS (Polycystic Ovary Syndrome).

Fibroids (leiomyomas) hupatikana kwa asilimia 20-70 ya wanawake wakiwa na umri wa kuzaa. Picha/ Canva. 

Hitilafu katika mji wa mimba 

Mji wa mimba ni sehemu maalum ambayo mimba hujishikiza baada ya kutungwa na kuruhusu ukuaji wa mtoto kwa miezi tisa.

Hitilafu yoyote katika eneo hili ikiwemo fibroids (uvimbe usio wa saratani kwenye kizazi), unaojulikana pia kama myoma, pamoja na endometriosis, (tishu za kizazi hukua nje ya mfuko wa uzazi) huweza kusababisha mwanamke kushindwa kubeba mimba au kuharibika mara kwa mara.

Kuziba kwa mirija ya mfuko wa uzazi

Changamoto nyingine ni kuziba kwa mirija ya uzazi ambako kunasabishwa na maambukizi kama PID au magonjwa ya zinaa na kuzia urutubishaji na usafirishai wa yai kwenda katika mji wa mimba.

“Inapotokea changamoto katika swala zima la mirija ina maana basi makutano ya mbegu na yai hayawezi kufanyika. Changamoto hauwezi kupata ujauzito,” amesema Dk Kimaro.

Hata hivyo, Dk Kimaro ameongeza kuwa mwanamke mwenye mrija mmoja bado anaweza kupata ujauzito, ingawa inaweza kuchukua muda mrefu zaidi. 

Endapo mirija yote imeathirika, teknolojia ya uzazi wa kusaidiwa kama upandikizaji (IVF) inaweza kuwa mbadala. 

Uwezo wa kushika mimba unategemea ushirikiano wa mifumo ya homoni, mayai yenye afya, na mji wa mimba wa mwanamke, pamoja na mbegu bora za mwanaume. Picha/ Canva.

Mbegu bora za mwanaume zatajwa

Licha ya jamii mara nyingi kuelekeza lawama kwa mwanamke, Dk Benny Kimaro anaeleza kuwa takribani asilimia 30 hadi 35 ya changamoto za uzazi zinamhusu mwanaume. 

Anabainisha kuwa ubora wa mbegu za kiume hupimwa kwa kuangalia idadi, uwezo wa kusogea, pamoja na umbo lake . 

Mbegu inapaswa kuwa na kichwa chenye uwezo wa kupenya kwenye yai na mkia unaoiwezesha kusafiri kwa kasi kuelekea kulikopo yai, kasoro katika vigezo hivi hupunguza uwezekano wa urutubishaji.

Kitaalamu, mwanaume anatakiwa kuwa na angalau mbegu milioni 15 kwa kila mililita moja ya shahawa ili kuongeza uwezekano wa ujauzito.

Idadi au ubora duni wa mbegu hupunguza uwezekano wa yai kurutubishwa na kati ya mbegu hizo,ni mbegu moja tu (au mbili kwa mapacha) ndiyo hufanikiwa kurutubisha yai.

 Wataalamu wanashauri wanandoa wote wawili kufika kliniki pamoja kwa ajili ya vipimo na ushauri badala ya kumlaumu mmoja.

Ufahamu wa ugonjwa wa kula kupita kiasi unaoathiri maelfu kimya kimya

  • Mara nyingi hali hizi huambatana na hofu au wasiwasi uliopitiliza kuhusu uzito na umbo la mwili.

Dar es Salaam. Chakula ni miongoni mwa hitaji muhimu la kiumbe hai chochote ikiwemo binadamu kikimsaidia kuimarisha ukuaji na kumpa ustawi wa mwili na akili.

Licha ya umuhimu wake katika maisha  ya binadamu, kisipotumiwa kwa kiwango sahihi mtumiaji anaweza kuangukia kwenye changamoto ya ulaji ama ‘eating disorder’ inayoweza kudhoofisha mwili na kukaribisha magonjwa.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) changamoto ya ulaji ni tatizo la afya ya akili linalohusisha tabia zisizo za kawaida katika ulaji wa chakula, mara nyingi zikiambatana na hofu au wasiwasi mkubwa kuhusu uzito na mwonekano wa mwili. 

Ugonjwa huo wa kula umegawanyika katika makundi mbalimbali ikiwemo ‘binge eating disorder’ na ‘bulimia nervosa’, ambayo yote yanahusisha ulaji kupita kiasi.

WHO inabainisha kuwa mwaka 2021 takribani watu milioni 16 duniani walikumbwa na moja ya hali hizo ikiwemo watoto na vijana milioni 3.4 .

Miongoni mwa dalili za changamoto hii ni ulaji wa  chakula kingi zaidi ya kiwango cha kawaida katika muda mfupi. Picha/ Canva.

Wataalamu wa afya waeleza chanzo

Daktari wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Rufaa ya Bombo mkoani Tanga, Dk Idi Mgaya, anafafanua kuwa chanzo cha tatizo hili si rahisi kubainika moja kwa moja.

“Ugonjwa wa kula kupita kiasi mara nyingi hauna chanzo kimoja cha moja kwa moja. Ni changamoto inayohusisha mwingiliano wa sababu za kibaiolojia, kisaikolojia na kijamii. Wakati mwingine unaweza kuchangiwa na vinasaba au mazingira,” amesema Dk Mgaya.

Dk Mgaya ameongeza kuwa wanao athirika zaidi ni vijana kuanzia umri wa miaka 18 ambao mara nyingi hukigeuza chakula kuwa njia ya kupata nafuu ya kihisia na furaha inayowapa ahueni ya kiakili.

WHO inabainisha kuwa licha ya ahueni hiyo wagonjwa hao hupitia msongo mkubwa wa mawazo na kuvurugika kwa utendaji wa kila siku, ikiwemo kushindwa kuzingatia masomo au kazi, pamoja na kuathirika kwa mahusiano ya kijamii.

Takribani asilimia 1 hadi 2 ya wanawake na chini ya asilimia 1 ya wanaume huathirika na ugonjwa huu wa kula kupita kiasi. Picha Canva

Matibabu

Matibabu ya ugonjwa wa kula kupita kiasi mara nyingi huhusisha tiba ya kisaikolojia, hususan Cognitive Behavioral Therapy (CBT), inayolenga kubadili mitazamo na tabia zisizo sahihi.

Kutibu ugonjwa huu, kunahitaji kufanya kazi kwa ushirikiano na timu ya wataalamu wa afya na afya ya akili wenye utaalamu wa kutibu aina hii ya tatizo la ulaji. 

Ingawa watalaamu hao hawajaainisha ni muda kiasi gani mtu anaweza kupona huenda ikawa ni miezi, mwaka au miaka kutegemea na hali ya mgonjwa.  

Mtu mwenye changamoto hii hula kupita kiasi na hata akitapika hurejea kuendelea kula. Picha/ Canva.

“Tiba huanza pale mgonjwa anapojitambua kuwa ana tatizo. Kupitia CBT, tunamshirikisha mgonjwa katika kuchunguza tabia zake, kumpa majukumu maalum ya kubadili mtazamo na kumjengea uwezo wa kudhibiti hisia zake,” amesisitiza Dk Mgaya.

Wataalamu wanashauri kuwa jamii iongeze uelewa kuhusu matatizo ya afya ya akili ili kupunguza unyanyapaa na kuwahamasisha wahanga kutafuta msaada mapema.

Ugonjwa wa kipindupindu, kuharisha ulivyowatesa Watanzania mwaka 2025

  • Ugonjwa wa kuharisha ulikuwa ni ugonjwa ama hali iliyoripotiwa zaidi mwaka 2025 katika mikoa yote ya Tanzania

Dar es Salaam. Huenda Watanzania wakatakiwa kuchukua tahadhari za kiafya zaidi ili kujikinga na magonjwa ya kipindupindu na kuharisha ambayo takwimu za hivi karibuni za Wizara ya Afya zinayataja kuwasumbua zaidi wananchi mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kuharisha ni hali ya kiafya inayohusisha kujisaidia choo chepesi zaidi kuliko kiwango cha kawaida kwa zaidi ya mara tatu kwa siku, hali ambayo huchangiwa zaidi na maambukizi ya bakteria na virusi vinavyoathiri mfumo wa mmeng’enyo wa chakula.

Wakati mwingine kuharisha, hutajwa kuwa miongoni mwa dalili za ugonjwa wa kipindupindu unaosababishwa na bakteria aitwaye Vibrio cholerae, ambao kwa miaka ya nyuma ulitajwa kuchangia idadi kubwa ya vifo.

Takwimu za Mfumo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Udhibiti wa Magonjwa (IDSR), zilizotolewa Februari 2, 2026 na Wizara ya Afya zinabainisha kuwa karibu nusu ya visa vyote 369,864 vya magonjwa yanayoripotiwa nchini vinatokana na ugonjwa wa kuharisha.

Visa 176,797 vilihusishwa na magonjwa ya kuharisha, sawa na asilimia 47.8 ya visa vyote vilivyoripotiwa katika robo ya kwanza na ya pili ya mwaka 2025.

Kila mtu hupata kuhara mara kwa mara, lakini inapodumu zaidi ya wiki nne, huchukuliwa kuwa kuhara sugu. Picha/ Gastro florida.

Takwimu hizo zinaonesha kuwa karibu mgonjwa mmoja kati ya wawili waliokwenda katika vituo vya afya alikuwa anakabiliwa na tatizo la kuharisha kutoka mikoa yote 26 ya Tanzania Bara.

Miongoni mwa mikoa iliyoongoza kwa visa vingi vya kuharisha ni Dodoma yenye visa 13,770 (asilimia 7.8), ikifuatiwa na Mara visa 13,622 (asilimia 7.7), Morogoro visa 11,879 (asilimia 6.7) na Rukwa visa 11,494 (asilimia 6.5). 

Mwezi wa Mei uliongoza kwa idadi kubwa ya visa, ambapo viliripotiwa visa 78,496 sawa na asilimia 21.2  ya visa vyote ikichangia vifo 33.

Mbali na Kuharisha kipindupindu pia kiliwatesa Watanzania mwaka 2025, visa 3,433  na vifo 26, sawa na asilimia 78.8 ya vifo vyote vikiripotiwa.

Nimonia, ‘typhoid’ pasua kichwa

Ripoti ya Wizara ya Afya inayataja magonjwa mengine yaliwasumbua Watanza ndani ya mwaka 2025 kuwa ni ugonjwa wa nimonia ambapo visa 133,310 vilirekodiwa ikifuatiwa na homa ya matumbo (typhoid) uliokuwa na visa 31,760.

Pneumonia ni maambukizi ya papo hapo ya njia ya hewa yanayohusisha alveoli na njia za hewa za mbali. Picha/ Dr J Suri.

Pia, kulikuwa na visa 12,062 vya kung’atwa na wanyama na visa 6,183 vya kung’atwa na nyoka, maambukizi makali ya njia ya hewa (SARI) yalishika nafasi ya sita kwa visa 4,213 pamoja na vifo saba vilivyoripotiwa.

Homa ya dengue pia yenye visa 84 na kichaa cha mbwa (rabies) kilichokuwa na visa 25 kiliingia katika orodha hiyo ya magonjwa 10 yaliyowatesa Watanzania suala linaloacha mzigo mkubwa wa udhaifu wa mwili kwa wananchi.

Ufaulu kidato cha nne unavyopanda na kushuka Tanzania

  • Takwimu zinaonesha ufaulu unashuka na kuongezeka  mwaka hadi mwaka katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021.

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta) limetangaza matokeo ya mitihani ya kidato cha nne iliyofanyika Novemba, 2025, ambapo ufaulu umeongezeka kidogo kulinganisha na miaka iliyopita.

Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Dk. Said Mohamed aliyekuwa akitangaza matokeo hayo jijini Dar es Salaam leo Januari 31, 2026 amesema kuwa ufaulu wa wanafunzi kwa kidato cha nne kwa mwaka 2025 ni asilimia 92.37. 

Uchambuzi uliofanywa na Nukta Habari unaonyesha kuwa ufaulu wa kidato cha nne umekuwa ukipanda na kushuka kwa miaka tofauti katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021.

Takwimu zinaonyesha kiwango cha ufaulu kiliongezeka kwa asilimia 0.67 na kufikia asilimia 87.79 mwaka 2022 kutoka asilimia 87.30 iliyorekodiwa mwaka 2021. Hata hivyo, ufaulu huo ulishuka kwa asilimia 0.32 na kufikia asilimia 87.65 mwaka 2023.

Ongezeko thabiti la matokeo ya kidato cha nne limeonekana kuanzia mwaka 2024 ambapo ufaulu uliongezeka kwa takriban asilimia 4.72 na kufikia asilimia 92.37.

Aidha, katika kipindi cha miaka mitano wavulana ndio wanaongoza kwa kuwa na ufaulu wa juu zaidi ya wasichana wakiwa na wastani wa ufaulu wa asilimia 92.75 wakiwaacha mbali wasichana wenye wastani wa asilimia 90.71.

WHO yatoa mwongozo mpya wa lishe mashuleni kudhibiti unene uliopitiliza

  • Takribani watoto na vijana milioni 188 wa umri wa kwenda shule waliishi na unene uliopitiliza 2025.
  • Ni nchi 48 pekee kati ya 408 zilizo na sera zinazozuia matangazo ya vyakula visivyofaa kwa watoto.

Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO) limetoa mwongozo mpya wa kimataifa wa lishe mashuleni, unaoziitaka nchi wanachama kuimarisha mazingira ya lishe shuleni ili kudhibiti ongezeko la unene uliopitiliza na kukabiliana na changamoto ya utapiamlo kwa watoto.

Uzito au unene uliopitiliza hufafanuliwa kama mkusanyiko usio wa kawaida au wa kupita kiasi wa mafuta mwilini ambao unaweza kuweka afya hatarini ikichangiwa zaidi na mtindo mbovu wa maisha, ulaji usiozingatia kanuni za afya na tabia bwete.

Takwimu za WHO zinakadiria kuwa mwaka 2024 takribani watoto milioni 35 walio chini ya umri wa miaka mitano duniani kote walikuwa na uzito uliopitiliza suala linaloweka afya zao rehani.

Hali ni mbaya zaidi kwa watoto na vijana milioni 188 wenye umri wa kwenda shule ambao waliripotiwa na WHO kuwa na unene uliopitiliza, sawa na mtoto mmoja kati ya 10, idadi iliyozidi kwa mara ya kwanza watoto wenye uzito pungufu.

WHO inapendekeza shule ziweke kanuni za lazima zitakazohamasisha upatikanaji wa vyakula vyenye afya. Picha/Canva.

Kutokana na uwepo wa changamoto hiyo, January 27, 2026, WHO ilitoa mwongozo wa lishe mashuleni utakaohakikisha vyakula na vinywaji vinavyotolewa shuleni, pamoja na vinavyopatikana katika mazingira yanayozunguka shule, ni vyenye afya na lishe bora.

“Uzito kupita kiasi na unene uliokithiri kwa watoto vinaendelea kuongezeka duniani, huku utapiamlo bado ukiwa changamoto ya kudumu. Shule ziko mstari wa mbele katika kukabiliana na mzigo huu maradufu wa utapiamlo,” inaeleza sehemu ya taarifa ya WHO.

Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dk Tedros Adhanom Ghebreyesus aliyekuwa akizunngumza alisema kuwa lishe shuleni ina athari ya moja kwa moja katika afya na maendeleo ya watoto.

“Chakula ambacho watoto hula shuleni kinaweza kuathiri uwezo wao wa kujifunza na kuwa na madhara ya muda mrefu kwa afya na ustawi wao. Lishe sahihi shuleni ni msingi wa kuzuia magonjwa baadaye maishani,” alisema.

Takribani mtoto mmoja kati ya 10 duniani ana unene uliopitiliza. Shule zinaweza kuwa sehemu ya kutatua tatizo hili. Picha/ Canva.

Katika muktadha wa kitaifa, baadhi ya nchi ikiwemo Tanzania, tayari zina miongozo ya chakula cha shule inayolenga kuboresha lishe kwa wanafunzi kupitia Mpango wa Taifa wa Chakula Shuleni (NSFG).

Mpango huo unazingatia Sera ya Afya ya mwaka 2007, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na Mpango wa Taifa wa Sekta Jumuishi wa Miaka Mitano wa Utekelezaji wa Lishe 2016/17 hadi 2020/2.

Kwa mujibu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, utoaji wa huduma za chakula shuleni huchangia kuboresha afya ya wanafunzi, kupunguza utoro, kuongeza usikivu darasani na kuinua kiwango cha ufaulu.

WHO inakadiria kuwa zaidi ya watoto milioni 466 duniani hupata chakula kupitia programu za chakula shuleni jambo linaloimarisha afya ya akili na kuimarisha uwezo wao wa kimasomo.

Kuongeza vyakula vyenye afya na kupunguza vyenye sukari na mafuta yasiyo na afya ni hatua muhimu ya kuwalinda watoto. Picha/ Canva.

Hata hivyo, shirika hilo linaonya kuwa bado kuna upungufu wa taarifa kuhusu ubora wa lishe ya chakula hicho, hali inayoweza kusababisha changamoto za kiafya.

Katika mwongozo wake mpya, WHO inapendekeza shule ziweke kanuni za lazima zitakazohamasisha upatikanaji wa vyakula vyenye afya na kupunguza matumizi ya vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi na mafuta yasiyo na afya, pamoja na kudhibiti mbinu za kibiashara zinazowalenga watoto.

Kwa sasa, nchi 104 zina sera za chakula chenye afya mashuleni huku karibu robo tatu zikiwa na vigezo vya lazima vya kuongoza muundo wa chakula cha shule huku nchi 48 pekee zikizuia matangazo ya vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi au mafuta yasiyo na afya.

Sekta ya fedha inavyoimarika Tanzania

  • Ukuaji huo umejidhihirisha kupitia ongezeko la idadi ya benki, taasisi za huduma ndogo za fedha, mawakala wa benki pamoja na rasilimali za kibenki.

Dar es Salaam. Katika siku za hivi karibuni, sekta ya fedha nchini Tanzania imeendelea kuonesha mwelekeo chanya wa ukuaji, ikichochewa na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi, upanuzi wa taasisi za kifedha na kuimarika kwa imani ya wananchi katika mifumo rasmi ya fedha. 

Ukuaji huo umejidhihirisha kupitia ongezeko la idadi ya benki, taasisi za huduma ndogo za fedha, mawakala wa benki pamoja na rasilimali za kibenki, hali inayoashiria kuimarika kwa mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula aliyekuwa akizungumza Januari 21, 2025 katika uzinduzi maadhimisho ya kitaifa ya wiki ya huduma ya fedha, amesema hadi kufikia Septemba 2025, Tanzania ilikuwa na jumla ya benki za kibiashara 35, benki za kijamii mbili, benki za maendeleo mbili pamoja na benki tatu za huduma ndogo za fedha. 

Aidha, taasisi 2,811 za huduma ndogo za fedha pamoja na vikundi vya kijamii vya huduma ndogo za fedha 70,913 zilisajiliwa, huku taasisi mbili za ubadilishanaji wa fedha zikiongeza idadi ya watoa huduma rasmi nchini.

Aidha, Luswetula ameeleza kuwa upanuzi huo umeenda sambamba na ongezeko kubwa la mawakala wa benki nchini. Ambapo Idadi ya mawakala wa benki imeongezeka kutoka 106,176 hadi kufikia 145,430, jambo linalorahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha hadi ngazi ya jamii.

Mbali na ongezeko la taasisi, rasilimali za kibenki nazo zimeendelea kuimarika na kufikia Sh71.8 trilioni Septemba 2025, ikilinganishwa na Sh62.2 trilioni zilizorekodiwa Septemba 2024.

Aidha, katika kipindi kama hicho, amana za benki zimeongezeka hadi Sh50.2 trilioni kutoka Sh42.7 trilioni mwaka uliotangulia, hatua inayotafsiriwa kama ishara ya kuongezeka kwa imani ya wananchi katika sekta ya fedha.

Katika maelezo yake, Luswetula pia amebainisha kuwa mikopo kwa sekta binafsi imekua kwa kasi kubwa. Ikiongezeka na kufikia Sh42 trilioni mwaka 2025 kutoka Sh35 trilioni mwaka 2024, sawa na ukuaji wa asilimia 24.

Hata hivyo, pamoja na ongezeko la mikopo, amebainisha kiwango cha mikopo chechefu bado kiko katika hali inayodhibitiwa. 

“Mikopo chechefu imeongezeka kwa asilimia 2.78, kiwango ambacho bado kipo ndani ya ukomo wa kisheria wa asilimia tano,” ameeleza Luswetula.

Soko la hisa laongezeka 

Kwa upande wa sekta ndogo ya mitaji na dhamana, Luswetula amesema Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) limeendelea kukua ambapo kuonesha ukuaji idadi ya kampuni zilizosajiliwa katika soko hilo imefikia 28 huku mifuko ya uwezeshaji ikifikia 21.

Aidha, ameainisha kuwa thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji ilifikia Sh63.7 trilioni katika kipindi kilichoishia Desemba 2025.

“Jumla ya mauzo ya hisa na hati fungani katika soko la hisa la Dar es Salaam yamefikia Sh6.87 trilioni vilevile thamani ya mifuko ya uwekezaji wa pamoja ilifikia Sh4.35 trilioni katika kipindi hicho,” ameongeza Luswetula.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks