Fahamu faida za ulaji wa brokoli
- Ni pamoja na kuzuia ugonjwa wa moyo na kuimarisha afya ya mifupa kulingana na uwepo wa nyuzi nyuzi na vitamini.
- Kusaidia mmeng’enyo wa chakula na matatizo ya kiungulia.
Dar es Salaam. Kuna aina za nyingi za mbogamboga na kila moja ina faida zake katika mwili wa binadamu ikiwemo kuimarisha kinga mwilini.
Pamoja na wingi wa mboga hizo, kila moja ina faida zake mahususi ambazo unaweza usizipate katika aina nyingine za mboga au ukazipata kwa uchache.
Katikati ya aina hizo za mboga ipo brokoli, mboga maarufu inayosifika kwa faida nyingi za kiafya ikiwemo wingi wa kirutubisho adimu cha vitamini K ambacho hakipatikani kwenye mboga nyingi.
“Ni miongoni mwa mmea wenye vitamini C nyingi, vitamini K ambayo ni ‘very rare’ (adimu sana) kuipata. Vitamini K inapatikana kwenye vyakula vichache, ina madini ya chuma, vitamini D, A.
…Lakini pia ina madini mengi ina kalsium, magnesium, potassium,” amesema Irine Kweka, Afisa Lishe kutoka Hospitali ya Kondoa jijini Dodoma.
Hata hivyo, Kweka ameongeza kuwa sifa kubwa ya brokoili uwepo wa antioxidanti nzuri kulingana na uwepo wa vitamini.
Kwanini ule brokoli?

Ikiwa bado unajiuliza sababu za kuongeza brokoli katika mlo wako wa kila siku Kweka aliyekuwa akizungumza na Nukta Habari amebainisha kuwa moja aya faida ya kutumia mboga hiyo katika mlo ni kusaidia mmeng’enyo wa chakula kulingana na wingi wa nyuzinyuzi.
Nyuzi nyuzi hizo pia husaidia tatizo la choo kigumu, kudhibiti kiwango cha asidi kwenye tumbo, kukabiliana na kiungulia au vidonda vya tumbo,pamoja na kuongeza idadi ya bakteria wazuri tumboni, ambao ni muhimu kwa usagaji bora wa chakula.
Bakteria hawa husaidia kuvunjavunja chakula kwa ufanisi na pia huchangia katika afya bora ya kinga ya mwili.
Kuzuia magonjwa ya moyo
Ulaji wa Brokoli husaidia kupunguza viwango vya lehemu (cholesterol) mbaya (LDL) na kuongeza lehemu nzuri (HDL), hali inayosaidia kupunguza hatari ya kupata magonjwa ya moyo.
Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya afya, Medical News Today brokoli ina nyuzi nyuzi, antioksidanti, na kemikali za kibaolojia zinazopunguza kiwango cha ehemu na kudumisha utendaji mzuri wa moyo.

Uwepo wa nyuzi nyuzi hizo kwa wingi, husaidia kuzuia kuziba kwa mishipa ya damu kwa kupunguza kiasi cha mafuta mabaya mwilini hali inayoweza kupunguza uwezekano wa kupata shinikizo la damu, kiharusi, na mshtuko wa moyo.
Kuimarisha afya ya mifupa
Tovuti ya Naturmed Scientific inaeleza kuwa mifupa yenye nguvu inahitaji virutubisho muhimu kama vile kalsiamu, fosforasi, na vitamini K, vyote ambavyo hupatikana kwa wingi katika brokoli.
Vitamini K inasaidia katika mgandisho wa damu na pia huchangia uimarishaji wa madini kwenye mifupa, jambo ambalo linapunguza uwezekano wa mifupa kuwa dhaifu au kuvunjika kwa urahisi.

Mifupa yenye nguvu inahitaji virutubisho muhimu kama vile kalsiamu, fosforasi, na vitamini K ambavyo pia hupatikana kwenye brokoli. Picha/ La Muscle.
Pia, brokoli ina kiasi kikubwa cha madini ya magnesiamu na zinki, hali inayowafanya walaji wa brokoli kupunguza msongamano wa mifupa (osteoporosis), unaochangia mifupa kuwa dhaifu na rahisi kuvunjika.
Kinga dhidi ya saratani
Taasisi ya kansa ya nchini Marekani (National Cancer Institute) inabainisha kuwa brokoli ina kemikali zinazozuia ukuaji wa seli zenye uwezo wa kusababisha saratani.
Tafiti mbalimbali zimeonesha kuwa ulaji wa mara kwa mara wa mboga za jamii ya ‘cruciferous’, ikiwemo brokoli, unaweza kupunguza hatari ya saratani ya matiti, saratani ya tezi dume, na saratani ya utumbo mpana.

Mbali na kinga dhidi ya saratani, brokoli pia inasaidia wagonjw wa saratani kupunguza madhara yanayotokana na matibabu kama mionzi na dawa za kemikali.
Kuimarisha afya ya ngozi
Ngozi yenye afya inahitaji lishe bora, na brokoli ni moja ya vyakula vinavyotoa virutubisho muhimu kwa ngozi.
Vitamini C inayopatikana kwa wingi kwenye brokoli inasaidia mwili kutengeneza collagen, ambayo ni protini muhimu kwa uimara na mng’ao wa ngozi.

Brokoli pia ina vioksidishaji vinavyosaidia kupunguza athari za miale ya jua ambayo inaweza kusababisha uharibifu wa ngozi huku vitamini A na E, vilivyopo katika mboga hiyo ambavyo vikiifanya ngozi kuwa naunyevu wa kutosha.
Kudhibiti sukari ya damu
Kwa watu wenye ugonjwa wa kisukari, brokoli ni moja ya vyakula vinavyopaswa kujumuishwa katika lishe. Ina misombo inayosaidia kudhibiti viwango vya sukari kwenye damu kwa kupunguza upinzani wa insulini.
Uwepo wa sulforaphane inayopatikana kwenye brokoli inaweza kusaidia kupunguza viwango vya sukari kwa wagonjwa wa kisukari aina ya pili.

Sulforaphane husaidia kongosho kutoa insulini kwa ufanisi zaidi na hivyo kudhibiti sukari mwilini.
Mbali na hayo, nyuzinyuzi zilizopo kwenye brokoli husaidia kupunguza kasi ya mmeng’enyo wa wanga, na hivyo kuzuia kuongezeka kwa ghafla kwa kiwango cha sukari baada ya kula.
Hii ni muhimu kwa watu wanaotaka kudhibiti uzito na kuepuka hatari ya kupata kisukari.
Kusaidia kuzuia mchakato wa kuzeeka
Mchakato wa kuzeeka kwa kiasi kikubwa unahusishwa na mkazo wa oksidativi na kupungua kwa kazi ya kimetaboliki wakati wa maisha ya binadamu.
Ingawa kuzeeka ni mchakato wa asili usioepukika, ubora wa lishe unadhaniwa kuwa na mchango mkubwa katika kuamua jinsi jeni zinavyotumika na maendeleo ya magonjwa yanayohusiana na umri

Ili kuhifadhi virutubisho vyake, ni vyema kupika brokoli kwa muda mfupi kwa kutumia njia kama kuipika kwa mvuke au kuitumia katika saladi. Kwa kuongeza brokoli katika lishe yako ya kila siku, unaweza kufurahia afya bora na kuzuia magonjwa mbalimbali.
Ifahamu eSim, faida na changamoto zake
- Ni teknolojia inayokuwezesha kutumia mtandao bila kuweka laini ya simu.
- Hupunguza hatari ya kupoteza taarifa muhimu kwa kupoteza au kuibiwa laini ya simu.
Dar es Salaam. Teknolojia ya mawasiliano inaendelea kupiga hatua kubwa tangu uvumbuzi wa kadi za SIM miaka ya 1990.
SIM ni kifupi cha Subscriber Identity Module, ambayo ni kadi maalum inayotumika kuhifadhi taarifa za mtumiaji wa mtandao wa simu, ikiwa ni pamoja na namba ya simu, mawasiliano, na hati za utambulisho za mtandao.
SIM inaruhusu simu kuunganishwa na mtandao wa mtoa huduma, ikimpa mtumiaji uwezo wa kupiga simu, kutuma ujumbe, na kutumia data za intaneti.
Hapo zamani, tulianza laini kubwa za simu zilizojulikana kama Full-size SIM, ambazo baadaye zilipunguzwa hadi Mini-SIM, kisha Micro-SIM na hatimaye Nano-SIM ambazo ndizo zinazotumika sana kwa sasa.
Kila hatua ya mabadiliko haya ililenga kupunguza ukubwa wa kadi ya SIM ili kutoa nafasi zaidi ndani ya simu kwa vifaa vingine muhimu kama vile betri kubwa na vifaa vya mawasiliano.

Hata hivyo, pamoja na kupungua kwa ukubwa wa SIM, hitaji la kubadilisha laini kwa mikono lilikuwa bado kikwazo.
Hapo ndipo teknolojia ya eSIM ilipoibuka, ikiwa suluhisho la kidigitali linalomwezesha mtumiaji kubadili mtandao bila hitaji la kubadilisha kadi ya SIM kwa mikono.
eSIM ni nini?
eSIM, au “Embedded SIM,” ni kadi ya SIM ya kidigitali ambayo imejengewa moja kwa moja ndani ya simu au kifaa kingine cha mawasiliano.
Tofauti na laini za kawaida zinazoweza kuondolewa na kubadilishwa, eSIM inafanya kazi kupitia programu maalum inayoruhusu mtumiaji kusajili na kubadili mitandao kwa urahisi bila kutumia kadi halisi.
Teknolojia hii inaleta mapinduzi katika sekta ya mawasiliano kwa kuondoa hitaji la kubeba na kubadilisha laini za plastiki kila mara unapotaka kutumia mtandao tofauti.

Kwa Tanzania, huduma ya eSIM inapatikana kwa sasa kupitia mitandao ya Vodacom, Tigo, Airtel, na Halotel ambapo wateja wanaweza kuhamia eSIM kwa kutembelea maduka yao rasmi.
Faida za eSIM
Tofauti na watumiaji wa laini za simu za kawaida, watumiaji wa eSIM wanaweza kubadilisha mitandao kwa urahisi bila hitaji la kununua au kubadilisha kadi ya SIM.
Kwa mfano, ukiwa na laini ya Vodacom lakini unataka kutumia Airtel, unaweza kufanya hivyo bila matatizo kama vile unavyo ingia na kutoka katika akaunti zako za mitandao ya kijamii.
Kutokana na kuwa eSIM haiondolewi kwenye simu kama laini za kawaida, inapunguza hatari ya kupoteza au kuibiwa laini ya simu yako. Hivyo humwezesha mtumiaji kuweza kutunza taarifa binafsi kwa uangalifu mkubwa.

Pia kwa kuwa eSIM haichukui nafasi kama SIM za kawaida, inatoa nafasi zaidi kwa vifaa vingine ndani ya simu, kama betri kubwa au teknolojia za hali ya juu.
eSim pia inafaa kwa wasafiri wa kimataifa kwa kuwa unaweza kununua huduma ya mtandao wa nchi husika bila kununua laini mpya.
Kwa mfano, mtumiaji wa Tigo Tanzania anapokuwa Dubai anaweza kutumia mtandao wa nchi hiyo bila hitaji la kubadilisha laini.
Changamoto za eSIM
Mbali na ubora au faida zinazotokana na eSim, teknolojia hii ina changamoto zake, kwa kuwa si kila mtandao unatoa huduma ya eSIM ingawa kwa Tanzania mitandao ya simu kama Vodacom, Tigo, Airtel na Halotel imeshaanza kutoa huduma hii, ijapokuwa bado haijawa ya kawaida kwa watoa huduma wote nchini.
Pia sio kila simu inaweza kutumia eSIM, inahitaji simu ambazo zina uwezo wa kuunga mkono teknolojia hiyo, hivyo wamiliki wa simu za zamani hawana uwezo wa kufurahia teknolojia hii bila kubadili simu.

Kwa kuwa kila kitu kipo kidigitali, hitilafu ya programu au tatizo la mtandao linaweza kufanya laini yako kushindwa kufanya kazi kwa muda fulani kwa kuwa teknolojia ya eSim inategemea zaidi huduma za mtandao.
Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023
Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya.
Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.
Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.
Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.
Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.

Jinsi ya kufungua programu zilizofichwa kwenye iPhone
- Zinaweza kufichwa, kufunguliwa na kurejeshwa kwa uthibitisho wa kibayometriki au nenosiri.
Dar es Salaam. Watumiaji wa simu za iPhone kutoka kampuni ya Apple yenye makao yake makuu California, Marekani, wameanza kufurahia uwezo wa kipengele kipya cha kuficha na kufunga programu kwenye simu zao kupitia toleo jipya la iOS 18 lililotolewa Septemba 2024.
Kipengele hicho husaidia kulinda programu na taarifa nyeti kutokuonekana na wengine wanapotumia simu kwa kuzificha programu kwenye folda maalumu ambalo uhitaji nenosiri au uthibitisho wa kibayometriki.
Ili kufunga au kuficha programu kwenye iPhone, bonyeza na ushikilie ikoni ya programu, kisha chagua ‘Require Face ID.’ Programu hiyo itatoweka kutoka kwenye skrini iliyozoeleka na haitapatikana hata kwenye matokeo ya utafutaji wa ‘Spotlight’.

Programu zilizofichwa huondolewa kwenye skrini kuu na kuhifadhiwa kwenye folda ya siri inayoitwa inayopatikana kwenye ‘App Library’. Picha |CNET
Lakini, wakati mwingine programu zinaweza kufichwa kwa makusudi au kwa bahati mbaya, na zikahitajika kutumiwa tena. Kujua hatua za kuziona kupitia mipangilio ni muhimu ili kusaidia kuzifungua bila kuhangaika.
Kuna njia mbili za kupata programu zilizofichwa kwenye iPhone, ya kwanza ni kufungua iPhone yako na kushuka hadi mwisho wa skrini ili kufikia ukurasa wa ‘App Library.’
Chini kabisa bonyeza ‘hidden folder’, kisha utaombwa kuthibitisha kwa kutumia ‘Face ID’ au ‘Touch ID’, ikiwa uthibitisho wa kibiometriki utashindikana, ingiza nenosiri.
Ukishafanya hivyo, utaweza kuona programu zote zilizofichwa. Ili kuzifungua, utahitaji kuthibitisha tena kwa njia hiyo hiyo yaani kwa kutumia Face ID, Touch ID, au nenosiri ili programu hizo zisifunguliwe na mtu mwingine yeyote bila kibali cha mwenye simu.
Njia ya pili ya kuna programu zilizofichwa ni kupitia mipangilio ‘settings’, hapa nenda kwenye ‘Settings’ kisha ‘Apps’ alafu uingie kwenye ‘Hidden Apps’, kuona programu zote zilizofichwa.

‘Screenshot’ ikionyesha unavyoweza kufunga programu za msingi kama ‘Notes’ kwa kuchagua ‘Require Face ID’ kwa usalama wa nyaraka zako. Picha |CNET
Wakati mwingine mtumiaji anaweza kuficha programu bila kukusudia na kuhitaji kuirejesha kwenye utaratibu wa upatikanaji wa kawaida kwenye ‘home screen’, ili kuirejesha fuata njia ifuatayo.
Fungua iPhone yako na nenda kwenye ‘App library’, kisha gusa ili kufungua folda ya programu zilizofichwa kwa kutumia Face ID au Touch ID.
Baada ya hapo, gusa na ushikilie programu mahususi unayotaka kuirejesha, alafu chagua ‘Don’t require Face ID,’ na uthibitishe kwa mara ya mwisho kwa kutumia uso, alama ya kidole au nenosiri.
Hatua hizo zitakapo fuatwa, programu lengwa itaondolewa kwenye folda la siri na kurudi tena kwenye skrini ya mwanzo, ambapo mtumiaji anaweza kufanya hivyo kwa kuitafuta kwenye ‘App library’ au kupitia ‘Spotlight’.
Mambo matatu ya kuzingatia unapotafuta kazi
- Ni pamoja na kuandaa wasifu binafsi na barua ya maombi kwa ufanisi.
Dar es Salaam. Ni ndoto ya kila mhitimu wa chuo kupata kazi ya kufanya anapomaliza masomo yake. Kazi inaweza kuwa ya kuajiriwa au kujiajiri katika shughuli mbalimbali za kibiashara.
Ndoto hizo hutimia kwa nyakati tofauti. Kwa wengine hupata kazi mapema na wengine husota mtaani wakitembeza bahasha na kutuma maombi kila nafasi zinapotangwa mtandaoni.
Kama wewe ni mmoja wa watu hao, yapo mambo muhimu unayotakiwa kuzingatia wakati unasaka ajira ya ndoto yako ikiwemo kuandaa wasifu na barua ya maombi ya kazi inayojitosheleza.
Mwanzilishi wa Jukwaa la Niajiri, Lilian Madeje anasema kuwa ni muhimu mtu anayetafuta kazi kuandika vizuri wasifu wake, ambao unaelezea taarifa zake kwa usahihi.
“Kwenye ‘CV’ (wasifu) kwa ujumla, lazima mtu ahakikishe amefanya uhuishaji (updating). Aweze kuainisha kwa uwazi elimu yake, namba za simu ziko sawa, na kuepuka makosa ya kisarufi ili anayepokea kwa upande wa pili asitumie muda mrefu kumuelewa muombaji anafanya nini,” anasema Madeje.

Wasifu binafsi ni muhimu uwe fupi, wenye mpangilio mzuri, na usio na makosa ya kisarufi. Picha/ Eastern Suburbs Mums.
Madeje anasema hakikisha barua ya kuomba kazi (Application/cover letter) au barua pepe iwe inajielezea vizuri, na ionyeshe ujuzi ulionao na jambo gani anaweza kufanya kwa nafasi husika.
“Kwenye ‘cover letter’ kuna wengine wanatuma bila ya ‘heading’ (kichwa), wengine unakuta hata ile ‘CV’ (wasifu) mtu hajaifanyia ‘labeling’ vizuri,” anasema Madeje. “Mtu inabidi awe na email (barua pepe) ya kujitambulisha vizuri, ni nani ambaye unamtafuta na kama hauna mtu angalau ujielezee kidogo, mimi ni fulani, nimeona tangazo kwenye gazeti au mtandaoni.”
Aidha, Madeje amebainisha kuwa ni vyema muombaji akajiwekea malengo ya kuomba kazi ili kujiongezea wigo wa kupata kazi.
“Tunaelewa fika kwamba kazi hazitoshi kwa watu wanaotoka vyuoni, lakini pia mtu inabidi ufanye ‘research’ (utafiti) yako. Umetoka chuo, unaenda kufanya ‘application’ (maombi) wapi? Unajipa ‘target’ (malengo) zako, labda kwa kipindi kila wiki unataka kufanya ‘application’ kiasi X ili uweze kuongeza wigo wako,” anasema Madeje.
Niajiri ni jukwaa la kiteknolojia la maendeleo ya nguvukazi linaloimarisha ujuzi wa vipaji vya ngazi ya mwanzoni na kuwapa mwonekano kwa waajiri, huku pia likiwa na zana inayowawezesha waajiri kufikia vipaji bora sokoni.
Afisa Mwajiri kutoka Shirika la Islamic Help, Zubery Titee anasema kuwa CV na barua ya maombi ya kazi zinatakiwa kuonyesha ufanisi wa maombi na kuwa na muundo mzuri wa kitaalamu.
Titee anasema wasifu huu unapaswa kujumuisha ujuzi, elimu, na uzoefu unaohusiana na nafasi ya kazi anayotafuta, na usitumie maneno mengi yasiyohitajika.
Kulingana na tovuti ya The Balance Careers , wasifu (CV) ni nyaraka ndefu inayojumuisha historia ya kitaalamu ya mtu, ikiwa ni pamoja na elimu, uzoefu wa kazi, utafiti, machapisho na mafanikio mengine.
Wasifu pia hutumika kwa madhumuni ya kitaalamu, kama vile maombi ya kazi au nafasi za utafiti katika vyuo vikuu.
Kwa upande mwingine, ‘resume’ ni taarifa fupi inayojumuisha taarifa muhimu kuhusu ujuzi, uzoefu wa kazi, na elimu. Lengo la ‘resume’ ni kutoa muhtasari wa haraka wa sifa za muombaji.

Ikiwa unabadilisha taaluma yako, unaanza katika nchi mpya, au umekuwa nje ya ajira kwa muda, wasifu wako unaweza kukusaidia kupata kazi yako ijayo kwa kuufanya kwa njia sahihi. Picha / Fiverr.
“Ni muhimu kuandaa ‘CV’ (wasifu) yenye kuvutia ambayo itaonyesha ‘profile’ yake, elimu, kozi mbalimbali, semina alizopata kushiriki pamoja na uzoefu katika kufanya kazi au kujitolea katika kazi,” anasema Titee.
Pia, uzoefu wa kazi unapaswa kuonyeshwa kwa uwazi kwenye wasifu ili kuwawezesha waajiri kufanya maamuzi sahihi.
“Waajiri wanapenda sana kuona uzoefu wa muombaji katika nafasi husika, na aghalabu hii ndio inatoa nafasi kubwa ya kuitwa kwenye usaili,” anaeleza Titee.
Uwezo wa kujieleza nao muhimu
Muombaji kazi awe na uwezo wa kujieleza vizuri kuhusu kile alichoandika kwenye wasifu wake binafsi. Maswali atakayoulizwa kwenye usaili yanaweza kutoka kwenye wasifu wake aliowasilisha.
Titee anasema kuwa ni muhimu kwa muombaji kuwa na uelewa wa kina kuhusu jina na malengo ya taasisi anayotaka kujiunga nayo. Waajiri wanapenda kuona muombaji mwenye ufanisi na uelewa wa kweli kuhusu kampuni au shirika analotaka kujiunga nalo.
“Mfano, unaomba kazi katika Shirika la Islamic Help, lakini kwenye barua yako ya maombi unaandika ‘Islamic Help Foundation’. Hii inaweza kuwa dalili ya kutokuwa makini,” anasema Titee.

Ni vyema muombaji kuwa na uwezo wa kujieleza vizuri kuhusu kile alichoandika kwenye wasifu wake binafsi. Picha/ Fair screen.
Muombaji awe na uwezo wa kutetea kile kilichoandikwa kwenye wasifu wake, kwani maswali mengi yanaweza kutokea huko au uelewa wake wa jumla unaweza kusaidia na baadaye kuzingatiwa katika kupata ajira.
Kujiandaa vizuri ni hatua ya kwanza kuelekea kwenye mafanikio yako ya kazi. Usikose kufuatilia toleo la pili la chapisho hili litakalokufunza namna ya kuandaa wasifu.