Undani idadi ya watalii wa kigeni ndani ya miaka 10 Tanzania

Katika kipindi cha miaka 10, Tanzania imepokea jumla ya watalii wa kigeni 13,711,190, ikiimarisha nafasi yake kama moja ya vivutio vikuu vya utalii barani Afrika. Mwaka 2024 umeibuka kuwa wenye mafanikio makubwa zaidi kwa sekta ya utalii, ukivutia watalii 2,141,895, idadi kubwa zaidi katika muongo mmoja.
Kwa upande mwingine, mwaka 2020 uliathirika pakubwa na janga la Uviko-19, ukirekodi idadi ndogo zaidi ya watalii 620,867. Hii inamaanisha kuwa idadi ya watalii walioingia mwaka 2024 ni mara tatu zaidi ya ile ya mwaka 2020, sawa na ongezeko la asilimia 244.9.
Mfumuko huu wa watalii unaonyesha mwelekeo mzuri wa sekta ya utalii, ambayo ina mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kwa kuongeza fedha za kigeni, fursa za ajira, na ukuaji wa biashara za ndani. Tanzania inaendelea kunufaika na vivutio vyake vya kipekee kama Hifadhi ya Serengeti, Mlima Kilimanjaro, Kreta ya Ngorongoro, na fukwe za Zanzibar.
Idadi ya watalii wa kigeni yapaa Tanzania

Tanzania imeendelea kung’ara katika sekta ya utalii baada ya kurekodi ongezeko kubwa la idadi ya watalii wa kigeni mwaka 2024. Kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jumla ya watalii 2,141,895 waliingia nchini, ikiwa ni ongezeko la asilimia 18.58 ikilinganishwa na mwaka 2023.
Hii ni mara tatu zaidi ya idadi ya watalii walioingia nchini mwaka 2020 wakati dunia ilipokumbwa na janga la Uviko-19, ambapo ni 620,867 pekee waliotembelea Tanzania.
Kwa upande wa miezi, Julai umeibuka kinara kwa kuvutia wageni wengi zaidi, huku watalii 218,065 wakiwasili nchini. Kinyume chake, Aprili ndiyo ilikuwa na idadi ndogo zaidi, ikiwa na watalii 116,280 pekee.
Ongezeko hili linaonyesha mvuto wa Tanzania kama kivutio cha utalii duniani, huku vivutio kama Hifadhi ya Serengeti, Mlima Kilimanjaro, na fukwe za Zanzibar vikichangia kwa kiasi kikubwa.
Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023

Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya.
Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.
Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.
Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.
Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.