Tumbaku yazitikisa kahawa, korosho mauzo nje ya nchi Tanzania

  • Thamani ya mauzo nje ya nchi yaongezeka takriban mara mbili ndani ya mwaka mmoja.

Dar es Salaam. Tumbaku ni moja ya bidhaa tatu asilia zinazoongoza kwa kuuzwa kwa wingi nje ya Tanzania na zilizoingiza fedha nyingi za kigeni licha ya kupigwa vita na wadau wa afya kuwa inahatarisha maisha ya watumiaji. 

Kwa mujibu wa Ripoti ya Hali ya Uchumi Tanzania mwaka 2023 iliyotolewa na Wizara ya Fedha hivi karibuni, katika bidhaa za asilia zinazouzwa nje ya nchi tumbaku inachuana kwa mbali na kahawa na korosho. 

Korosho, kahawa, chai na mkonge ni miongoni mwa mazao makubwa ya asilia ambayo huchangia kwa kiwango kikubwa fedha za kigeni nchini ila ukuaji wa uzalishaji wa tumbaku umezidi kuyapiga kikumbo mazao hayo. 

“Mwaka 2023, thamani ya mauzo ya tumbaku nje ilikuwa Dola za Marekani milioni 340.4 (Sh828.2 bilioni) ikilinganishwa na Dola za Marekani milioni 178.5 (Sh411.5 bilioni) mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 90.7,” inasema ripoti hiyo iliyotolewa na Wizara ya Fedha.

Ripoti hiyo inaeleza kuwa mafanikio hayo yalitokana na kuongezeka kwa mauzo ya tumbaku kwa zaidi ya mara moja na nusu hadi kufikia tani 82,000 mwaka 2023 kutoka tani 49,300 mwaka 2022. 

Uuzaji wa zao hilo nje ya nchi ulienda sanjari na kiwango cha uzalishaji wa tumbaku ulioongezeka takriban mara mbili ndani ya mwaka mmoja kutoka tani 70,699 mwaka 2022 hadi tani 122,859 mwaka jana. 

Uzalishaji wa tumbaku umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka Tanzania jambo lililochochea ongezeko la kiwango cha zao hilo kuuzwa nje ya nchi. Picha: Akili Mnemba. Picha hii imetengenezwa na akili mnemba kwa ajili ya kuongeza muktadha kwenye makala hii tu na si kuonyesha uhalisia.

Bei yaibeba tumbaku

Wastani wa bei ya kuuza tumbaku uliongezeka kwa asilimia 14.5 katika soko la dunia na kufikia Dola za Marekani 4,150.8 (Sh11.1 milioni) kwa tani mwaka 2023 kutoka Dola za Marekani 3,624.1(Sh9.7 milioni) kwa tani mwaka 2022.

Ingawa kiasi cha wingi wa korosho kinachouzwa nje ya Tanzania ni zaidi ya mara mbili ya kiasi cha tumbaku na kahawa, thamani ya tumbaku kwenye soko la kimataifa kwa Shilingi ya Tanzania inazidi kwa zaidi ya mara 1.5 ya thamani ya korosho na kahawa. 

Kwa hesabu hizo, tumbaku inakuwa bidhaa asilia yenye thamani kubwa zaidi inayouzwa nje ya nchi. Bidhaa nyingine zisizoasilia zinazochangia zaidi fedha za kigeni ni dhahabu, utalii na bidhaa za viwandani. 

Miaka ya hivi karibuni kumekuwa na hamasa kubwa ya kuongeza ufanisi katika uzalishaji wa tumbaku kwa kutumia mbinu za kisasa za kilimo na kuimarisha uchakataji wake ili kupunguza athari kwa mazingira.

Mfano, kampuni Mkwawa Tobacco Processing Limited (MTPL), imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika usindikaji tumbaku, ikiongeza ajira na kuinua uchumi wa wananchi na wafanyabiashara. 

Uwekezaji huo katika uzalishaji na usindikaji unaofanywa na wakulima na viwanda vya zao hilo, unafanya tumbaku kuwa ni miongoni mwa bidhaa asilia zinazochangia kiwango kikubwa kwenye pato la taifa.  

Pamoja na uwekezaji huo kumekuwa na presha kubwa kutoka kwa wadau wa afya hasa wanaharakati wakiitaka Serikali kudhibiti vikali uzalishaji na utumiaji wa tumbaku unaochangia maradhi kwa binadamu ikiwemo matatizo ya mapafu.

Uteuzi Dk Ndugulile WHO kuipaisha Tanzania kimataifa

  • Ateuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika na kuwa mtu wa kwanza kutoka Afrika Mashariki kushika wadhifa huo.
  • Mwanadiplomasia huyo huzungumza lugha zaidi ya moja.

Dar es Salaam. Tanzania imeendelea kung’aa katika anga za uongozi kimataifa mara baada ya Mbunge wa Jimbo la Kigamboni jijini Dar es Salaam Dk Faustine Ndugulile kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika. 

Dk Ndungulile, ambaye ni daktari wa binadamu kitaaluma, sasa anaingia kwenye orodha ya wanadiplomasia mashuhuri Tanzania wanaoongoza taasisi za kimataifa katika ngazi ya dunia na kikanda. 

Kiongozi huyo anakuwa wa kwanza kutoka ukanda wa Afrika Mashariki kuchukua kijiti hicho kutoka kwa Dk Mtashidiso Moeti ambaye amehudumu katika nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka 10 tangu mwaka 2014. 

Kwa mujibu wa WHO uteuzi Dk Ndugulile unatarajiwa kuridhiwa kwenye kikao cha 156 cha Bodi ya Utendaji wa WHO kitakachofanyika Februari, 2025 huko jijini Geneva, Uswizi ikiwa ndiyo mwanzo wa safari ya miaka mitano ya uongozi wa mtaalamu huyo wa afya. 

Dk Ndugulile (55) mwenye Shahada ya udaktari wa madawa pamoja na shahada ya uzamili kwenye mikrobiolojia na chanjo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amewahi kushika nyazifa mbalimbali ndani ya Serikali ikiwemo ya unaibu waziri wa afya. 

Ushindi huo wa Dk Ndugulile aliyekuwa akichuana na wataalamu wengine kutoka Rwanda, Niger na Senegal ni moja ya hatua muhimu kwa Tanzania kuendelea kuimarisha taswira yake katika nyanja za kimataifa hususan katika taasisi kuu za kufanya maamuzi duniani. 

Nchi wanachama wa Afrika walimteua Dk Ndugulile jijini Brazzaville nchini Congo jambo ambalo amesema ni heshima kubwa kwake. 

“Nia yangu ni kufanya kazi pamoja nanyi na naimani kwamba kwa pamoja tutaweza kujenga Afrika yenye afya bora,” amesema Dk Ndugulile.

Dk Ndugulile, aliyewahi kuwa Waziri wa zamani wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano alijunga na siasa tangu 2010 kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) huku akishikilia nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye sera za afya kutokana na uzoefu wake wa kazi.

Mtaalamu huyo wa afya ameongoza miradi mbalimbali katika huduma za afya nchini Tanzania na kuandika machapisho ya tafiti zinazohusu afya ya umma ambazo zimechangia katika maendeleo ya sera za afya inayolenga kuboresha afya ya wananchi.

“Dk Ndugulile amepata imani na uaminifu wa wanachama wa nchi wa kanda hii kwa kuchaguliwa kuwa Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, hii ni heshima kubwa na jukumu kubwa sana…mimi na familia nzima ya WHO barani Afrika na duniani kote tutakusaidia katika kila hatua,” amebainisha Dk Ghebreyesus.

Hata hivyo, kuteuliwa kwake kama Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika ni hatua muhimu katika kufanikisha malengo ya afya kwa nchi za Afrika hii inathibitisha kutokana na  uzoefu na utaalamu wake kwenye uwanja wa afya.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akimpigia kampeni Dk Ndugulile alieleza kwenye mtandao wa X (zamani Twitter) kuwa kiongozi ameiheshimisha nchi na kwamba Afrika itanufaika na utaalamu wake. 

“Nina imani kuwa ujuzi na uzoefu wako katika sekta ya afya utawezesha Afrika kuwa na sauti muhimu katika uwanja wa kimataifa katika kukabiliana na changamoto za kiafya kwa mamilioni ya watu katika bara letu,” amesema Rais Samia.

Unavyoweza kuandaa mirathi mtandaoni kupitia akaunti ya kidijitali

  • Ni kwa kutumia nyenzo maalum ya usimamiaji wa mirathi ya kimtandao.
  • Hupunguza upotevu wa taarifa mtandaoni baada ya mtumiaji kufariki.

Dar es Salaam. Matumizi ya teknolojia na mtandao yamezidi kushika kasi siku za hivi karibuni yakiwawezesha watu kuwasiliana huku wengine wakiitumia kuhifadhi mambo muhimu ikiwemo nyaraka za kibenki, hati za nyumba na kumbukumbu za maisha yao.

Lakini umewahi kufikiria nini kitatokea kwa taarifa ulizohifadhi mtandaoni baada ya kifo chako? 

Watu wengi wamekua wakiacha mirathi ya mali zinazohamishika na wanazomiliki kwa wanafamilia wao ili wafaidike lakini husahau kuacha urithi wa taarifa muhimu walizohifadhi mtandaoni kwenye mikono salama.

Leo tunaangazia umuhimu wa kuandaa mipango ya kuhifadhi taarifa zako za mtandaoni kwa watu unaowaamini kabla ya kufariki.

Jinsi ya kuandaa mirathi ya akaunti yako

Intaneti imeongeza wigo wa ufikiaji na matumizi ya huduma mbalimbali kidijitali kama miamala ya kifedha, hifadhi ya nyaraka muhimu, hati, picha na video ambazo zinaweza kuwa na faida kwa watu wa karibu utakaowaacha, Google inaweza kuwaruhusu kupata baadhi ya vitu hivyo endapo utaamua mapema.

Kupitia huduma ya akaunti ya google isiyotumika, unaweza  kuamua kitakachotendeka mara tu akaunti yako inapoacha kutumika kwa muda uliouweka, kuliko kuzuia kabisa ikae kwenye seva bila kufikika na watu muhimu wanaosalia.

Kwanza andaa orodha ya akaunti zote unazomiliki zikiwa na majina na nywila zake, kisha chagua watu au mtu unayemwamini atakayekuwa na jukumu la kuzisimamia kisha ufuate vigezo vya sera ya urithi ya mtoa huduma.

Kabla akaunti yako kufungwa kwa kutotumika ni muhimu kuweka mpangilio (setting) ili kupata taarifa kupitia barua pepe na ujumbe mfupi wa simu.

Warithi wa taarifa zako ulizohifadhi mtandaoni lazima wathibitishe kupitia ujumbe mfupi (SMS) kabla hawajapewa ruhusa ya ufikiaji wa taarifa hizo, pia unaweza kuwatumia jumbe binafsi za alama za kidijitali za vidole vyako ili kurahisisha zoezi hilo.

Baada ya kuthibitisha mrithi atapata sms itakayomjulisha kupewa taarifa hizo na kiungo maalum (link) itakayomuwezesha kupakua taarifa zote ulizohifadhi.

Usipoacha urithi wa kidijitali, watu wako wa karibu watahitaji kuwasiliana na Google juu ya akaunti yako ili kuwafahamisha kuwa umefariki, sambamba na kuwapa uthibitisho wa kifo ili waruhusiwe kupata vitu maalumu utakavyokua umeruhusu wao kuvifikia kwa sababu hawataweza kufungua vitu vyote vya kwenye akaunti yako.

Faida za kuacha mrithi wa taarifa za mtandaoni

Kupanga urithi wa akaunti za kidijitali husaidia ulinzi wa taarifa kwa kuhakikisha kuwa picha au video za familia, mawasiliano muhimu na nyaraka za kifedha zinabaki salama za kuweza kupatikana kwa warithi wako.

Pia husaidia kuwapunguzia watu wako wa karibu mzigo wa kutafuta na kupata taarifa zako baada ya kifo chako sambamba na kuhakikisha kuwa taarifa hizo zinatumika kulingana na matakwa yako.

Usikose sehemu ya pili ya makala hii ambapo tutaangazia jinsi unavyoweza kupata taarifa zilizohifadhiwa mtandaoni na ndugu, jamaa au rafiki aliyeaga dunia.

Enable Notifications OK No thanks