Fursa au changamoto, idadi ya vituo vya kubadili fedha za kigeni ikipaa Tanzania
- Imeongezeka zaidi ya mara 16 ndani ya kipindi cha miaka mitano.
Dar es Salaam. Kwa miji mikubwa ya utalii na biashara kama Arusha, Zanzibar na Dar es Salaam ni kawaida kukutana na mabango ya vituo vya kubadilisha fedha za kigeni vinavyowawezesha mamia ya wazawa na wageni kupata huduma hizo za kifedha.
Miaka michache tu iliyopita huduma hizo zilikuwa zikitolewa kupita matawi ya kibenki au vituo vichache vilivyokuwepo katika miji mikubwa pekee au katikati ya miji.
Kwa sasa hali hiyo imebadilika, baada ya kuongezeka kwa vituo hivyo zaidi ya mara 16 ndani ya kipindi cha miaka mitano.

Ripoti ya Usimamizi wa Sekta ya Fedha mwaka 2025 inayotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inabainisha kuwa vituo vya kubadilisha fedha za kigeni vimefikia 65 mwaka 2025 kutoka vituo vinne vilivyokuwepo mwaka 2021.
Hii ni sawa na kusema idadi ya vituo hivyo muhimu katika sekta ya uchumi imepaa kwa asilimia 1,525, jambo linaloashiria kupanuka kwa upatikanaji wa huduma rasmi za kubadilisha fedha za kigeni nchini.
NBS inafafanua kuwa vituo vinne vilivyokuwepo mwaka 2021, vilikuwa na matawi 40, pamoja na benki za biashara 34 vikiongezeka hadi vituo 65 vyenye matawi 182, benki 35 za kibiashara na hoteli 12 mwaka 2025.
Wakati vituo vya kubadilisha fedha za kigeni vikiongezeka BoT inabainisha kuwa mauzo ya fedha za kigeni yameongezeka kwa asilimia 19.3 ndani ya miaka mitano.
Mauzo hayo yalipaa kutoka Dola za Marekani 7.2 bilioni waka 2021 hadi Dola za Marekani bilioni 8.9 mwaka 2025,
BoT inabainisha kuwa ongezeko hilo imechangiwa na kuongezeka kwa shughuli za utalii nchi, biashara za kimataifa baina ya Tanzania na mataifa ya nje pamoja na sera nzuri za Serikali zinazovutia wawekezaji nchini.
Ni kicheko, maumivu
Mchambuzi wa masuala ya uchumi Paul Chengula, anasema kuongezeka kwa vituo hivyo ni fursa kwa wafanyabiashara na makampuni yanayojihusisisha na biashara hiyo.
“Wafanyabiashara wa kubadili fedha wananufaika zaidi kwa sababu inawapa fursa ya kuuza zaidi, lakini pia inawapa ajira vijana ambao wanafanya kazi katika maduka na makampuni hayo” amesema Chengula.
Chengula ameongezea kuwa, biashara ya fedha za kigeni imechochea kukua na kuongezeka kwa fursa mbalimbali za kiuchumi na kupungua ka njia za mkato zinazosababishia hasara Serikali.
“Uwepo wa hii biashara umeongeza wingi wa fedha za kigeni, jambo linalowezesha wafanyabiashara, watalii na wawekezaji kupata sarafu za kigeni kwa urahisi, lakini hata mtiririko wa fedha unakua ni wa uwazi hali inayochochea kuondoa, njia za mkato kama utakatishaji fedha” amesema Chengula.
Hata hivyo, Chengula amesema ongezeko la vituo hivyo linaweza kuwa changamoto kwa mabenki yaliyokuwa yakitawala biashara hiyo kwa sababu idadi ya wateja waliokuwa ikiwahudumia itapungua.
“Wanaoathirika zaidi ni mabenki, ambayo awali yalikua yameitawala biashara hii kwa kiasi kikubwa, sasa inawabidi wafanye njia nyingine kuhakikisha bado wanaendelea kuliteka soko” ameongeza Chengula.

Dar es Salaam kinara
Dar es Salaam imeendelea kuwa kitovu na mhimili mkubwa wa huduma za kubadilisha fedha za kigeni nchini Tanzania, ikiwa na nusu ya matawi yote ya kubadilishia fedha za kigeni nchini, ukiwa na takribani matawi 91 kati ya 182 yaliyopo nchini.
Hii ni sawa na kusema vituo vitano kati ya 10 vya kubadilishia fedha za kigeni vipo katika jiji la Dar es Salaam ambalo ni kitovu cha uchumi wa nchi na mataifa jirani.
Mbali na Dar es Salaam, Visiwa vya Zanzibar vimeshika nafasi ya pili ikiwa na matawi 33 ikifuatiwa na Arusha yenye matawi 31, Kilimanjaro matawi 10 na mikoa mingine iliyosalia ikiwa na jumla ya matawi 17.