Matukio ya ulaghai mtandaoni yashuka kwa asilimia 25
- Mtwara yavunja rekodi ya kuwa na matukio machache zaidi ikiwa na matukio 25.
Dar es Salaam. Huenda watumiaji wa mitandao wakaondokana na changamoto ya ulaghai mtandaoni baada ya pungua kwa matukio hayo kwa asilimia 25 ndani ya kipindi cha miezi mitatu.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ulaghai mtandaoni ni kitendo cha kutumia intaneti, simu, au mitandao ya kijamii kuiba pesa, taarifa za siri, ama kudanganya watu.
Ulaghai huu unaweza kufanyika kwa njia ya ujumbe wa uongo (kutumiwa SMS za kuomba fedha au kudanganya umeshinda zawadi), wizi wa nenosiri (kuombwa kutoa namba ya siri au namba ya uthibitisho – OTP) pamoja na kutumia viungo feki.
Takwimu za mawasiliano za robo ya mwaka inayoishia Juni 2026 zinazotewa na TCRA, zinaonesha ulaghai umepungua kutoka matukio 9,816 yaliyoripotiwa robo mwaka inayoishia Machi 2026 hadi kufikia matukio 7,334 katika robo ya mwaka inayoishia Juni 2026.
Kwa takwimu hizi ni sawa na kusema matukio 2,482 hayajaripotiwa ndani ya miezi mitatu iliyopita suala linalotoa ahueni kwa wananchi.
Rukwa kinara

Ripoti ya TCRA inabainisha kuwa mkoa ya Rukwa unaongoza kwa majaribio ya ulaghai ikiwa na matukio 2,495, zaidi ya robo tatu ya majaribio yote ya ulaghai nchini.
Uchambuzi uliofanywa na Nukta Habari umebaini kuwa mkoa huo umekuwa kinara kwa ulaghai kwa zaidi ya miaka mitano, ukipanda au kushuka kila baada ya miezi mitatu.
Licha ya kuwa kinara, takwimu za TCRA zinabainisha kuwa ulaghai mtandaoni katika mkoa wa Rukwa unapungua karibu kila mwezi suala linalotoa ahueni kwa wakazi wa eneo hilo.
Mathalan, katika ripoti ya robo ya kwanza 2025 matukio 7,385 yalirekodiwa mkoani Rukwa, yaliyopungua na kufikia matukio 3,444 katika robo ya pili, 2025.
Mbali na Rukwa, mkoa wa Morogoro umeshika nafasi ya pili kwa kurekodi matukio 2,129 huku wilaya ya Kilombero ikiripoti matukio 1,781 ambayo ni zaidi ya nusu ya matukio yaliyorekodiwa na mkoa mzima.
Mikoa mingine iliyoongoza kwa kuripoti matukio ya ulaghai kwa njia ya mtandao ni Dar es Salaam ikishika nafasi ya tatu ikiwa na matukio 615, ikifuatiwa na Mbeya yenye matukio 370.
Kwa upande wa mikoa iliyorekodi matukio machache zaidi ya ulaghai wa mtandaoni ni Shinganya ikiwa na matukio 33, ikifuatiwa na Lindi matukio 31 na Mtwara ikishika mkia kwa kuwa na matukio machache zaidi ikiwa na matukio 25.
Kwa upande wa Zanzibar mkoa wa Mjini Magharibi ndio umeongoza kwa majaribio ya utapeli kwa njia ya mtandao ukiwa na jumla ya matukio 35 huku Mkoa wa Kusini unguja ukifuata kwa kuwa na matukio 5.
Mtandao wa Yas waongoza

Ripoti ya TCRA inaonesha baadhi ya makampuni yanayo toa huduma za mawasiliano nchi yaliyorekodi kiwango kikubwa zaidi cha majaribio ya uhalifu.
Mtandao wa Yas ndiyo iliyorekodi idadi kubwa zaidi ya majaribio katika robo iliyoishia Juni, 2026 ikiwa na jumla ya matukio 2,306, sawa na asilimia 31.4 ya matukio yote.
Licha ya kuwa na idadi kubwa zaidi, Yas ilipunguza idadi ya matukio hayo kutoka 2,659 yaliyo rekodiwa miezi mitatu iliyopita hadi matukio 2,306, TTCL inafuata ikiwa na matukio 2,039, sawa na asilimia 27.8, huku Vodacom ikiwa na matukio 1,364, Airtel 1,053 na Halotel 572.
TTCL ilirekodi punguzo kubwa zaidi kwa asilimia, kutoka matukio 3,375 hadi 2,039, sawa na asilimia 39.59, kwa upande wa Vodacom matukio yalipungua kwa asilimia 27.56, huku Airtel matukio yakipungua kwa asilimia 24.73.
Wakati mitandao mingine ikirekodi kupungua kwa matukio, Halotel ndiyo iliyokwenda kinyume na mwenendo wa jumla, ikiripotiwa kuwa na matukio yaliyoongezeka kutoka 500 hadi 572 ikiwa ni sawa na ongezeko la matukio kwa na asilimia 14.4
Mapambano yanaendelea
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Angellah Kairuki aliyekuwa akizungumza katika uzinduzi wa ripoti hiyo amesema kupungua kwa matukio ya ulaghai wa mtandao nchini, kunatokana na jitihada za wazi za Serikali pamoja na wadau wa mawasiliano katika kukabiliana na tatizo hilo.
“Kupungua huku kwa matukio ya ulaghai kunatokana na upekuzi na ukaguzi mbalimbali zilizofanywa na TCRA kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani, pamoja na wadau wa mawasiliano katika mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Mbeya na Mara zikiwalenga wahusika ambao wanafanya matukio ya ulaghai nchini…,” amesema Kairuki.
Kwa upande wa watumiaji wa mitandao ya simu amewahimiza kutoa taarifa za majaribio ya utapeli wanapokutana nayo kupitia namba 15040 ili zifuatiliwe na hatua za kisheria zipate kuchukuliwa ikiwemo kuzifungia namba hizo.
Aidha, Kairuki amesema Serikali inaendelea na kampeni mbalimbali zenye kuongeza uelewa na usalama kwa watumiaji wa huduma za kimawasiliano ikiwemo ‘futa au delete kabisa’ na ‘sambaza mchongo sio uongo’ inayosisitiza kutosambaza taarifa zisizo sahihi kwenye majukwaa ya kidigitali.
Fursa, watumiaji wa intaneti Tanzania wakifikia milioni 58.1
- Hadi kufikia robo ya mwaka inayoishia Desemba 2025, watumiaji wa intaneti walikuwa milion 58.1 kutoka milioni 56.3 iliyorekodiwa Septemba 2025.
- Intaneti hiyo hutumiwa zaidi na simu za janja.
- Hiyo inaongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na fursa za mtandaoni.
Dar es Salaam. Idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za intaneti imeendelea kuongezeka kwa kasi na kufikia milioni 58.1 suala linalotajwa kuendelea kufungua fursa zaidi za kiuchumi.
Takwimu za mawasiliano za robo ya nne ya mwaka 2025 zilizotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zinaonesha matumizi ya huduma z aintaneti yameongezeka kwa asilimia 3.2.
Takwimu hizo zinaonyesha kuwa hadi kufikia Desemba 2025 watumiaji wa intaneti walifikia milioni 58.1 kutoka watumiaji 56.3 waliokuwepo Septemba 2025.
Idadi hiyo ni sawa na ongezeko la watumiaji milioni 1.8 ndani ya kipindi cha miezi mitatu kuanzia Septemba hadi Disemba mwaka jana.
Kwa mujibu wa TCRA, idadi hiyo inajumuisha laini zote zilizotumia huduma ya intaneti angalau mara moja katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita, bila kujali teknolojia iliyotumika kupitia njia mbalimbali, zikiwemo laini za simu za mkononi, nyaya za faiba (fiber), pamoja na teknolojia za mawimbi (wireless).
Uchambuzi wa takwimu hizo uliofanywa na Nukta Habari kwa miaka 10 mfululizo umebaini ongezeko la watumiaji wa intaneti nchini Tanzania mwaka hadi mwaka.
Huenda ukuaji huo umechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuendelea kuimarika kwa miundombinu ya mawasiliano nchini, ikiwemo ongezeko la minara ya simu iliyofikia 10,029 kufikia mwisho wa mwaka 2024.
Aidha, intaneti inayotumia mtandao wa simu za mkononi (mobile wireless internet) imeendelea kuwa njia kuu ya upatikanaji wa huduma hiyo, ikichangia asilimia 99 ya usajili wote wa intaneti nchini.
Mbali na ongezeko la matumizi ya intaneti, matumizi ya simu janja (smartphones) pia yameongezeka, ambapo kiwango cha upenyo wake kimefikia asilimia 41.82.
Hata hivyo, simu za kawaida (feature phones) bado zinaendelea kutumika kwa kiwango kikubwa zaidi zikiwa na asilimia 87.11 ya matumizi.
Ni fursa iliyojificha
Wachambuzi wa uchumi wanaeleza kuwa ongezeko hilo la matumizi ya intaneti linafungua fursa mpya katika biashara, elimu, huduma za kifedha na ajira za kidijitali, huku likichochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.
Akizungumza kuhusu mwenendo huo, Profesa Abel Kinyondo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amesema kuwa ongezeko la usajili wa laini zinazotumia intaneti halimaanishi moja kwa moja kuwa idadi hiyo ni sawa na watumiaji halisi, kwa kuwa mtu mmoja anaweza kuwa na laini zaidi ya moja.
Amefafanua kuwa pamoja na changamoto zilizopo, intaneti imeleta mapinduzi makubwa katika shughuli za kiuchumi kwa kurahisisha biashara, masoko na huduma za kifedha.
“Leo mtu anaweza kufanya biashara akiwa sehemu yoyote nchini bila kulazimika kusafiri. Intaneti imeongeza urahisi wa kufanya miamala, kutangaza bidhaa na kupata taarifa mbalimbali kwa haraka,” amesema Profesa Kinyondo.
Hata hivyo, ameonya kuwa matumizi ya intaneti yanaambatana na changamoto mbalimbali zikiwemo uhalifu wa mtandaoni, udanganyifu katika biashara za mtandaoni na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.
Pia amewataka vijana kutumia intaneti kwa manufaa, ikiwemo kujifunza ujuzi mpya, kufanya biashara na kutafuta maarifa, huku wakizingatia tahadhari dhidi ya matumizi yanayoweza kuhatarisha usalama wao binafsi na maadili ya jamii.
Idadi ya redio yazidi kupaa Tanzania

- Idadi ya vituo vya redio Tanzania imezidi kuongezeka kwa kasi baada ya vituo 17 kuanzishwa ndani ya mwaka mmoja.
Dar es Salaam. Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Redio leo Februari 13, 2022, redio ni chombo muhimu ambacho Watanzania wana kitumia kupata habari zinazowawezesha kufanya maamuzi katika maisha yao ya kila siku.
Licha ya kuongezeka kwa changamoto za kifedha zinazoendelea kuvikabili vyombo mbalimbali vya habari duniani, idadi ya vituo vya redio Tanzania imezidi kuongezeka kwa kasi baada ya vituo 17 kuanzishwa ndani ya mwaka mmoja.
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inaeleza katika ripoti mpya ya mawasilino ya robo ya mwisho ya mwaka 2021 kuwa hadi Desemba mwaka jana kulikuwa na vituo 210 vya redio nchini kutoka vituo 193 mwaka 2020.
Uchambuzi wa mwenendo wa takwimu za vituo vya redio uliofanywa na Nukta (www.nukta.co.tz) unaonyesha kuwa vituo vingi vya redio vilizaliwa mwaka 2016 baada ya vituo 42 kuanzishwa ndani ya mwaka mmoja.
Hata hivyo, mwaka 2018 ndiyo mwaka ambao vituo vichache zaidi vilianzishwa ndani ya mwaka mmoja kutokana na kuongezeka kwa vituo viwili tu vya redio kutoka 156 mwaka 2017 hadi 158 mwaka 2018.