Uteuzi Dk Ndugulile WHO kuipaisha Tanzania kimataifa

  • Ateuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika na kuwa mtu wa kwanza kutoka Afrika Mashariki kushika wadhifa huo.
  • Mwanadiplomasia huyo huzungumza lugha zaidi ya moja.

Dar es Salaam. Tanzania imeendelea kung’aa katika anga za uongozi kimataifa mara baada ya Mbunge wa Jimbo la Kigamboni jijini Dar es Salaam Dk Faustine Ndugulile kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika. 

Dk Ndungulile, ambaye ni daktari wa binadamu kitaaluma, sasa anaingia kwenye orodha ya wanadiplomasia mashuhuri Tanzania wanaoongoza taasisi za kimataifa katika ngazi ya dunia na kikanda. 

Kiongozi huyo anakuwa wa kwanza kutoka ukanda wa Afrika Mashariki kuchukua kijiti hicho kutoka kwa Dk Mtashidiso Moeti ambaye amehudumu katika nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka 10 tangu mwaka 2014. 

Kwa mujibu wa WHO uteuzi Dk Ndugulile unatarajiwa kuridhiwa kwenye kikao cha 156 cha Bodi ya Utendaji wa WHO kitakachofanyika Februari, 2025 huko jijini Geneva, Uswizi ikiwa ndiyo mwanzo wa safari ya miaka mitano ya uongozi wa mtaalamu huyo wa afya. 

Dk Ndugulile (55) mwenye Shahada ya udaktari wa madawa pamoja na shahada ya uzamili kwenye mikrobiolojia na chanjo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amewahi kushika nyazifa mbalimbali ndani ya Serikali ikiwemo ya unaibu waziri wa afya. 

Ushindi huo wa Dk Ndugulile aliyekuwa akichuana na wataalamu wengine kutoka Rwanda, Niger na Senegal ni moja ya hatua muhimu kwa Tanzania kuendelea kuimarisha taswira yake katika nyanja za kimataifa hususan katika taasisi kuu za kufanya maamuzi duniani. 

Nchi wanachama wa Afrika walimteua Dk Ndugulile jijini Brazzaville nchini Congo jambo ambalo amesema ni heshima kubwa kwake. 

“Nia yangu ni kufanya kazi pamoja nanyi na naimani kwamba kwa pamoja tutaweza kujenga Afrika yenye afya bora,” amesema Dk Ndugulile.

Dk Ndugulile, aliyewahi kuwa Waziri wa zamani wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano alijunga na siasa tangu 2010 kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) huku akishikilia nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye sera za afya kutokana na uzoefu wake wa kazi.

Mtaalamu huyo wa afya ameongoza miradi mbalimbali katika huduma za afya nchini Tanzania na kuandika machapisho ya tafiti zinazohusu afya ya umma ambazo zimechangia katika maendeleo ya sera za afya inayolenga kuboresha afya ya wananchi.

“Dk Ndugulile amepata imani na uaminifu wa wanachama wa nchi wa kanda hii kwa kuchaguliwa kuwa Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, hii ni heshima kubwa na jukumu kubwa sana…mimi na familia nzima ya WHO barani Afrika na duniani kote tutakusaidia katika kila hatua,” amebainisha Dk Ghebreyesus.

Hata hivyo, kuteuliwa kwake kama Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika ni hatua muhimu katika kufanikisha malengo ya afya kwa nchi za Afrika hii inathibitisha kutokana na  uzoefu na utaalamu wake kwenye uwanja wa afya.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akimpigia kampeni Dk Ndugulile alieleza kwenye mtandao wa X (zamani Twitter) kuwa kiongozi ameiheshimisha nchi na kwamba Afrika itanufaika na utaalamu wake. 

“Nina imani kuwa ujuzi na uzoefu wako katika sekta ya afya utawezesha Afrika kuwa na sauti muhimu katika uwanja wa kimataifa katika kukabiliana na changamoto za kiafya kwa mamilioni ya watu katika bara letu,” amesema Rais Samia.

Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania

Dar es Salaam. Miongoni mwa masuala yanayogusa zaidi vijana wengi waliopo kwenye ndoa na wasio kwenye ndoa kwa sasa ni suala la kuwa na watoto. 

Miongoni mwa maswali makubwa huwa ni lini wapate watoto, idadi ya watoto lakini ni njia gani sahihi itakayomfanya wanawake vijana wasipate ujauzito bila kutarajia. Wataalamu wanasisitiza kuwa ni vema wazazi vijana wakapanga mipango yao vema ya kijamii na kiuchumi kabla ya kupata watoto. 

Hata hivyo, si watu wote wanapanga ipasavyo juu ya kupata watoto. Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa mwaka 2022 unabainisha kuwa nchini Tanzania takriban wanawake wanne kati ya 10 au asilimia 38 ya waliolewa wenye umri wa miaka 15 hadi 49 wanatumia njia ya aina yeyote ya uzazi wa mpango.

Ripoti ya utafiti huo uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa ushirikiano na taasisi nyingine iwepo Wizara ya Afya inabainisha ipo baadhi ya mikoa yenye kiwango kikubwa cha wanawake wenye wanaotumia ipasavyo njia za uzazi wa mpango ikiongozwa na Njombe huku mingine ikitumia kwa kiwango kidogo sana kama Simiyu. 

Je, waifahamu mikoa inayoongoza kwa matumizi ya njia za uzazi wa mpango Tanzania? 

Ulaji milo mitatu ya chakula bado kitendawili Tanzania

  • Idadi ya wanaokula milo mitatu yashuka kwa asilimia 8.2.
  • Mtanzania mmoja kati ya 10, anakula mlo mmoja wa chakula.
  • Uviko -19, uhaba wa chakula baadhi ya maeneo vyatajwa kama sababu.

Dar es Salaam. Wakati wataalamu wa afya wakihimiza kula milo mitatu ya chakula kwa siku au zaidi ili kuwa na afya bora, hali ni tofauti nchini Tanzania kwani idadi ya watu wanaokula milo mitatu kwa siku imeshuka kwa asilimia 8.2.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Kufuatilia Hali ya Kaya Tanzania (NPS) ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), idadi ya Watanzania wanaokula milo mitatu imeshuka kutoka asilimia 71.2 mwaka 2014/15 mpaka asilimia 63 mwaka 2020/21.

Hii ni kumaanisha kuwa kati ya Watanzania kumi ni sita ndio wanaokula milo mitatu ya chakula au zaidi kwa siku. 

Wakati idadi ya wanaokula milo mitatu au zaidi ikishuka, idadi ya wanaokula milo miwili hadi mmoja imeongezeka. Mathalani wanaokula mlo mmoja wameongezeka kutoka asilimia 0.6 mpaka 1.6 huku wanaokula milo miwili wakiongezeka kutoka 28.2 mpaka 35.4.

Uchambuzi wa takwimu uliofanywa na Nukta habari umebaini kuwa kwa mujjbu wa ripoti hiyo katika kila Watanzania kumi basi mmoja hula mlo mmoja tu wa chakula huku watatu kati ya 10 wakila milo miwili ya chakula.

Hata hivyo, hali ya ulaji wa chakula imeonekana mbaya zaidi katika maeneo ya vijijini kuliko mjini kwani, Watanzania waishio mjini wana wastani mzuri zaidi wa kula milo mitatu kwa asilimia 74.8 huku vijijini wakiwa na asilimia 57.3.

Vivyo hivyo, idadi ya wanaokula mlo mmoja vijijini ni kubwa zaidi ambao ni  asilimia 1.8 wakati mjini ni 1.2 huku asilimia ya wanaokula milo miwili vijijini ikiwa ni mara mbili zaidi ya wale waishio mjini.

Huenda hali hiyo imechangiwa na kuwepo kwa upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo hapa nchini hali iliyosababishwa na mtawanyiko wa mvua pamoja na visumbufu.


Soma zaidi


Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Chakula nchini ya mwaka 2020/21 imeeleeza kuwa pamoja na kuwa na ziada ya chakula halmashauri 17 kutoka mikoa nane nchini ilitarajiwa kukutana na uhaba wa chakula mwaka juzi.

“Upungufu huo umechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo mtawanyiko mbaya wa mvua, visumbufu vya mimea kama vile wanyamapori, ndege aina ya kwelea kwelea na viwavijeshi vamizi, ”  inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Aidha uwepo wa ugonjwa wa Uviko-19 uliathiri shughuli za kilimo kwani ulisababisha changamoto katika upatikanaji wa pembejeo muhimu za kilimo kama vile mbegu, mbolea, viuatilifu na zana za kilimo.

Janga hilo lilichangia watu kupoteza ajira na biashara, na hivyo kukosa kipato kwa ajili ya kukidhi ya mahitaji ya kila siku ya chakula. 


Tangazo:

Wanasayansi kuja na chanjo ya Uviko-19 ya kunywa

  • Matokeo ya utafiti wa awali yaonyesha mwitikio chanya. 
  • Inatarajiwa itachochea ongezeko la watu wanaopata chanjo.

Dar es Salaam. Huenda idadi ya watu wanaopata chanjo ya Uviko-19 ikaongezeka siku za usoni pale wanasayansi watakapokamilisha utafiti wao kuhusu chanjo ya ugonjwa huo ambayo mtu anaweza kuipata kwa kunywa.

Mpaka sasa katika aina zote za chanjo zilizoidhinishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), huingizwa katika mwili wa binadamu kwa kutumia njia ya sindano jambo ambalo limekuwa kigezo kwa baadhi ya watu kutochanja kwa kuogopa maumivu ya sindano.

Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya teknolojia ya nchini Marekani ya Cnet watafiti na wanasayansi wameongeza nguvu katika ugunduzi wa chanjo mpya kupitia mfumo wa upumuaji au kinywa.

Chanjo hiyo itakayofahamika kama QYNDR (kinder),  imeshakamilisha sehemu ya kwanza ya majaribio yake na sasa inasubiri fedha kwa ajili ya majaribio zaidi na kisha iingizwe sokoni.

Kwa mujibu wa Kyle Flanigan ambaye ni mtengenezaji wa chanjo hiyo, ‘kinder’ itatumia njia rafiki kuingia kwenye mwili wa binadamu.

Flanigan anasema matokeo ya utafiti wa chanjo hiyo yaliyofanyika nchini New Zealand yana mwitikio chanya ingawa bado hayajakaguliwa na mamlaka za kiafya za kimataifa.

“Si rahisi kutengeneza na kuifanya  na chanjo iweze kufanya kazi kupitia mfumo wa mmeng’enyo, tuligundua njia itakayoifanya chanjo ipite tumboni na kutoa matokeo yanayofaa, “ anasema Flanigan.

Habari za uwepo wa majaribio ya chanjo za Uviko-19 kwa njia ya mfumo wa mmeng’enyo wa chakula zinakuja kipindi ambacho mzalishaji wa chanjo za Pfizer anakabiliwa na ukosoaji mkubwa nchini Marekani kuhusiana na ufanisi wa chanjo zake.

Hata hivyo mpaka sasa WHO hawajatoa taarifa yoyote ya kuthibitisha shutuma hizo dhidi ya Pfizer zaidi ya kuendelea kusisitiza matumizi ya chanjo kwani zimesaidia kuokoa mamilioni ya maisha ya watu.

Wataalamu wa afya wanaendelea kusisitiza kuwa ugonjwa wa Uviko-19 bado upo na unaua  ingawa kwa kasi ndogo ambapo kwa mujibu wa WHO Januari 23 mwaka huu watu 1,017 walipoteza maisha siku hiyo huku jumla ya watu milioni 6.7 wakipoteza maisha tangu kuanza kwa janga hilo mwaka 2019.

Kraken: Kirusi kipya cha Uviko-19 kinachowatesa wanasayansi

  • Kinatajwa kuenea kwa kasi zaidi kuliko virusi vilivyopita.
  • Uwezo wa kubadili jeni zake ni miongoni mwa sababu.
  • Barakoa yatajwa kama njia bora zaidi ya kujikinga na kirusi hicho.

Dar es Salaam. Ingawa si jambo linalozungumzwa sana kwa sasa, lakini wasiwasi unaendelea kuongezeka kwa wanayansi ambao wanajaribu kutafuta ufumbuzi wa kukabiliana na makali ya kirusi kipya cha Uviko-19 ambacho kinaenea kwa kasi barani Ulaya.

Kirusi hicho kinachoitwa XBB.1.5 au Kraken ni matokeo ya mabadiliko ya kijeni ya kirusi aina ya Omicron XBB ambacho nacho kiliripotiwa kuwa na kasi kubwa katika kuenea kwake.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kirusi hicho kiliripotiwa kwa mara ya kwanza Oktoba 2022, nchini Marekani na sasa tayari kimeenea katika nchi 38 barani Ulaya ikiwemo Sweden, Kanada, Australia na Ufaransa.

Disemba mwaka jana, China ilitangaza kuwa wastani wa watu 60,000 walipoteza maisha kutokana na virusi vya Omicron aina ya BA.5.2 na BF.7 vilivyozuka nchini humo.


Soma zaidi:


Mapema Januari mwaka huu Mkurugenzi wa masuala ya Teknolojia kutoka WHO, Maria Van Kerkhove alisema kirusi hicho ndiyo kinaambukiza kwa kasi zaidi kuliko aina nyingine za virusi.

“Sababu kubwa ni kutokana na kirusi hiki kuwa na uwezo wa kubadilisha jeni zake mara kwa mara hivyo si rahisi kukidhibiti,” anasema Kerkhove.

Pamoja na kwamba kirusi hichi kinaenea kwa kasi bado hakuna uhakika kwamba kinaweza kusababisha maafa makubwa kuliko ilivyokuwa awali.

Kutokana na uwezo wa kirusi hicho kujibadili mara kwa mara kulingana na mazingira wataalamu wa afya wameshauri pamoja na chanjo ya uviko-19 njia inayotajwa kuwa na uhakika zaidi ni kuvaa barakoa muda wote mtu anapokuwa kwenye mikusanyiko.

Kwa mujibu wa Kituo Cha Kudhibiti Magonjwa nchini Marekani (CDC) mpaka sasa asilimia 43 ya visa vya maambukizi ya Uviko-19 nchini humo yamesababishwa na kirusi hicho kipya.


Tangazo


Ifahamu kansa ya shingo ya kizazi na athari zake

  • Husababishwa na maambukizi ya muda mrefu ya virusi vya  “human papilloma”
  • Virusi hivyo huenezwa kwa njia ya kujamiiana.
  • Upatikanaji duni wa kinga na matibabu huchangia asilimia 90 ya vifo duniani kote.

Dar es Salaam. Licha ya kuwepo nchini kwa miaka mingi kansa ya shingo  ya kizazi imeendelea kugharimu maisha ya wanawake wengi huku kukiwa na uelewa mdogo kuhusu chanzo cha ugonjwa huo na namna unavyoweza kuutibu.

Januari kila mwaka hutumika kutoa elimu na uelewa juu ya visababishi vya ugonjwa huo na jinsi ya kukabiliana nao kwa wasichana.

Taasisi ya Saratani ya Ocean Road inasema kwa kiasi kikubwa saratani hii husababishwa na maambukizi ya mda mrefu (persistence infection) ya virusi viitwavyo “human papilloma”, ambavyo huenezwa kwa njia ya kujamiiana. 

“Kawaida mwili una uwezo wa hudhibiti maambukizi haya yaingiapo mwilini, lakini yasipodhibitiwa kikamilifu na kuwepo mwilini kwa muda mrefu husababisha ugonjwa wa saratani ya shingo ya kizazi,” inasema taasisi hiyo.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema matibabu ya mapema yanaweza kuokoa maisha ya wanawake takriban 342,000 waliopoteza maisha kwa ugonjwa huo mwaka 2020 na wagonjwa wapya 604,000 waliopata maambukizi hayo duniani kote kwa mwaka huo huo.

“Knsa ya shingo ya kizazi inazuilika  lakini upatikanaji duni wa kinga, uchunguzi na matibabu huchangia asilimia 90 ya vifo,” linasema Shirika hilo.

Hata hivyo, kabla ya mtu kupata madhara anaweza kugundua mapema dalili za ugonjwa huo kwa kujifanyia uchunguzi mwenyewe.

WHO inasema inachukua miaka 15 hadi 20 kwa saratani ya shingo ya kizazi kukua kwa wanawake walio na kinga ya kawaida na miaka 5 hadi 10 tu kwa wanawake walio na kinga dhaifu, kama vile walio na maambukizo ya VVU ambayo hayajatibiwa.

Enable Notifications OK No thanks