Fahamu faida za ulaji wa brokoli

  • Ni pamoja na kuzuia ugonjwa wa moyo na kuimarisha afya ya mifupa kulingana na uwepo wa nyuzi nyuzi na vitamini.
  • Kusaidia mmeng’enyo wa chakula na matatizo ya kiungulia.

Dar es Salaam. Kuna aina za nyingi za mbogamboga na kila moja ina faida zake katika mwili wa binadamu ikiwemo kuimarisha kinga mwilini.

Pamoja na wingi wa mboga hizo, kila moja ina faida zake mahususi ambazo unaweza usizipate katika aina nyingine za mboga au ukazipata kwa uchache.

Katikati ya aina hizo za mboga ipo brokoli, mboga maarufu inayosifika kwa faida nyingi za kiafya ikiwemo wingi wa kirutubisho adimu cha vitamini K ambacho hakipatikani kwenye mboga nyingi.

“Ni miongoni mwa mmea wenye vitamini C nyingi, vitamini K ambayo ni ‘very rare’ (adimu sana) kuipata. Vitamini K inapatikana kwenye vyakula vichache, ina madini ya chuma, vitamini D, A. 

…Lakini pia ina madini mengi ina kalsium, magnesium, potassium,” amesema  Irine Kweka,  Afisa Lishe kutoka Hospitali ya Kondoa jijini Dodoma.

Hata hivyo, Kweka ameongeza kuwa sifa kubwa ya brokoili uwepo wa  antioxidanti nzuri kulingana na uwepo wa vitamini.

Kwanini ule brokoli?

Brokoli husaidia kupunguza viwango vya lehemu (cholesterol) mbaya (LDL) na kuongeza lehemu nzuri (HDL).Picha/Nutrition and Health Innovation Research Institute.

Ikiwa bado unajiuliza sababu za kuongeza brokoli katika mlo wako wa kila siku Kweka aliyekuwa akizungumza na Nukta Habari amebainisha kuwa moja aya faida ya kutumia mboga hiyo katika mlo ni kusaidia mmeng’enyo wa chakula kulingana na wingi wa nyuzinyuzi.

Nyuzi nyuzi hizo pia husaidia tatizo la choo kigumu, kudhibiti kiwango cha asidi kwenye tumbo, kukabiliana na kiungulia au vidonda vya tumbo,pamoja na kuongeza idadi ya bakteria wazuri tumboni, ambao ni muhimu kwa usagaji bora wa chakula. 

Bakteria hawa husaidia kuvunjavunja chakula kwa ufanisi na pia huchangia katika afya bora ya kinga ya mwili. 

Kuzuia magonjwa ya moyo

Ulaji wa Brokoli husaidia kupunguza viwango vya lehemu (cholesterol) mbaya (LDL) na kuongeza lehemu nzuri (HDL), hali inayosaidia kupunguza hatari ya kupata magonjwa ya moyo.

Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya afya,  Medical News Today brokoli ina nyuzi nyuzi, antioksidanti, na kemikali za kibaolojia zinazopunguza kiwango cha ehemu na kudumisha utendaji mzuri wa moyo. 

Juisi ya brokoli inaweza kusaidia kudhibiti ugonjwa wa kisukari na hata kuuzuia kabisa. Picha/ Daily Express.

Uwepo wa nyuzi nyuzi hizo kwa wingi, husaidia kuzuia kuziba kwa mishipa ya damu kwa kupunguza kiasi cha mafuta mabaya mwilini hali inayoweza kupunguza uwezekano wa kupata shinikizo la damu, kiharusi, na mshtuko wa moyo.

Kuimarisha afya ya mifupa

Tovuti ya Naturmed Scientific inaeleza kuwa mifupa yenye nguvu inahitaji virutubisho muhimu kama vile kalsiamu, fosforasi, na vitamini K, vyote ambavyo hupatikana kwa wingi katika brokoli. 

Vitamini K inasaidia katika mgandisho wa damu na pia huchangia uimarishaji wa madini kwenye mifupa, jambo ambalo linapunguza uwezekano wa mifupa kuwa dhaifu au kuvunjika kwa urahisi.

Mifupa yenye nguvu inahitaji virutubisho muhimu kama vile kalsiamu, fosforasi, na vitamini K ambavyo pia hupatikana kwenye brokoli. Picha/ La Muscle.

Pia, brokoli ina kiasi kikubwa cha madini ya magnesiamu na zinki, hali inayowafanya walaji wa brokoli kupunguza msongamano wa mifupa (osteoporosis), unaochangia mifupa kuwa dhaifu na rahisi kuvunjika.

Kinga dhidi ya saratani

Taasisi ya kansa ya nchini Marekani (National Cancer Institute) inabainisha kuwa brokoli ina kemikali zinazozuia ukuaji wa seli zenye uwezo wa kusababisha saratani. 

Tafiti mbalimbali zimeonesha kuwa ulaji wa mara kwa mara wa mboga za jamii ya ‘cruciferous’, ikiwemo brokoli, unaweza kupunguza hatari ya saratani ya matiti, saratani ya tezi dume, na saratani ya utumbo mpana.

Mboga hizi ni za kipekee kwa namna nyingi kimuundo wa kemikali, ikiwa ni pamoja na kiwango chao cha juu cha misombo yenye salfa inayoitwa glukosinolati, ambayo huwapa harufu yao ya kipekee. Picha/ Everyday Health.

Mbali na kinga dhidi ya saratani, brokoli pia inasaidia wagonjw wa saratani  kupunguza madhara yanayotokana na matibabu kama mionzi na dawa za kemikali.

 Kuimarisha afya ya ngozi

Ngozi yenye afya inahitaji lishe bora, na brokoli ni moja ya vyakula vinavyotoa virutubisho muhimu kwa ngozi. 

Vitamini C inayopatikana kwa wingi kwenye brokoli inasaidia mwili kutengeneza collagen, ambayo ni protini muhimu kwa uimara na mng’ao wa ngozi.

Brokoli ina nguvu za ustawi wa mwili kwa kiwango cha nyuzi joto 360º, ikisaidia afya ya moyo, ngozi, na nywele. Picha/ Wild Element.

Brokoli pia ina vioksidishaji vinavyosaidia kupunguza athari za miale ya jua ambayo inaweza kusababisha uharibifu wa ngozi  huku vitamini A na E, vilivyopo katika mboga hiyo ambavyo vikiifanya ngozi kuwa naunyevu wa kutosha. 

 Kudhibiti sukari ya damu

Kwa watu wenye ugonjwa wa kisukari, brokoli ni moja ya vyakula vinavyopaswa kujumuishwa katika lishe. Ina misombo inayosaidia kudhibiti viwango vya sukari kwenye damu kwa kupunguza upinzani wa insulini.

Uwepo wa sulforaphane inayopatikana kwenye brokoli inaweza kusaidia kupunguza viwango vya sukari kwa wagonjwa wa kisukari aina ya pili. 

Nyuzinyuzi zilizopo kwenye brokoli husaidia kuzuia kuongezeka kwa ghafla kwa kiwango cha sukari baada ya kula. Picha/Times of India.

Sulforaphane husaidia kongosho kutoa insulini kwa ufanisi zaidi na hivyo kudhibiti sukari mwilini.

Mbali na hayo, nyuzinyuzi zilizopo kwenye brokoli husaidia kupunguza kasi ya mmeng’enyo wa wanga, na hivyo kuzuia kuongezeka kwa ghafla kwa kiwango cha sukari baada ya kula. 

Hii ni muhimu kwa watu wanaotaka kudhibiti uzito na kuepuka hatari ya kupata kisukari.

Kusaidia kuzuia mchakato wa kuzeeka

Mchakato wa kuzeeka kwa kiasi kikubwa unahusishwa na mkazo wa oksidativi na kupungua kwa kazi ya kimetaboliki wakati wa maisha ya binadamu.

Ingawa kuzeeka ni mchakato wa asili usioepukika, ubora wa lishe unadhaniwa kuwa na mchango mkubwa katika kuamua jinsi jeni zinavyotumika na maendeleo ya magonjwa yanayohusiana na umri 

Matumizi ya mboga hii kwa wingi husaidia kupunguza kasi ya uzee. Picha/Nature4Nature.

Ili kuhifadhi virutubisho vyake, ni vyema kupika brokoli kwa muda mfupi kwa kutumia njia kama kuipika kwa mvuke au kuitumia katika saladi. Kwa kuongeza brokoli katika lishe yako ya kila siku, unaweza kufurahia afya bora na kuzuia magonjwa mbalimbali.

Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023

Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya. 

Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.

Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.

Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.

Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.

 Lishe inavyoweza kukabiliana na matatizo ya mgongo wazi na vichwa vikubwa

  • Hii ni pamoja na ulaji wa matunda na mboga mboga.
  • Nchini Tanzania takribani watoto 7,500 huzaliwa na matatizo ya mgongo wazi pamoja na vichwa vikubwa.

Dar es Salaam. Lishe bora imetajwa kuwa miongoni mwa kinga za magonjwa ya mgongo wazi na vichwa vikubwa yanayowapata watoto wachanga wenye umri kati ya 0 hadi miezi miwili.

Magonjwa hayo ambayo kitaalamu huitwa ‘Spinal bifida and Hydrocephalus’ mara nyingi hugundulika pale tu mtoto anapozaliwa huku wengine wakichukua muda zaidi.

Kituo cha Kudhibiti na Kukinga Magonjwa nchini Marekani  (CDC) kimesema  watoto wengi wanaozaliwa na mgongo wazi mara nyingi hupata ulemavu wa kichwa kikubwa kunakosababishwa na ubongo kujaa maji.

Picha hii inaonesha mgongo wazi, ugonjwa ambao mtoto anazaliwa huku uti wa mgongo ukiwa wazi (kidonda/uvimbe mgongoni) kutokana na pingili za mgongo kutokuziba vizuri.picha/StoryMd

“Hii inatokea kutokana na kifaa cha ubongo kutokufanya kazi ipasavyo katika kuchuja na kutoa majimaji kupitia njia za asili ndani ya ubongo na uti wa mgongo. Matokeo yake ni kwamba kuna maji mengi yanakusanyika ndani na kuzunguka ubongo,” imesema CDC.

Majimaji hayo ya ziada yanaweza kusababisha sehemu za ubongo zinazojulikana kama ventrikali kuwa kubwa kupita kiasi, na hivyo kusababisha kichwa kuvimba. 

CDC imesema Miongoni mwa dalili za tatizo la kichwa kikubwa ni pamoja na kichwa cha mtoto kuwa kikubwa kuliko kawaida, macho kuelekea chini, utosi kuzidi kwa mtoto mchanga na mtoto kutapika sana na kuhisi kizunguzungu.

Kwa upande wa mgongo wazi kituo hicho kimezitaja dalili zake kuwa ni pamoja na mtoto kuwa na uvimbe ama kidondo katika uti wa mgongo, mtoto kuwa na baka, chale au nywele zisizo za kawaida katika eneo la uti wa mgongo.

Nchini Tanzania takribani watoto 7,500 huzaliwa na matatizo ya mgongo wazi pamoja na vichwa vikubwa huku watoto 1000 tu ndio wanaopatiwa matibabu kwa mwaka.

Takwimu hizo zimetolewa na Dk Hamisi Shabani kutoka katika Hospitali ya Taifa Muhimbili iliyopo jijini Dar es Salaam wakati akifanyiwa mahojiano kwenye kipindi cha televisheni kupitia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ambapo pia amewatoa hofu wazazi kwa kuwa tatizo hilo linatibika.

“Hili tatizo hasa la kichwa kikubwa linatibika na mtoto anarudi kuwa mtu mzima kabisa kama wanajamii wengine hili la mgongo wazi linategemea ule ulemavu umefikia kiwango gani lakini pia unatibika…

…Nisiwatishe Watanzania kwa sababu haya matibabu yanapatikana katika hospitali zetu,” ameeleza Dk Shabani ambaye pia ni daktari bingwa wa upasuaji wa magonjwa ya ubongo,uti wa mgongo pamoja na mgongo wazi.

Hata hivyo,daktari Hamisi amekiri kuwepo kwa kiwango kidogo cha elimu sahihi ya visababishi na tiba ya magonjwa hayo jambo linalopelekea kuwa na idadi kubwa ya watoto ambao hawajapatiwa matibabu.

Lishe bora suluhisho la kudumu

Wakati madaktari wakiendelea kuhamasisha tiba ya magonjwa hayo, wataalamu wa lishe wanasema lishe bora kwa mama mjamzito na wanawake wenye umri wa kuzaa ndiyo suluhisho la kudumu kwa matatizo ya mgongo wazi na vichwa vikubwa.

“Wanatakiwa waanze kutumia vile vidonge vya ‘Fefo’ mapema, vidonge hivi vina ‘combination’ (mchanganyiko) ya madini ya chuma na vitamini ya Foliki asidi ambayo inasaidia katika kupunguza matatizo ya watoto kuzaliwa na matatizo ya vichwa vikubwa na mgongo wazi, ”amesema Malimi Kitunda Mtaalamu wa lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC).

Mfano wa dawa ambazo wanawake wajawazito wanatakiwa kutumia kwa maelekezo ya wataalamu wa afya mara tu wanapokuwa wameanza kuhudhuria kliniki. Picha/Dk Mwanyika.

Malimi ameongeza kuwa pia ni vyema mtu kutumia vyakula ambayo vimeongezwa virutubishi vya madini ya foliki asidi kwa wingi kama vile mahindi na unga wa ngano ambao una ziada ya virutubisho.

“Kwa sasa hivi tunaongeza virutubishi vya foliki asidi kwenye mahindi na unga wa ngano kwa ajili ya kupambana na tatizo hilo la watoto kuzaliwa na tatizo la mgongo wazi pamoja na vichwa vikubwa,” amebainisha hilo Malimi.

Aidha, Malimi ameeleza kuwa kwa sasa virutubisho hivyo vinapatikana Tanzania na vimeanza kutumiwa na wazalishaji wakubwa wa unga wa mahindi na ngano.

Vyakula vyenye vitamini ya foliki asidi kwa wingi ni pamoja na  maharage, kabichi, mahindi, maini, mihogo, viazi, maziwa na mayai.

Hata hivyo, matunda kama papai,parachichi,ndizi,machungwa, tikiti maji, nanasi, kakara, tufaa, zabibu na matunda mengine pia yapaswa kuzingatiwa kabla na wakati wote wa ujauzito.

Uteuzi Dk Ndugulile WHO kuipaisha Tanzania kimataifa

  • Ateuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika na kuwa mtu wa kwanza kutoka Afrika Mashariki kushika wadhifa huo.
  • Mwanadiplomasia huyo huzungumza lugha zaidi ya moja.

Dar es Salaam. Tanzania imeendelea kung’aa katika anga za uongozi kimataifa mara baada ya Mbunge wa Jimbo la Kigamboni jijini Dar es Salaam Dk Faustine Ndugulile kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika. 

Dk Ndungulile, ambaye ni daktari wa binadamu kitaaluma, sasa anaingia kwenye orodha ya wanadiplomasia mashuhuri Tanzania wanaoongoza taasisi za kimataifa katika ngazi ya dunia na kikanda. 

Kiongozi huyo anakuwa wa kwanza kutoka ukanda wa Afrika Mashariki kuchukua kijiti hicho kutoka kwa Dk Mtashidiso Moeti ambaye amehudumu katika nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka 10 tangu mwaka 2014. 

Kwa mujibu wa WHO uteuzi Dk Ndugulile unatarajiwa kuridhiwa kwenye kikao cha 156 cha Bodi ya Utendaji wa WHO kitakachofanyika Februari, 2025 huko jijini Geneva, Uswizi ikiwa ndiyo mwanzo wa safari ya miaka mitano ya uongozi wa mtaalamu huyo wa afya. 

Dk Ndugulile (55) mwenye Shahada ya udaktari wa madawa pamoja na shahada ya uzamili kwenye mikrobiolojia na chanjo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amewahi kushika nyazifa mbalimbali ndani ya Serikali ikiwemo ya unaibu waziri wa afya. 

Ushindi huo wa Dk Ndugulile aliyekuwa akichuana na wataalamu wengine kutoka Rwanda, Niger na Senegal ni moja ya hatua muhimu kwa Tanzania kuendelea kuimarisha taswira yake katika nyanja za kimataifa hususan katika taasisi kuu za kufanya maamuzi duniani. 

Nchi wanachama wa Afrika walimteua Dk Ndugulile jijini Brazzaville nchini Congo jambo ambalo amesema ni heshima kubwa kwake. 

“Nia yangu ni kufanya kazi pamoja nanyi na naimani kwamba kwa pamoja tutaweza kujenga Afrika yenye afya bora,” amesema Dk Ndugulile.

Dk Ndugulile, aliyewahi kuwa Waziri wa zamani wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano alijunga na siasa tangu 2010 kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) huku akishikilia nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye sera za afya kutokana na uzoefu wake wa kazi.

Mtaalamu huyo wa afya ameongoza miradi mbalimbali katika huduma za afya nchini Tanzania na kuandika machapisho ya tafiti zinazohusu afya ya umma ambazo zimechangia katika maendeleo ya sera za afya inayolenga kuboresha afya ya wananchi.

“Dk Ndugulile amepata imani na uaminifu wa wanachama wa nchi wa kanda hii kwa kuchaguliwa kuwa Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, hii ni heshima kubwa na jukumu kubwa sana…mimi na familia nzima ya WHO barani Afrika na duniani kote tutakusaidia katika kila hatua,” amebainisha Dk Ghebreyesus.

Hata hivyo, kuteuliwa kwake kama Mkurugenzi wa Shirika la Afya (WHO), Kanda ya Afrika ni hatua muhimu katika kufanikisha malengo ya afya kwa nchi za Afrika hii inathibitisha kutokana na  uzoefu na utaalamu wake kwenye uwanja wa afya.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akimpigia kampeni Dk Ndugulile alieleza kwenye mtandao wa X (zamani Twitter) kuwa kiongozi ameiheshimisha nchi na kwamba Afrika itanufaika na utaalamu wake. 

“Nina imani kuwa ujuzi na uzoefu wako katika sekta ya afya utawezesha Afrika kuwa na sauti muhimu katika uwanja wa kimataifa katika kukabiliana na changamoto za kiafya kwa mamilioni ya watu katika bara letu,” amesema Rais Samia.

Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania

Dar es Salaam. Miongoni mwa masuala yanayogusa zaidi vijana wengi waliopo kwenye ndoa na wasio kwenye ndoa kwa sasa ni suala la kuwa na watoto. 

Miongoni mwa maswali makubwa huwa ni lini wapate watoto, idadi ya watoto lakini ni njia gani sahihi itakayomfanya wanawake vijana wasipate ujauzito bila kutarajia. Wataalamu wanasisitiza kuwa ni vema wazazi vijana wakapanga mipango yao vema ya kijamii na kiuchumi kabla ya kupata watoto. 

Hata hivyo, si watu wote wanapanga ipasavyo juu ya kupata watoto. Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa mwaka 2022 unabainisha kuwa nchini Tanzania takriban wanawake wanne kati ya 10 au asilimia 38 ya waliolewa wenye umri wa miaka 15 hadi 49 wanatumia njia ya aina yeyote ya uzazi wa mpango.

Ripoti ya utafiti huo uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa ushirikiano na taasisi nyingine iwepo Wizara ya Afya inabainisha ipo baadhi ya mikoa yenye kiwango kikubwa cha wanawake wenye wanaotumia ipasavyo njia za uzazi wa mpango ikiongozwa na Njombe huku mingine ikitumia kwa kiwango kidogo sana kama Simiyu. 

Je, waifahamu mikoa inayoongoza kwa matumizi ya njia za uzazi wa mpango Tanzania? 

Ulaji milo mitatu ya chakula bado kitendawili Tanzania

  • Idadi ya wanaokula milo mitatu yashuka kwa asilimia 8.2.
  • Mtanzania mmoja kati ya 10, anakula mlo mmoja wa chakula.
  • Uviko -19, uhaba wa chakula baadhi ya maeneo vyatajwa kama sababu.

Dar es Salaam. Wakati wataalamu wa afya wakihimiza kula milo mitatu ya chakula kwa siku au zaidi ili kuwa na afya bora, hali ni tofauti nchini Tanzania kwani idadi ya watu wanaokula milo mitatu kwa siku imeshuka kwa asilimia 8.2.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Kufuatilia Hali ya Kaya Tanzania (NPS) ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), idadi ya Watanzania wanaokula milo mitatu imeshuka kutoka asilimia 71.2 mwaka 2014/15 mpaka asilimia 63 mwaka 2020/21.

Hii ni kumaanisha kuwa kati ya Watanzania kumi ni sita ndio wanaokula milo mitatu ya chakula au zaidi kwa siku. 

Wakati idadi ya wanaokula milo mitatu au zaidi ikishuka, idadi ya wanaokula milo miwili hadi mmoja imeongezeka. Mathalani wanaokula mlo mmoja wameongezeka kutoka asilimia 0.6 mpaka 1.6 huku wanaokula milo miwili wakiongezeka kutoka 28.2 mpaka 35.4.

Uchambuzi wa takwimu uliofanywa na Nukta habari umebaini kuwa kwa mujjbu wa ripoti hiyo katika kila Watanzania kumi basi mmoja hula mlo mmoja tu wa chakula huku watatu kati ya 10 wakila milo miwili ya chakula.

Hata hivyo, hali ya ulaji wa chakula imeonekana mbaya zaidi katika maeneo ya vijijini kuliko mjini kwani, Watanzania waishio mjini wana wastani mzuri zaidi wa kula milo mitatu kwa asilimia 74.8 huku vijijini wakiwa na asilimia 57.3.

Vivyo hivyo, idadi ya wanaokula mlo mmoja vijijini ni kubwa zaidi ambao ni  asilimia 1.8 wakati mjini ni 1.2 huku asilimia ya wanaokula milo miwili vijijini ikiwa ni mara mbili zaidi ya wale waishio mjini.

Huenda hali hiyo imechangiwa na kuwepo kwa upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo hapa nchini hali iliyosababishwa na mtawanyiko wa mvua pamoja na visumbufu.


Soma zaidi


Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Chakula nchini ya mwaka 2020/21 imeeleeza kuwa pamoja na kuwa na ziada ya chakula halmashauri 17 kutoka mikoa nane nchini ilitarajiwa kukutana na uhaba wa chakula mwaka juzi.

“Upungufu huo umechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo mtawanyiko mbaya wa mvua, visumbufu vya mimea kama vile wanyamapori, ndege aina ya kwelea kwelea na viwavijeshi vamizi, ”  inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Aidha uwepo wa ugonjwa wa Uviko-19 uliathiri shughuli za kilimo kwani ulisababisha changamoto katika upatikanaji wa pembejeo muhimu za kilimo kama vile mbegu, mbolea, viuatilifu na zana za kilimo.

Janga hilo lilichangia watu kupoteza ajira na biashara, na hivyo kukosa kipato kwa ajili ya kukidhi ya mahitaji ya kila siku ya chakula. 


Tangazo:

Wanasayansi kuja na chanjo ya Uviko-19 ya kunywa

  • Matokeo ya utafiti wa awali yaonyesha mwitikio chanya. 
  • Inatarajiwa itachochea ongezeko la watu wanaopata chanjo.

Dar es Salaam. Huenda idadi ya watu wanaopata chanjo ya Uviko-19 ikaongezeka siku za usoni pale wanasayansi watakapokamilisha utafiti wao kuhusu chanjo ya ugonjwa huo ambayo mtu anaweza kuipata kwa kunywa.

Mpaka sasa katika aina zote za chanjo zilizoidhinishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), huingizwa katika mwili wa binadamu kwa kutumia njia ya sindano jambo ambalo limekuwa kigezo kwa baadhi ya watu kutochanja kwa kuogopa maumivu ya sindano.

Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya teknolojia ya nchini Marekani ya Cnet watafiti na wanasayansi wameongeza nguvu katika ugunduzi wa chanjo mpya kupitia mfumo wa upumuaji au kinywa.

Chanjo hiyo itakayofahamika kama QYNDR (kinder),  imeshakamilisha sehemu ya kwanza ya majaribio yake na sasa inasubiri fedha kwa ajili ya majaribio zaidi na kisha iingizwe sokoni.

Kwa mujibu wa Kyle Flanigan ambaye ni mtengenezaji wa chanjo hiyo, ‘kinder’ itatumia njia rafiki kuingia kwenye mwili wa binadamu.

Flanigan anasema matokeo ya utafiti wa chanjo hiyo yaliyofanyika nchini New Zealand yana mwitikio chanya ingawa bado hayajakaguliwa na mamlaka za kiafya za kimataifa.

“Si rahisi kutengeneza na kuifanya  na chanjo iweze kufanya kazi kupitia mfumo wa mmeng’enyo, tuligundua njia itakayoifanya chanjo ipite tumboni na kutoa matokeo yanayofaa, “ anasema Flanigan.

Habari za uwepo wa majaribio ya chanjo za Uviko-19 kwa njia ya mfumo wa mmeng’enyo wa chakula zinakuja kipindi ambacho mzalishaji wa chanjo za Pfizer anakabiliwa na ukosoaji mkubwa nchini Marekani kuhusiana na ufanisi wa chanjo zake.

Hata hivyo mpaka sasa WHO hawajatoa taarifa yoyote ya kuthibitisha shutuma hizo dhidi ya Pfizer zaidi ya kuendelea kusisitiza matumizi ya chanjo kwani zimesaidia kuokoa mamilioni ya maisha ya watu.

Wataalamu wa afya wanaendelea kusisitiza kuwa ugonjwa wa Uviko-19 bado upo na unaua  ingawa kwa kasi ndogo ambapo kwa mujibu wa WHO Januari 23 mwaka huu watu 1,017 walipoteza maisha siku hiyo huku jumla ya watu milioni 6.7 wakipoteza maisha tangu kuanza kwa janga hilo mwaka 2019.

Kraken: Kirusi kipya cha Uviko-19 kinachowatesa wanasayansi

  • Kinatajwa kuenea kwa kasi zaidi kuliko virusi vilivyopita.
  • Uwezo wa kubadili jeni zake ni miongoni mwa sababu.
  • Barakoa yatajwa kama njia bora zaidi ya kujikinga na kirusi hicho.

Dar es Salaam. Ingawa si jambo linalozungumzwa sana kwa sasa, lakini wasiwasi unaendelea kuongezeka kwa wanayansi ambao wanajaribu kutafuta ufumbuzi wa kukabiliana na makali ya kirusi kipya cha Uviko-19 ambacho kinaenea kwa kasi barani Ulaya.

Kirusi hicho kinachoitwa XBB.1.5 au Kraken ni matokeo ya mabadiliko ya kijeni ya kirusi aina ya Omicron XBB ambacho nacho kiliripotiwa kuwa na kasi kubwa katika kuenea kwake.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kirusi hicho kiliripotiwa kwa mara ya kwanza Oktoba 2022, nchini Marekani na sasa tayari kimeenea katika nchi 38 barani Ulaya ikiwemo Sweden, Kanada, Australia na Ufaransa.

Disemba mwaka jana, China ilitangaza kuwa wastani wa watu 60,000 walipoteza maisha kutokana na virusi vya Omicron aina ya BA.5.2 na BF.7 vilivyozuka nchini humo.


Soma zaidi:


Mapema Januari mwaka huu Mkurugenzi wa masuala ya Teknolojia kutoka WHO, Maria Van Kerkhove alisema kirusi hicho ndiyo kinaambukiza kwa kasi zaidi kuliko aina nyingine za virusi.

“Sababu kubwa ni kutokana na kirusi hiki kuwa na uwezo wa kubadilisha jeni zake mara kwa mara hivyo si rahisi kukidhibiti,” anasema Kerkhove.

Pamoja na kwamba kirusi hichi kinaenea kwa kasi bado hakuna uhakika kwamba kinaweza kusababisha maafa makubwa kuliko ilivyokuwa awali.

Kutokana na uwezo wa kirusi hicho kujibadili mara kwa mara kulingana na mazingira wataalamu wa afya wameshauri pamoja na chanjo ya uviko-19 njia inayotajwa kuwa na uhakika zaidi ni kuvaa barakoa muda wote mtu anapokuwa kwenye mikusanyiko.

Kwa mujibu wa Kituo Cha Kudhibiti Magonjwa nchini Marekani (CDC) mpaka sasa asilimia 43 ya visa vya maambukizi ya Uviko-19 nchini humo yamesababishwa na kirusi hicho kipya.


Tangazo


Enable Notifications OK No thanks