Hatua za kumuanzishia mtoto wa miezi sita chakula cha ziada

  • Hatua hizo zimegawanyika katika wiki tatu.
  • Mtoto huanza kupewa vijiko viwili hadi kufikia robo kikombe akifikisha mwaka mmoja.

Arusha. Lishe ni miongoni mwa mahitaji muhimu katika ukuaji wa mtoto ikimuwezesha kukua vyema na kumuepusha na magonjwa.

Katika miezi sita ya mwanzo wataalamu wa lishe hushauri mtoto apewe maziwa ya mama pekee bila kuchanganya na chochote ili kumpatia virutubisho vinavyohitajika katika hatua hiyo ya ukuaji.

Mwongozo wa lishe kwa watoto wadogo uliotolewa na Taasisi ya Chakula na Lishe (TFNC) unabainisha kuwa baada ya miezi sita ya mwanzo mtoto mchanga anahitaji chakula cha ziada ili kumpatia virutubisho ambavyo hupungua katika maziwa ya mama kadri mtoto anayokuwa.

“Vyakula vya nyongeza vinahitajika ili kumpatia mtoto nishati, vitamini na madini ambayo maziwa ya mama hayatoshelezi kadri mtoto anavyoendelea kukua,” umesema muongozo wa TFNC.

Mwongozo huo umebainisha kuwa mtoto anatakiwa kupata angalau makundi matatu ya chakula kwa kila mlo kati ya kundi la wanga, vyakula vya jamii ya kunde, mafuta na sukari, matunda na vile vyenye asili ya wanyama.

Hata hivyo, vyakula hivyo vya ziada hupaswa kuongezwa kwa hatua kadhaa ili mtoto aweze kuzoea na kurahisisha umengenywaji wake katika mfumo wa chakula wa mtoto.

Daktari Reinfrida Ngairo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) ambaye pia ni mkufunzi wa lishe ya mama na mtoto ameimbia Nukta Habari kuwa hatua hizo zimegawanyika katika wiki tatu.

Ni muhimu kuzingatia uzito sahihi wa chakula cha mtoto ili aweze kuoata nishati na virutubisho vingine vya muhimu.Picha/Haakaa.

Wiki ya kwanza

Daktari Ngairo anasema mtoto anayeanzishiwa vyakula vya ziada huanza kupewa vyakula vyepesi (vya maji maji) kwa kiwango kidogo kisichozidi vijiko vitatu kwa siku mbili hadi tatu za mwanzoni.

“Lengo katika wiki ya kwanza ya kuanzisha chakula ni ku ‘introduce’ (kuitambulisha) tu ladha… kwa hiyo akila hata vijiko vitatu tu vinatosha akitaka zaidi ni sawa mpe zaidi na mlo mmoja unatosha kwa wiki ya kwanza.” ameongeza Dk Ngairo.

Vyakula hivyo ni pamoja na matunda yaliyopondwa na kuchanganywa na maziwa ya mama, maziwa ya kopo, au supu  kama ndizi, parachichi, papai, embe na tikiti huku siku ya tatu na kuendelea mzazi akiruhusiwa kumpa mtoto uji mwepesi wa nafaka moja ikiwemo mahindi, mtama, ulezi au uwele

“Kuchanganya nafaka zote kwa pamoja, unauchosha mfumo wa tumbo na mtoto anaweza hata asiweze pata virutubisho vyote vnavyohitajika…

kuanzia siku ya tatu ile anapoanza uji unaweza anza pia vyakula vingine mfano bogalishe, mtori, rojo la karoti, viazi, mboga majani na viazi lishe,” amesema Dk Ngairo.

Wiki ya pili

Katika wiki ya pili baada ya mtoto kuzoea chakula Dk Ngairo anashauri kumuanzishia vyakula vinavyoweza kuleta mzio mara moja kwa siku ikiwemo karanga, samaki, kiini cha yai, ufuta na aina nyingine.

“Kwa hiyo hapa unaweza mpa mtoto asubuhi mtori wa supu ya samaki umeweka mnofu kdogo wa samaki ukasaga…unafaya hivi siku mbili au tatu mfululizo ili ujue kama kitampa shida au la,” ameongeza Dk Ngairo.

Wataalamu wa afya wanashauri mtoto apate angalau aina tatu za makundi ya chakula.Picha/Felix Hospital.

Wiki ya tatu

Kuanzia wiki ya tatu hadi mtoto atakapofikisha mwaka mmoja unaruhusiwa kuchanganya vyakula mfano ndizi, kiazi, supu na mboga za majani pia kumpa uji wa nafaka mbili, mbegu na karanga.. 

Mtoto anakiwa kupewa vyakula hivyo mara tatu au nne kwa siku pamoja na asusa kama sharubati nzito na matunda kati ya mlo na mlo bila kusahau kunyoshwa kila anapohitaji.

Mwongozo wa TFNC unabainisha kuwa kadri mtoto anavyoendelea kukua anatakiwa kumaliza kikombe au kibakuli cha ujazo wa mililita 250 kwa mlo mmoja huku akiendelea kuacha vyakula laini sana kwenda vyakula vilivyopondwa hadi kufikia vyakula vyenye vipande vya kutafuna

Dk Ngairo amewataka wazazi kuzingatia kutoweka chumvi wala sukari katika chakula cha mtoto hadi anapofikisha umri wa mwaka mmoja ili kulinda figo ya mtoto na kusaidia mtoto asipoteze hamu ya kula.

Hakikisha vyombo vya mtoto vinaoshwa ipasavyo huku chakula kikipikwa katika hali ya usafi ili kumuepusha na magonjwa pamoja na kuzingatia mbinu bora za ulishaji.

Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023

Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya. 

Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.

Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.

Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.

Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.

Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania

Dar es Salaam. Miongoni mwa masuala yanayogusa zaidi vijana wengi waliopo kwenye ndoa na wasio kwenye ndoa kwa sasa ni suala la kuwa na watoto. 

Miongoni mwa maswali makubwa huwa ni lini wapate watoto, idadi ya watoto lakini ni njia gani sahihi itakayomfanya wanawake vijana wasipate ujauzito bila kutarajia. Wataalamu wanasisitiza kuwa ni vema wazazi vijana wakapanga mipango yao vema ya kijamii na kiuchumi kabla ya kupata watoto. 

Hata hivyo, si watu wote wanapanga ipasavyo juu ya kupata watoto. Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa mwaka 2022 unabainisha kuwa nchini Tanzania takriban wanawake wanne kati ya 10 au asilimia 38 ya waliolewa wenye umri wa miaka 15 hadi 49 wanatumia njia ya aina yeyote ya uzazi wa mpango.

Ripoti ya utafiti huo uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa ushirikiano na taasisi nyingine iwepo Wizara ya Afya inabainisha ipo baadhi ya mikoa yenye kiwango kikubwa cha wanawake wenye wanaotumia ipasavyo njia za uzazi wa mpango ikiongozwa na Njombe huku mingine ikitumia kwa kiwango kidogo sana kama Simiyu. 

Je, waifahamu mikoa inayoongoza kwa matumizi ya njia za uzazi wa mpango Tanzania? 

Ulaji milo mitatu ya chakula bado kitendawili Tanzania

  • Idadi ya wanaokula milo mitatu yashuka kwa asilimia 8.2.
  • Mtanzania mmoja kati ya 10, anakula mlo mmoja wa chakula.
  • Uviko -19, uhaba wa chakula baadhi ya maeneo vyatajwa kama sababu.

Dar es Salaam. Wakati wataalamu wa afya wakihimiza kula milo mitatu ya chakula kwa siku au zaidi ili kuwa na afya bora, hali ni tofauti nchini Tanzania kwani idadi ya watu wanaokula milo mitatu kwa siku imeshuka kwa asilimia 8.2.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Kufuatilia Hali ya Kaya Tanzania (NPS) ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), idadi ya Watanzania wanaokula milo mitatu imeshuka kutoka asilimia 71.2 mwaka 2014/15 mpaka asilimia 63 mwaka 2020/21.

Hii ni kumaanisha kuwa kati ya Watanzania kumi ni sita ndio wanaokula milo mitatu ya chakula au zaidi kwa siku. 

Wakati idadi ya wanaokula milo mitatu au zaidi ikishuka, idadi ya wanaokula milo miwili hadi mmoja imeongezeka. Mathalani wanaokula mlo mmoja wameongezeka kutoka asilimia 0.6 mpaka 1.6 huku wanaokula milo miwili wakiongezeka kutoka 28.2 mpaka 35.4.

Uchambuzi wa takwimu uliofanywa na Nukta habari umebaini kuwa kwa mujjbu wa ripoti hiyo katika kila Watanzania kumi basi mmoja hula mlo mmoja tu wa chakula huku watatu kati ya 10 wakila milo miwili ya chakula.

Hata hivyo, hali ya ulaji wa chakula imeonekana mbaya zaidi katika maeneo ya vijijini kuliko mjini kwani, Watanzania waishio mjini wana wastani mzuri zaidi wa kula milo mitatu kwa asilimia 74.8 huku vijijini wakiwa na asilimia 57.3.

Vivyo hivyo, idadi ya wanaokula mlo mmoja vijijini ni kubwa zaidi ambao ni  asilimia 1.8 wakati mjini ni 1.2 huku asilimia ya wanaokula milo miwili vijijini ikiwa ni mara mbili zaidi ya wale waishio mjini.

Huenda hali hiyo imechangiwa na kuwepo kwa upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo hapa nchini hali iliyosababishwa na mtawanyiko wa mvua pamoja na visumbufu.


Soma zaidi


Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Chakula nchini ya mwaka 2020/21 imeeleeza kuwa pamoja na kuwa na ziada ya chakula halmashauri 17 kutoka mikoa nane nchini ilitarajiwa kukutana na uhaba wa chakula mwaka juzi.

“Upungufu huo umechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo mtawanyiko mbaya wa mvua, visumbufu vya mimea kama vile wanyamapori, ndege aina ya kwelea kwelea na viwavijeshi vamizi, ”  inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Aidha uwepo wa ugonjwa wa Uviko-19 uliathiri shughuli za kilimo kwani ulisababisha changamoto katika upatikanaji wa pembejeo muhimu za kilimo kama vile mbegu, mbolea, viuatilifu na zana za kilimo.

Janga hilo lilichangia watu kupoteza ajira na biashara, na hivyo kukosa kipato kwa ajili ya kukidhi ya mahitaji ya kila siku ya chakula. 


Tangazo:

Wanasayansi kuja na chanjo ya Uviko-19 ya kunywa

  • Matokeo ya utafiti wa awali yaonyesha mwitikio chanya. 
  • Inatarajiwa itachochea ongezeko la watu wanaopata chanjo.

Dar es Salaam. Huenda idadi ya watu wanaopata chanjo ya Uviko-19 ikaongezeka siku za usoni pale wanasayansi watakapokamilisha utafiti wao kuhusu chanjo ya ugonjwa huo ambayo mtu anaweza kuipata kwa kunywa.

Mpaka sasa katika aina zote za chanjo zilizoidhinishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), huingizwa katika mwili wa binadamu kwa kutumia njia ya sindano jambo ambalo limekuwa kigezo kwa baadhi ya watu kutochanja kwa kuogopa maumivu ya sindano.

Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya teknolojia ya nchini Marekani ya Cnet watafiti na wanasayansi wameongeza nguvu katika ugunduzi wa chanjo mpya kupitia mfumo wa upumuaji au kinywa.

Chanjo hiyo itakayofahamika kama QYNDR (kinder),  imeshakamilisha sehemu ya kwanza ya majaribio yake na sasa inasubiri fedha kwa ajili ya majaribio zaidi na kisha iingizwe sokoni.

Kwa mujibu wa Kyle Flanigan ambaye ni mtengenezaji wa chanjo hiyo, ‘kinder’ itatumia njia rafiki kuingia kwenye mwili wa binadamu.

Flanigan anasema matokeo ya utafiti wa chanjo hiyo yaliyofanyika nchini New Zealand yana mwitikio chanya ingawa bado hayajakaguliwa na mamlaka za kiafya za kimataifa.

“Si rahisi kutengeneza na kuifanya  na chanjo iweze kufanya kazi kupitia mfumo wa mmeng’enyo, tuligundua njia itakayoifanya chanjo ipite tumboni na kutoa matokeo yanayofaa, “ anasema Flanigan.

Habari za uwepo wa majaribio ya chanjo za Uviko-19 kwa njia ya mfumo wa mmeng’enyo wa chakula zinakuja kipindi ambacho mzalishaji wa chanjo za Pfizer anakabiliwa na ukosoaji mkubwa nchini Marekani kuhusiana na ufanisi wa chanjo zake.

Hata hivyo mpaka sasa WHO hawajatoa taarifa yoyote ya kuthibitisha shutuma hizo dhidi ya Pfizer zaidi ya kuendelea kusisitiza matumizi ya chanjo kwani zimesaidia kuokoa mamilioni ya maisha ya watu.

Wataalamu wa afya wanaendelea kusisitiza kuwa ugonjwa wa Uviko-19 bado upo na unaua  ingawa kwa kasi ndogo ambapo kwa mujibu wa WHO Januari 23 mwaka huu watu 1,017 walipoteza maisha siku hiyo huku jumla ya watu milioni 6.7 wakipoteza maisha tangu kuanza kwa janga hilo mwaka 2019.

Kraken: Kirusi kipya cha Uviko-19 kinachowatesa wanasayansi

  • Kinatajwa kuenea kwa kasi zaidi kuliko virusi vilivyopita.
  • Uwezo wa kubadili jeni zake ni miongoni mwa sababu.
  • Barakoa yatajwa kama njia bora zaidi ya kujikinga na kirusi hicho.

Dar es Salaam. Ingawa si jambo linalozungumzwa sana kwa sasa, lakini wasiwasi unaendelea kuongezeka kwa wanayansi ambao wanajaribu kutafuta ufumbuzi wa kukabiliana na makali ya kirusi kipya cha Uviko-19 ambacho kinaenea kwa kasi barani Ulaya.

Kirusi hicho kinachoitwa XBB.1.5 au Kraken ni matokeo ya mabadiliko ya kijeni ya kirusi aina ya Omicron XBB ambacho nacho kiliripotiwa kuwa na kasi kubwa katika kuenea kwake.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kirusi hicho kiliripotiwa kwa mara ya kwanza Oktoba 2022, nchini Marekani na sasa tayari kimeenea katika nchi 38 barani Ulaya ikiwemo Sweden, Kanada, Australia na Ufaransa.

Disemba mwaka jana, China ilitangaza kuwa wastani wa watu 60,000 walipoteza maisha kutokana na virusi vya Omicron aina ya BA.5.2 na BF.7 vilivyozuka nchini humo.


Soma zaidi:


Mapema Januari mwaka huu Mkurugenzi wa masuala ya Teknolojia kutoka WHO, Maria Van Kerkhove alisema kirusi hicho ndiyo kinaambukiza kwa kasi zaidi kuliko aina nyingine za virusi.

“Sababu kubwa ni kutokana na kirusi hiki kuwa na uwezo wa kubadilisha jeni zake mara kwa mara hivyo si rahisi kukidhibiti,” anasema Kerkhove.

Pamoja na kwamba kirusi hichi kinaenea kwa kasi bado hakuna uhakika kwamba kinaweza kusababisha maafa makubwa kuliko ilivyokuwa awali.

Kutokana na uwezo wa kirusi hicho kujibadili mara kwa mara kulingana na mazingira wataalamu wa afya wameshauri pamoja na chanjo ya uviko-19 njia inayotajwa kuwa na uhakika zaidi ni kuvaa barakoa muda wote mtu anapokuwa kwenye mikusanyiko.

Kwa mujibu wa Kituo Cha Kudhibiti Magonjwa nchini Marekani (CDC) mpaka sasa asilimia 43 ya visa vya maambukizi ya Uviko-19 nchini humo yamesababishwa na kirusi hicho kipya.


Tangazo


Ifahamu kansa ya shingo ya kizazi na athari zake

  • Husababishwa na maambukizi ya muda mrefu ya virusi vya  “human papilloma”
  • Virusi hivyo huenezwa kwa njia ya kujamiiana.
  • Upatikanaji duni wa kinga na matibabu huchangia asilimia 90 ya vifo duniani kote.

Dar es Salaam. Licha ya kuwepo nchini kwa miaka mingi kansa ya shingo  ya kizazi imeendelea kugharimu maisha ya wanawake wengi huku kukiwa na uelewa mdogo kuhusu chanzo cha ugonjwa huo na namna unavyoweza kuutibu.

Januari kila mwaka hutumika kutoa elimu na uelewa juu ya visababishi vya ugonjwa huo na jinsi ya kukabiliana nao kwa wasichana.

Taasisi ya Saratani ya Ocean Road inasema kwa kiasi kikubwa saratani hii husababishwa na maambukizi ya mda mrefu (persistence infection) ya virusi viitwavyo “human papilloma”, ambavyo huenezwa kwa njia ya kujamiiana. 

“Kawaida mwili una uwezo wa hudhibiti maambukizi haya yaingiapo mwilini, lakini yasipodhibitiwa kikamilifu na kuwepo mwilini kwa muda mrefu husababisha ugonjwa wa saratani ya shingo ya kizazi,” inasema taasisi hiyo.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema matibabu ya mapema yanaweza kuokoa maisha ya wanawake takriban 342,000 waliopoteza maisha kwa ugonjwa huo mwaka 2020 na wagonjwa wapya 604,000 waliopata maambukizi hayo duniani kote kwa mwaka huo huo.

“Knsa ya shingo ya kizazi inazuilika  lakini upatikanaji duni wa kinga, uchunguzi na matibabu huchangia asilimia 90 ya vifo,” linasema Shirika hilo.

Hata hivyo, kabla ya mtu kupata madhara anaweza kugundua mapema dalili za ugonjwa huo kwa kujifanyia uchunguzi mwenyewe.

WHO inasema inachukua miaka 15 hadi 20 kwa saratani ya shingo ya kizazi kukua kwa wanawake walio na kinga ya kawaida na miaka 5 hadi 10 tu kwa wanawake walio na kinga dhaifu, kama vile walio na maambukizo ya VVU ambayo hayajatibiwa.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks