Mapinduzi sekta ya benki Tanzania, kutoka ATM hadi mawakala

Dar es Salaam. Kwa mtazamo wa kawaida, ATM inaweza kuonekana kama huduma rahisi kwa mteja lakini kwa benki, ATM ni moja ya miundombinu yenye gharama kubwa zaidi kuiendesha.
Mtaalamu wa uchumi na fedha kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa Abel Kinyondo anaeleza kuwa kila ATM inahitaji uwekezaji mkubwa tangu mwanzo inaponunuliwa.
Profesa Kinyondo ameiambia Nukta Habari kuwa mbali na gharama ya kununua mashine, benki hulazimika kulipia eneo la kuiweka, umeme, huduma ya intaneti inayofanya kazi saa 24, ulinzi, matengenezo ya mara kwa mara pamoja na usafirishaji wa fedha kila mashine inapomaliza fedha.
“Kila ATM ni kama tawi dogo lisilo na wafanyakazi, lakini bado linahitaji gharama nyingi ili liendelee kufanya kazi kila siku,” anaeleza Profesa.
Anasema tofauti na ATM, wakala tayari anakuwa na mtaji wake, duka lake, eneo lake la biashara pamoja na baadhi ya miundombinu muhimu jambo linalozifanya benki kutoingia gharama kubwa kuanzisha kituo kipya cha huduma.
Kwa lugha rahisi ni kwamba wakala anasaidia benki kupunguza gharama za uendeshaji wakati akiendelea kutoa huduma zilezile kwa wateja.