Wanafunzi zaidi ya 5,000 wapata mikopo HESLB awamu ya pili
- Ni wanafunzi 5,168 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya Sh19.9 bilioni.
- Idadi hiyo inakamilisha orodha ya wanafunzi 52,473 wa mwaka wa kwanza ambao wamepangiwa mikopo hadi sasa.
Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya awamu ya pili ya wanafunzi 5,168 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya Sh19.9 bilioni kwa mwaka wa masomo 2020/21 unaotarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Novemba.
“Wanachotakiwa kufanya kwa sasa ni kutembelea katika akaunti zao za SIPA (Student’s Individual Permanent Account) walizotumia kuomba mkopo na watapata taarifa za kina kuhusu mkopo,” amesema Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru katika taarifa yake iliyotolewa Jumanne Novemba 17, Jijini Dar es Salaam.
Idadi hiyo ya wanafunzi waliopangiwa mkopo inakamilisha orodha ya wanafunzi 52,473 wa mwaka wa kwanza ambao wamepangiwa mikopo hadi leo yenye thamani ya Sh170.02 bilioni.
Mikopo hiyo husaidia wanafunzi kuweza kumudu gharama za masomo na maisha wakati wakiendelea na masomo ya elimu ya juu.
Soma zaidi:
- Waombaji 10,452 Heslb wapewa siku nne kurekebisha kasoro
- Heslb yaanika kozi zitakazopewa kipaumbele mikopo elimu ya juu 2019-2020
- TCU yaanika sifa za wanafunzi kujiunga vyuo vikuu Tanzania
Novemba 11, 2020, HESLB ilitangaza orodha ya awamu ya kwanza yenye wanafunzi 47,305 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya Sh150.03 bilioni.
Kati ya wanafunzi hao, wanaume walikuwa ni 26,964 sawa na asilimia 57.37 au zaidi ya nusu ya wanafunzi waliopata mikopo hiyo.
“Serikali imeshatupatia fedha na tumeanza kuzipeleka vyuoni…lengo letu ni kuhakikisha wanafunzi wenye sifa wanazikuta fedha vyuoni ambako watajisajili na kupokea ili watimize ndoto zao,” alisema Badru Novemba 14.
Kuhusu wanafunzi waombaji ambao maombi yao yalikua na upungufu, Badru amesema HESLB imetoa muda wa siku tano kuanzia kesho (Novemba 18, 2020) kurekebisha taarifa zao na kuzituma kwa njia ya mtandao.
“Tuna wanafunzi wachache ambao maombi yao yana upungufu ambao kuanzia kesho wataweza kuingia katika akaunti zao za SIPA walizotumia kuomba mkopo na kurekebisha kwa kuweka nyaraka sahihi na tutazifanyia uchambuzi na wenye sifa watapangiwa mikopo mapema iwezekanavyo,” amesema Badru.
Katika mwaka 2020/21, Serikali imetenga Sh464 bilioni kwa ajili ya kugharamia mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu 145,000 wakiwemo wanafunzi 54,000 wa mwaka wa kwanza na wanafunzi 91,000 wanaoendelea na masomo.