Waliopata mikopo awamu ya tatu elimu ya juu hawa hapa
- Wanafunzi zaidi ya 15,000 wamepata mikopo hiyo awamu ya tatu.
- Idadi hiyo inafanya wanufaika hadi sasa kufikia 60,356.
- Wanafunzi awamu ya tatu kutangazwa hivi karibuni.
Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya awamu ya tatu yenye wanafunzi 15,261 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya Sh37.9 bilioni kwa mwaka wa masomo 2021/22.
HESLB imetoa taarifa hiyo leo Oktoba 26, 2021 ikiwa ni siku chache kabla ya vyuo vikuu kufunguliwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Mkurugenzi wa Upangaji na Utoaji Mikopo wa HESLB, Dk Veronica Nyahende amesema orodha iliyotolewa leo inafanya jumla ya wanafunzi wapya wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo kufikia 60,356 ambao wamepata mkopo wenye thamani ya Sh157.3 bilioni.
Dk. Nyahende amesema, tayari HESLB imeanza kupeleka fedha za wanafunzi waliopangiwa mikopo kwa awamu zote tatu katika vyuo mbalimbali.
Wanafunzi wametakiwa kupata taarifa za kina katika akaunti walizotumia kuomba mkopo maarufu kama SIPA (Student’s Individual Permanent Account) ili kujiandaa kwenda vyuoni kwa ajili ya kujisajili.
Orodha nyingine kuja baadaye
Dk Nyahende amesema orodha ya awamu ya nne itatolewa siku chache zijazo baada ya kukamilisha uchambuzi wa maombi unaoendelea na kuwataka waombaji mikopo kutembelea akaunti zao za SIPA kupata taarifa kuhusu maombi yao.
“Orodha hii ya tatu inajumuisha wanafunzi wenye sifa zikiwemo kuwa wahitaji, wameomba kwa usahihi na wamekamilisha taratibu za udahili wa chuo kimoja. Tunakamilisha uchambuzi wa maombi mengine na tutatoa orodha ya awamu ya nne siku chache zijazo,” amesema Dk Nyahende.
Serikali imetenga Sh570 bilioni kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka 2021/22 kwa wanafunzi 160,000 wa elimu ya juu.
Kati yao, wanafunzi 70,000 ni wanufaika wa mwaka wa kwanza na wanafunzi zaidi ya 90,000 ni wale wanaoendelea na masomo baada ya kufaulu mitihani yao ya mwaka.
“Serikali imeshatupatia fedha na tumeanza kuzipeleka vyuoni … lengo letu ni kuhakikisha wanafunzi wanaopangiwa wanazikuta fedha vyuoni ambako watajisajili na kupokea fedha ili watimize ndoto zao,” amesema Dk Nyahende akitoa wito wa utulivu kwa waombaji wa mikopo wanaosubiri awamu inayofuata.
Latest
