Njia za kumsaidia mtoto wako kupenda hisabati

  • Ni pamoja na kumpongeza na kumnunulia vitabu na programu za kielimu.
  • Mueleze mtoto umuhimu wa hisabati katika maisha yake ya kila siku.

Dar es Salaam. Somo la hisabati limekuwa kama ugonjwa usio natiba kwa wanafunzi wa ngazi mbalimbali za elimu nchini Tanzania. 

Hili limekuwa likijidhirisha katika matokeo ya mitihani ya kitaifa. Ufaulu wa wanafunzi katika somo hili umekuwa wa chini zaidi kuliko masomo mengine. 

Mathalani, katika matokeo ya kidato cha nne mwaka 2024 yaliyotolewa na Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), ni asilimia 25.35 ya watahiniwa waliofanya mtihani wa hisabati, ndio walifaulu kwa kupata daraja A hadi D. 

Hiyo ni sawa kusema karibu robo tatu (wanafunzi 7 kati ya 10) walifeli somo hilo. Pia umefaulu huo wa mwaka jana umeshuka kutoka asilimia 25.42 iliyorekodiwa mwaka 2023. 

Suala hili la kufanya vibaya kwa wanafunzi katika somo la hisabati, limekuwa likiibua maswali mengi yasiyo na majibu miongoni mwa wazazi, walimu na wadau wa elimu. Baadhi ya wadau wanapendekeza uitishwe mjadala wa kitaifa kutafuta suluhu ya kudumu kuwawezesha wanafunzi kufanya vizuri katika soko hili. 

Mchambuzi wa masuala ya elimu na mwandishi wa vitabu, Richard Mabala amewahi kuiambia Nukta Habari (nukta.co.tz) kuwa suluhu ya pamoja itakayohusisha makundi yote kwenye jamii, inaweza kutoa mwelekeo mpya wa hisabati na kuwafanya wanafunzi wengi walipende somo hilo. 

Wadau wengine wa elimu wanasema mbinu shirikishi za ufundishaji zinaweza kusaidia wanafunzi kupenda somo hilo. 

Picha hii imetengenezwa kwa Akili Unde ikiwa lengo ni kukuonyesha namna unavyoweza kushirikiana na mwanao kuhakikisha anaelewa soma la hesabu.

Mwalimu wa hisabati kutoka Shule ya Sekondari Aga Khan Mzizima jijini Dar es Salaam, Veronica Sarungi, anasisitiza kuwa inawezekana kumfanya mwanafunzi kupenda hisabati kwa kutumia mbinu sahihi ikiwemo kutokumkatisha tamaa mtoto pale anapokuwa amefanya vibaya katika somo hilo. 

Ni kawaida kwa wazazi, walimu na hata wanafunzi wenzao kuwatisha watoto kwa kauli kama “Hisabati ni ngumu” au “Wewe huwezi hesabu.” 

Mwalimu Veronica anasema kauli hizo zina athari mbaya kwa watoto, kwani huwafanya kujiwekea vikwazo vya kisaikolojia na kuamini kuwa hawana uwezo wa kufanikisha somo hili. 

Badala ya kuwatia hofu, ni muhimu kuwahamasisha watoto kwa kuwatia moyo hata wanapokosea.

“Kwa mfano, mzazi au mwalimu anaweza kumwambia mtoto kuwa makosa ni sehemu ya kujifunza na mafanikio yanapatikana kwa kufanya mazoezi. Hili litawapa wanafunzi ujasiri wa kukabiliana na changamoto za somo hili bila woga,” anasema Mwalimu Veronica. 

Pia wape watoto changamoto ndogo ndogo wanazoweza kuzitatua kwa urahisi. Hii itawasaidia kuona hisabati sio somo gumu kama wanavyodhani au kuaminishwa. 

Mtaalam huyo wa hesabu anawashauri walimu wanaofundisha somo hilo kutumia mbinu za kisaikolojia zinazosaidia kujenga ujasiri wa wanafunzi. 

Mbinu rahisi kama kuanzisha maswali ya msingi, kuelezea dhana kwa njia ya mfano, na kuwapongeza kwa juhudi zao zinaweza kubadilisha mtazamo wao kuhusu hisabati.

Tumia mfano wa maisha halisi

Hisabati ipo kila mahali katika maisha yetu ya kila siku, na njia moja ya kumfanya mtoto aipende ni kuhusianisha somo hili na mazingira yanayomzunguka. 

Kwa mfano, mzazi anaweza kumwonyesha mtoto jinsi ya kuhesabu fedha anaponunua vitu dukani, kupanga bajeti ya matumizi ya nyumbani, au hata kupima vitu kama urefu na uzito.

Mfano mwingine ni michezo rahisi ya namba. Watoto wengi hupenda kucheza, na kwa kutumia michezo inayojumuisha hesabu, unaweza kuwafanya wajifunze kwa furaha.

Watoto wengi hupenda kucheza na kwa kutumia michezo inayojumuisha hesabu husaidia kuwajengea kumbukumbu nzuri kichwani. Picha/ Akili unde.

Hii huwasaidia kuelewa kuwa hisabati si somo la darasani tu bali ni ujuzi wa maisha ambao kila mtu anahitaji.

Pia katika shughuli za kila siku, mzazi anaweza kumuuliza mtoto maswali rahisi ya kihisabati kama, “tuna vijiko 10, tukiondoa viwili, vitabaki vingapi?”. 

Kwa njia hii, mtoto anapata fursa ya kujifunza hisabati kwa vitendo, jambo linalowafanya kuona somo hili kuwa la kufurahisha na linalotumika kila siku.

Nunua vitabu na programu za hisabati

Vitabu vya mazoezi ya hisabati ni nyenzo muhimu ya kujifunza, hasa kwa watoto wanaopenda kujifunza wakiwa nyumbani. 

Vitabu hivi vina maswali ya ngazi mbalimbali, kuanzia maswali rahisi hadi magumu, ambayo yanaweza kumsaidia mtoto kukuza maarifa yake hatua kwa hatua. 

Kwa mfano, vitabu vya watoto wa shule za msingi vinaweza kuwa na michoro na mifano ya kuvutia inayorahisisha uelewa wa dhana za msingi.

Uwepo wa vitabu mbalimbali humsaidia mtoto kuwa na uwezo wa kufanya maswali mengi kutoka kwenye vitabu tofauti. Picha/ Canva.

Kwa upande wa teknolojia, mzazi anaweza kutumia simu janja au kompyuta kuhamasisha mtoto kujifunza kupitia programu za kielimu.

Kuna programu nyingi za bure zinazopatikana mtandaoni ambazo zina michezo na maswali yanayofundisha hisabati kwa njia za kuvutia. 

Michezo kama hii inachochea ubunifu na hamasa kwa watoto, kwani wanajifunza kwa kucheza badala ya kuhisi wanalazimishwa.

Mbali na teknolojia, wazazi wanaweza kutumia majukwaa kama YouTube ambapo walimu wa hisabati huchapisha video za elimu. 

Video hizi zinaweza kuwa msaada mkubwa kwa watoto wanaopenda kujifunza kwa njia ya kuona, na zinawapa nafasi ya kurudia masomo mara kadhaa hadi waelewe kikamilifu.

Toa zawadi kwa mtoto akifanya vizuri

Kwa mfano, mzazi anaweza kumwekea mtoto changamoto ndogo, kama kumaliza maswali 10 ya hisabati, na kumpa zawadi endapo atamaliza kwa usahihi. 

Kulinganana tovuti ya Mrs Mayers Leaning Lab, watoto wanahamasika zaidi wanapopewa zawadi au pongezi kwa juhudi zao. 

Zawadi hizi zinaweza kuwa za vifaa kama kalamu, daftari, au hata vitu vidogo wanavyopenda, au maneno ya kuwahamasisha kama “Umefanya vizuri sana leo.”

Hii huwafanya watoto kuona hisabati kama mchezo wa kufurahisha unaowapa zawadi badala ya mzigo wa kimasomo unaowakandamiza.

Zawadi ni kitu kinachopendwa na kila mtu hivyo kumpa mtoto zawadi baada ya kufanya vizuri itamfanya kuongeza jitihada zaidi. Picha/ Canva.

Zaidi ya hayo, zawadi hizi huchochea ushindani wa afya ya akili miongoni mwa wanafunzi wa darasa moja au familia moja. 

Watoto wanapojua kuwa juhudi zao zinathaminiwa, wanakuwa na hamu zaidi ya kujifunza na kushinda changamoto nyingine. Hii huwasaidia kujiamini zaidi na kuona hisabati kama somo linalowezekana.

Michezo ya hisabati

Michezo ya namba ni njia bora ya kuwafanya watoto kushiriki kikamilifu katika kujifunza hisabati. 

Kwa mfano, michezo kama sudoku, ‘bingo’ ya namba, au kutafuta mifumo ya namba husaidia watoto kuboresha uwezo wao wa kufikiri.

Wakati wa kucheza, mzazi au mwalimu anaweza kuelezea dhana za hisabati zinazojitokeza kwenye mchezo husika, kama vile kujumlisha, kutoa, kuzidisha, au kugawanya.

Kwa kutumia michezo mbalimbali kunaweza kumsaidia mtoto kuwa na kumbukumbu za muda mrefu. Picha/ Canva.

Hii huwafanya watoto kuelewa kuwa hisabati si tu namba za kubahatisha bali ni somo linalohitaji mbinu na mikakati.

Michezo inayohusisha mashindano huwafanya watoto kuwa na hamu zaidi ya kushiriki. Wanafurahia changamoto wanapojaribu kuwashinda wenzao, huku wakiwa wanajifunza hisabati kwa vitendo. Kwa njia hii, hisabati inakuwa somo la kufurahisha na linalochochea maarifa mapya.

Tumia vifaa vya kuonyesha na vitu halisi

Watoto huelewa vizuri zaidi wanapofundishwa kwa kuona vitu halisi. Kwa mfano, walimu na wazazi wanaweza kutumia maharage, sarafu, au vijiti vya plastiki kufundisha dhana kama kuhesabu, kujumlisha, au kugawanya.

Mbali na vitu vya asili, chati na michoro pia ni nyenzo bora za kufundishia. 

Hii huwafanya watoto kuelewa dhana ngumu kwa urahisi zaidi ukilinganisha na njia za kawaida. Picha/ Canva.

Chati zinaweza kusaidia kuelezea mifumo ya namba, kama vile jedwali la kuzidisha, huku michoro ikielezea dhana za kijiometri kama pembe, mistari, na maumbo. Hii huwafanya watoto kuelewa dhana ngumu kwa urahisi zaidi.

Hii itawasaidia watoto kufikiri kuwa hisabati ni somo la vitendo na siyo nadharia pekee.

Anzisha mashindano ya hisabati

Mashindano ya hisabati ni njia nzuri ya kuwafanya watoto kujifunza kwa njia ya ushindani. 

Mashindano haya huwapa watoto nafasi ya kuonyesha maarifa yao, kujifunza kutoka kwa wenzao, na kupata hamasa ya kushinda zawadi au kutambuliwa.

Kwa mfano, kuna mashindano ya hisabati yanayoandaliwa na shule, vyuo, au taasisi za elimu, ambapo wanafunzi hushindana kutatua maswali ya hesabu kwa muda mfupi. Watoto wanaposhiriki katika mashindano haya, wanajifunza kushughulikia changamoto kwa haraka na kwa usahihi.

Kwenye mashindano siku zote kila mtu huwa na shauku ya kushinda hivyo na kwa watoto ushindani huwapa hamu ya kuwa bora zaidi. Picha/ Canva.

Kupitia mashindano haya, watoto hupata uzoefu wa kushirikiana na wenzao, jambo linalowasaidia kuboresha ujuzi wa kijamii na kuimarisha hamasa yao ya kujifunza. 

Wazazi wanashauriwa kuwatafutia watoto wao mashindano yanayofaa kulingana na umri na uwezo wao.

Elezea umuhimu wa hisabati katika maisha

Watoto mara nyingi huona hisabati kama somo lisilo na faida ya moja kwa moja katika maisha yao ya kila siku. 

Kwa kubadilisha mtazamo huu, mzazi au mwalimu anaweza kuwaonyesha umuhimu wa hisabati kwa kuelezea jinsi inavyotumika katika kazi mbalimbali kama biashara, uhandisi, sayansi, na hata burudani.

Kwa mfano, msanii wa muziki anahitaji hisabati ili kupanga bajeti ya muziki wake, huku mwanamichezo akitumia hisabati kupima muda na umbali wa mazoezi yake. 

Ni vyema kuwajengea uwezo wa kujitambua mapema watoto ili kadri wanavyokuwa wasione hesabu kama janga la Taifa. Picha/ Akili Unde.

Hii inawafanya watoto kuona hisabati kama nyenzo ya kufanikisha ndoto zao za maisha.

Kuelezea jinsi hisabati inavyotumika kusimamia fedha, kupanga ratiba, au hata kupima afya kunawapa watoto mtazamo wa kivitendo kuhusu somo hili. 

Matokeo yake ni kwamba wanajifunza kuipenda hisabati kwa sababu wanaona thamani yake katika maisha yao ya kila siku.

Kwa kutumia mbinu hizi, mzazi au mwalimu anaweza kubadilisha mtazamo wa mtoto kuhusu hisabati na kumfanya aipende na kuimudu kwa urahisi.

Undani idadi ya watalii wa kigeni ndani ya miaka 10 Tanzania

Katika kipindi cha miaka 10, Tanzania imepokea jumla ya watalii wa kigeni 13,711,190, ikiimarisha nafasi yake kama moja ya vivutio vikuu vya utalii barani Afrika. Mwaka 2024 umeibuka kuwa wenye mafanikio makubwa zaidi kwa sekta ya utalii, ukivutia watalii 2,141,895, idadi kubwa zaidi katika muongo mmoja.

Kwa upande mwingine, mwaka 2020 uliathirika pakubwa na janga la Uviko-19, ukirekodi idadi ndogo zaidi ya watalii 620,867. Hii inamaanisha kuwa idadi ya watalii walioingia mwaka 2024 ni mara tatu zaidi ya ile ya mwaka 2020, sawa na ongezeko la asilimia 244.9.

Mfumuko huu wa watalii unaonyesha mwelekeo mzuri wa sekta ya utalii, ambayo ina mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kwa kuongeza fedha za kigeni, fursa za ajira, na ukuaji wa biashara za ndani. Tanzania inaendelea kunufaika na vivutio vyake vya kipekee kama Hifadhi ya Serengeti, Mlima Kilimanjaro, Kreta ya Ngorongoro, na fukwe za Zanzibar.

Idadi ya watalii wa kigeni yapaa Tanzania

Tanzania imeendelea kung’ara katika sekta ya utalii baada ya kurekodi ongezeko kubwa la idadi ya watalii wa kigeni mwaka 2024. Kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jumla ya watalii 2,141,895 waliingia nchini, ikiwa ni ongezeko la asilimia 18.58 ikilinganishwa na mwaka 2023.

Hii ni mara tatu zaidi ya idadi ya watalii walioingia nchini mwaka 2020 wakati dunia ilipokumbwa na janga la Uviko-19, ambapo ni 620,867 pekee waliotembelea Tanzania.

Kwa upande wa miezi, Julai umeibuka kinara kwa kuvutia wageni wengi zaidi, huku watalii 218,065 wakiwasili nchini. Kinyume chake, Aprili ndiyo ilikuwa na idadi ndogo zaidi, ikiwa na watalii 116,280 pekee.

Ongezeko hili linaonyesha mvuto wa Tanzania kama kivutio cha utalii duniani, huku vivutio kama Hifadhi ya Serengeti, Mlima Kilimanjaro, na fukwe za Zanzibar vikichangia kwa kiasi kikubwa.

Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023

Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya. 

Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.

Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.

Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.

Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.

Tumbaku yazitikisa kahawa, korosho mauzo nje ya nchi Tanzania

  • Thamani ya mauzo nje ya nchi yaongezeka takriban mara mbili ndani ya mwaka mmoja.

Dar es Salaam. Tumbaku ni moja ya bidhaa tatu asilia zinazoongoza kwa kuuzwa kwa wingi nje ya Tanzania na zilizoingiza fedha nyingi za kigeni licha ya kupigwa vita na wadau wa afya kuwa inahatarisha maisha ya watumiaji. 

Kwa mujibu wa Ripoti ya Hali ya Uchumi Tanzania mwaka 2023 iliyotolewa na Wizara ya Fedha hivi karibuni, katika bidhaa za asilia zinazouzwa nje ya nchi tumbaku inachuana kwa mbali na kahawa na korosho. 

Korosho, kahawa, chai na mkonge ni miongoni mwa mazao makubwa ya asilia ambayo huchangia kwa kiwango kikubwa fedha za kigeni nchini ila ukuaji wa uzalishaji wa tumbaku umezidi kuyapiga kikumbo mazao hayo. 

“Mwaka 2023, thamani ya mauzo ya tumbaku nje ilikuwa Dola za Marekani milioni 340.4 (Sh828.2 bilioni) ikilinganishwa na Dola za Marekani milioni 178.5 (Sh411.5 bilioni) mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 90.7,” inasema ripoti hiyo iliyotolewa na Wizara ya Fedha.

Ripoti hiyo inaeleza kuwa mafanikio hayo yalitokana na kuongezeka kwa mauzo ya tumbaku kwa zaidi ya mara moja na nusu hadi kufikia tani 82,000 mwaka 2023 kutoka tani 49,300 mwaka 2022. 

Uuzaji wa zao hilo nje ya nchi ulienda sanjari na kiwango cha uzalishaji wa tumbaku ulioongezeka takriban mara mbili ndani ya mwaka mmoja kutoka tani 70,699 mwaka 2022 hadi tani 122,859 mwaka jana. 

Uzalishaji wa tumbaku umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka Tanzania jambo lililochochea ongezeko la kiwango cha zao hilo kuuzwa nje ya nchi. Picha: Akili Mnemba. Picha hii imetengenezwa na akili mnemba kwa ajili ya kuongeza muktadha kwenye makala hii tu na si kuonyesha uhalisia.

Bei yaibeba tumbaku

Wastani wa bei ya kuuza tumbaku uliongezeka kwa asilimia 14.5 katika soko la dunia na kufikia Dola za Marekani 4,150.8 (Sh11.1 milioni) kwa tani mwaka 2023 kutoka Dola za Marekani 3,624.1(Sh9.7 milioni) kwa tani mwaka 2022.

Ingawa kiasi cha wingi wa korosho kinachouzwa nje ya Tanzania ni zaidi ya mara mbili ya kiasi cha tumbaku na kahawa, thamani ya tumbaku kwenye soko la kimataifa inazidi kwa zaidi ya mara 1.5 ya thamani ya korosho na kahawa. 

Kwa hesabu hizo, tumbaku inakuwa bidhaa asilia yenye thamani kubwa zaidi inayouzwa nje ya nchi. Bidhaa nyingine zisizoasilia zinazochangia zaidi fedha za kigeni ni dhahabu, utalii na bidhaa za viwandani. 

Miaka ya hivi karibuni kumekuwa na hamasa kubwa ya kuongeza ufanisi katika uzalishaji wa tumbaku kwa kutumia mbinu za kisasa za kilimo na kuimarisha uchakataji wake ili kupunguza athari kwa mazingira.

Mfano, kampuni Mkwawa Tobacco Processing Limited (MTPL), imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika usindikaji tumbaku, ikiongeza ajira na kuinua uchumi wa wananchi na wafanyabiashara. 

Uwekezaji huo katika uzalishaji na usindikaji unaofanywa na wakulima na viwanda vya zao hilo, unafanya tumbaku kuwa ni miongoni mwa bidhaa asilia zinazochangia kiwango kikubwa kwenye pato la taifa.  

Pamoja na uwekezaji huo kumekuwa na presha kubwa kutoka kwa wadau wa afya hasa wanaharakati wakiitaka Serikali kudhibiti vikali uzalishaji na utumiaji wa tumbaku unaochangia maradhi kwa binadamu ikiwemo matatizo ya mapafu.

Enable Notifications OK No thanks