Njia za kumsaidia mtoto wako kupenda hisabati
- Ni pamoja na kumpongeza na kumnunulia vitabu na programu za kielimu.
- Mueleze mtoto umuhimu wa hisabati katika maisha yake ya kila siku.
Dar es Salaam. Somo la hisabati limekuwa kama ugonjwa usio natiba kwa wanafunzi wa ngazi mbalimbali za elimu nchini Tanzania.
Hili limekuwa likijidhirisha katika matokeo ya mitihani ya kitaifa. Ufaulu wa wanafunzi katika somo hili umekuwa wa chini zaidi kuliko masomo mengine.
Mathalani, katika matokeo ya kidato cha nne mwaka 2024 yaliyotolewa na Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), ni asilimia 25.35 ya watahiniwa waliofanya mtihani wa hisabati, ndio walifaulu kwa kupata daraja A hadi D.
Hiyo ni sawa kusema karibu robo tatu (wanafunzi 7 kati ya 10) walifeli somo hilo. Pia umefaulu huo wa mwaka jana umeshuka kutoka asilimia 25.42 iliyorekodiwa mwaka 2023.
Suala hili la kufanya vibaya kwa wanafunzi katika somo la hisabati, limekuwa likiibua maswali mengi yasiyo na majibu miongoni mwa wazazi, walimu na wadau wa elimu. Baadhi ya wadau wanapendekeza uitishwe mjadala wa kitaifa kutafuta suluhu ya kudumu kuwawezesha wanafunzi kufanya vizuri katika soko hili.
Mchambuzi wa masuala ya elimu na mwandishi wa vitabu, Richard Mabala amewahi kuiambia Nukta Habari (nukta.co.tz) kuwa suluhu ya pamoja itakayohusisha makundi yote kwenye jamii, inaweza kutoa mwelekeo mpya wa hisabati na kuwafanya wanafunzi wengi walipende somo hilo.
Wadau wengine wa elimu wanasema mbinu shirikishi za ufundishaji zinaweza kusaidia wanafunzi kupenda somo hilo.

Mwalimu wa hisabati kutoka Shule ya Sekondari Aga Khan Mzizima jijini Dar es Salaam, Veronica Sarungi, anasisitiza kuwa inawezekana kumfanya mwanafunzi kupenda hisabati kwa kutumia mbinu sahihi ikiwemo kutokumkatisha tamaa mtoto pale anapokuwa amefanya vibaya katika somo hilo.
Ni kawaida kwa wazazi, walimu na hata wanafunzi wenzao kuwatisha watoto kwa kauli kama “Hisabati ni ngumu” au “Wewe huwezi hesabu.”
Mwalimu Veronica anasema kauli hizo zina athari mbaya kwa watoto, kwani huwafanya kujiwekea vikwazo vya kisaikolojia na kuamini kuwa hawana uwezo wa kufanikisha somo hili.
Badala ya kuwatia hofu, ni muhimu kuwahamasisha watoto kwa kuwatia moyo hata wanapokosea.
“Kwa mfano, mzazi au mwalimu anaweza kumwambia mtoto kuwa makosa ni sehemu ya kujifunza na mafanikio yanapatikana kwa kufanya mazoezi. Hili litawapa wanafunzi ujasiri wa kukabiliana na changamoto za somo hili bila woga,” anasema Mwalimu Veronica.
Pia wape watoto changamoto ndogo ndogo wanazoweza kuzitatua kwa urahisi. Hii itawasaidia kuona hisabati sio somo gumu kama wanavyodhani au kuaminishwa.
Mtaalam huyo wa hesabu anawashauri walimu wanaofundisha somo hilo kutumia mbinu za kisaikolojia zinazosaidia kujenga ujasiri wa wanafunzi.
Mbinu rahisi kama kuanzisha maswali ya msingi, kuelezea dhana kwa njia ya mfano, na kuwapongeza kwa juhudi zao zinaweza kubadilisha mtazamo wao kuhusu hisabati.
Tumia mfano wa maisha halisi
Hisabati ipo kila mahali katika maisha yetu ya kila siku, na njia moja ya kumfanya mtoto aipende ni kuhusianisha somo hili na mazingira yanayomzunguka.
Kwa mfano, mzazi anaweza kumwonyesha mtoto jinsi ya kuhesabu fedha anaponunua vitu dukani, kupanga bajeti ya matumizi ya nyumbani, au hata kupima vitu kama urefu na uzito.
Mfano mwingine ni michezo rahisi ya namba. Watoto wengi hupenda kucheza, na kwa kutumia michezo inayojumuisha hesabu, unaweza kuwafanya wajifunze kwa furaha.

Hii huwasaidia kuelewa kuwa hisabati si somo la darasani tu bali ni ujuzi wa maisha ambao kila mtu anahitaji.
Pia katika shughuli za kila siku, mzazi anaweza kumuuliza mtoto maswali rahisi ya kihisabati kama, “tuna vijiko 10, tukiondoa viwili, vitabaki vingapi?”.
Kwa njia hii, mtoto anapata fursa ya kujifunza hisabati kwa vitendo, jambo linalowafanya kuona somo hili kuwa la kufurahisha na linalotumika kila siku.
Nunua vitabu na programu za hisabati
Vitabu vya mazoezi ya hisabati ni nyenzo muhimu ya kujifunza, hasa kwa watoto wanaopenda kujifunza wakiwa nyumbani.
Vitabu hivi vina maswali ya ngazi mbalimbali, kuanzia maswali rahisi hadi magumu, ambayo yanaweza kumsaidia mtoto kukuza maarifa yake hatua kwa hatua.
Kwa mfano, vitabu vya watoto wa shule za msingi vinaweza kuwa na michoro na mifano ya kuvutia inayorahisisha uelewa wa dhana za msingi.

Kwa upande wa teknolojia, mzazi anaweza kutumia simu janja au kompyuta kuhamasisha mtoto kujifunza kupitia programu za kielimu.
Kuna programu nyingi za bure zinazopatikana mtandaoni ambazo zina michezo na maswali yanayofundisha hisabati kwa njia za kuvutia.
Michezo kama hii inachochea ubunifu na hamasa kwa watoto, kwani wanajifunza kwa kucheza badala ya kuhisi wanalazimishwa.
Mbali na teknolojia, wazazi wanaweza kutumia majukwaa kama YouTube ambapo walimu wa hisabati huchapisha video za elimu.
Video hizi zinaweza kuwa msaada mkubwa kwa watoto wanaopenda kujifunza kwa njia ya kuona, na zinawapa nafasi ya kurudia masomo mara kadhaa hadi waelewe kikamilifu.
Toa zawadi kwa mtoto akifanya vizuri
Kwa mfano, mzazi anaweza kumwekea mtoto changamoto ndogo, kama kumaliza maswali 10 ya hisabati, na kumpa zawadi endapo atamaliza kwa usahihi.
Kulinganana tovuti ya Mrs Mayers Leaning Lab, watoto wanahamasika zaidi wanapopewa zawadi au pongezi kwa juhudi zao.
Zawadi hizi zinaweza kuwa za vifaa kama kalamu, daftari, au hata vitu vidogo wanavyopenda, au maneno ya kuwahamasisha kama “Umefanya vizuri sana leo.”
Hii huwafanya watoto kuona hisabati kama mchezo wa kufurahisha unaowapa zawadi badala ya mzigo wa kimasomo unaowakandamiza.

Zaidi ya hayo, zawadi hizi huchochea ushindani wa afya ya akili miongoni mwa wanafunzi wa darasa moja au familia moja.
Watoto wanapojua kuwa juhudi zao zinathaminiwa, wanakuwa na hamu zaidi ya kujifunza na kushinda changamoto nyingine. Hii huwasaidia kujiamini zaidi na kuona hisabati kama somo linalowezekana.
Michezo ya hisabati
Michezo ya namba ni njia bora ya kuwafanya watoto kushiriki kikamilifu katika kujifunza hisabati.
Kwa mfano, michezo kama sudoku, ‘bingo’ ya namba, au kutafuta mifumo ya namba husaidia watoto kuboresha uwezo wao wa kufikiri.
Wakati wa kucheza, mzazi au mwalimu anaweza kuelezea dhana za hisabati zinazojitokeza kwenye mchezo husika, kama vile kujumlisha, kutoa, kuzidisha, au kugawanya.

Hii huwafanya watoto kuelewa kuwa hisabati si tu namba za kubahatisha bali ni somo linalohitaji mbinu na mikakati.
Michezo inayohusisha mashindano huwafanya watoto kuwa na hamu zaidi ya kushiriki. Wanafurahia changamoto wanapojaribu kuwashinda wenzao, huku wakiwa wanajifunza hisabati kwa vitendo. Kwa njia hii, hisabati inakuwa somo la kufurahisha na linalochochea maarifa mapya.
Tumia vifaa vya kuonyesha na vitu halisi
Watoto huelewa vizuri zaidi wanapofundishwa kwa kuona vitu halisi. Kwa mfano, walimu na wazazi wanaweza kutumia maharage, sarafu, au vijiti vya plastiki kufundisha dhana kama kuhesabu, kujumlisha, au kugawanya.
Mbali na vitu vya asili, chati na michoro pia ni nyenzo bora za kufundishia.

Chati zinaweza kusaidia kuelezea mifumo ya namba, kama vile jedwali la kuzidisha, huku michoro ikielezea dhana za kijiometri kama pembe, mistari, na maumbo. Hii huwafanya watoto kuelewa dhana ngumu kwa urahisi zaidi.
Hii itawasaidia watoto kufikiri kuwa hisabati ni somo la vitendo na siyo nadharia pekee.
Anzisha mashindano ya hisabati
Mashindano ya hisabati ni njia nzuri ya kuwafanya watoto kujifunza kwa njia ya ushindani.
Mashindano haya huwapa watoto nafasi ya kuonyesha maarifa yao, kujifunza kutoka kwa wenzao, na kupata hamasa ya kushinda zawadi au kutambuliwa.
Kwa mfano, kuna mashindano ya hisabati yanayoandaliwa na shule, vyuo, au taasisi za elimu, ambapo wanafunzi hushindana kutatua maswali ya hesabu kwa muda mfupi. Watoto wanaposhiriki katika mashindano haya, wanajifunza kushughulikia changamoto kwa haraka na kwa usahihi.

Kupitia mashindano haya, watoto hupata uzoefu wa kushirikiana na wenzao, jambo linalowasaidia kuboresha ujuzi wa kijamii na kuimarisha hamasa yao ya kujifunza.
Wazazi wanashauriwa kuwatafutia watoto wao mashindano yanayofaa kulingana na umri na uwezo wao.
Elezea umuhimu wa hisabati katika maisha
Watoto mara nyingi huona hisabati kama somo lisilo na faida ya moja kwa moja katika maisha yao ya kila siku.
Kwa kubadilisha mtazamo huu, mzazi au mwalimu anaweza kuwaonyesha umuhimu wa hisabati kwa kuelezea jinsi inavyotumika katika kazi mbalimbali kama biashara, uhandisi, sayansi, na hata burudani.
Kwa mfano, msanii wa muziki anahitaji hisabati ili kupanga bajeti ya muziki wake, huku mwanamichezo akitumia hisabati kupima muda na umbali wa mazoezi yake.

Hii inawafanya watoto kuona hisabati kama nyenzo ya kufanikisha ndoto zao za maisha.
Kuelezea jinsi hisabati inavyotumika kusimamia fedha, kupanga ratiba, au hata kupima afya kunawapa watoto mtazamo wa kivitendo kuhusu somo hili.
Matokeo yake ni kwamba wanajifunza kuipenda hisabati kwa sababu wanaona thamani yake katika maisha yao ya kila siku.
Kwa kutumia mbinu hizi, mzazi au mwalimu anaweza kubadilisha mtazamo wa mtoto kuhusu hisabati na kumfanya aipende na kuimudu kwa urahisi.
Njia za kuiokoa Tanzania na janga la kufeli hesabu, sayansi
- Lugha ya kujifunzia na mtindo wa uulizaji maswali vyatajwa ni miongoni mwa sababu zinazofelisha wengi.
- Wadau wa elimu washauri Serikali kuongeza walimu na kuchunguza ubora wa walimu wa sayansi waliopo
- Wazazi watakiwa kuwasaidia watoto wao kufaulu masomo ya sayansi
Dar es Salaam. Kwa mara nyingine wanafunzi waliofanya mtihani wa Upimaji wa Kitaifa wa Kidato cha Pili (FTNA) mwaka 2022 wameingia kwenye historia ya watoto waliowahi kufanya vibaya zaidi kwenye masomo ya sayansi na hesabu Tanzania.
Katika matokeo yaliyotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani (Necta), kiwango cha ufaulu wa watoto hao siyo tu kuwa kimeshuka bali zaidi ya watahiniwa wanane kati ya 10 waliofanya mtihani huo Oktoba 2022 wamefeli Hisabati ama Basic Mathematics kwa kimombo dadi ambayo ni karibu sawa na wanafunzi waliofeli somo la Fizikia.
Ufaulu wa jumla umeporomoka kutoka asilimia 92 mwaka 2021 mpaka asilimia 85 mwaka 2022 huku ufaulu wa masomo ya sayansi ukiwa chini zaidi ya wastani wa masomo yote. Miaka ya nyuma ufaulu ulikuwa na mwenendo wa kupanda mwaka hadi mwaka.
Hali pia si shwari kwenye Kemia baada ya wanafunzi takriban saba kati ya 10 au asilimia 66 wakifeli somo la Kemia. Katika somo la Baiolojia nusu ya wanafunzi yaani asilimia 53 ya waliofanya mtihani nao walifeli somo la Baiolojia ambalo ni muhimu katika kufahamu bailojia ya binadamu, wanyama na mimea.
Sayansi, hesabu tatizo sugu
Hii si mara ya kwanza kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kufeli vibaya katika masomo ya hesabu na sayansi jambo linalotishia maendeleo ya Tanzania kupitia sayansi na teknolojia.
Baadhi ya wadau wa elimu nchini Tanzania wameiambia Nukta Habari kuwa miongoni mwa sababu za kushuka ufaulu ni pamoja na ugumu wa lugha ya kujifunzia sekondari ambayo ni Kingereza.
Mdau wa elimu Mwalimu Richard Mabala amesema kuwa lugha ya kujifunzia pamoja na namna maswali yalivyoulizwa ni miongoni mwa sababu iliyosababisha wanafunzi hao kufeli.
“Wanafunzi hawa hata matokeo yao ya darasa la saba yalionesha ufaulu katika somo la Kiingereza umeshuka sasa sekondari wameenda kukutana na masomo magumu zaidi katika lugha ambayo hawaijui vema lazima wafeli tu, “ amesema Mabala ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika lisilo la kiserikali la HakiElimu.
Baadhi ya walimu wanaeleza kuwa mabadiliko ya mara kwa mara katika mfumo wa uulizaji maswali huenda ni miongoni mwa sababu zilizofanya wanafunzi hao wa kidato cha pili kufeli vibaya sayansi na hesabu.
Mwalimu wa shule za Agha Khan jijini Dar es salaam Veronica Sarungi ameiambia Nukta Habari kuwa baada ya mtihani huo wa kidato cha pili alizungumza na wanafunzi na kumweleza kuwa mfumo waliokutana nao si ule waliokuwa wamewafundisha watoto hao.
Lugha ni tatizo?
“Maswali ni yale yale lakini yalikuwa katika mfumo wa mafumbo zaidi sasa mwanafunzi kwanza haifahamu vizuri hiyo lugha, halafu unamletea mfumo mgumu zaidi bila shaka hawezi kufaulu,” anasema Veronica na kubainisha kuwa mtihani wa mwaka jana una utofauti mkubwa na ile ya mwaka 2021 na 2020.
Wakati wadau hao wa elimu wakieleza hayo, Ripoti ya Uchambuzi wa Matokeo ya Shule ya Msingi ya mwaka 2020 iliyotolewa na Necta inaonesha somo la Kiingereza lilikuwa na ufaulu wa chini zaidi kuliko masomo yote likiwa na wastani wa asilimia 57.
Hii inamaanisha kwamba ni takriban wanafunzi sita tu kati ya 10 ambao ndio wamefanya mtihani wa kidato cha pili mwaka 2022, walifaulu mtihani wa Kiingereza mwaka 2020 katika matokeo ya darasa la saba.
Zinazohusiana
-
Ufaulu ya darasa la nne washuka kwa asilimia 3.35
- Watahiniwa zaidi ya 270 wafutiwa matokeo darasa la nne, kidato cha pili
Mbinu zitakazosaidia kuongeza ufaulu wa sayansi, hesabu
Baadhi ya wadau wa elimu wanaeleza kuwa mwarobaini wa tatizo hilo ni pamoja na Serikali kuongeza miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi kuelewa masomo ya sayansi na hesabu na kutazama upya lugha ya kufundishia ambayo mwanafunzi ataelewa.
“Ni wakati wa Serikali kuharakisha ukamilishaji wa sera ya lugha ya kujifunzia ili wanafunzi wasome kwa lugha wanayoielewa. Lugha inayotumika sana ni Kiswahili kwa kuwa hata nje ya masomo ndio hutumika zaidi katika nyanja zote za mwanafunzi huyu,” anasema Mabala ambaye ni mwandishi wa vitabu mbalimbali vikiwemo vinavyotumika shuleni.
Mabala anaeleza kuwa Serikali inatakiwa kuongeza vitabu vya kiada na ziada vya masomo hayo ya sayansi na hisabati ili watoto wapate wasaa mzuri wa kujisomea na kufanya mazoezi.
Ongeza walimu wenye ubora
Mbali na lugha ya kujifunzia, wataalamu wengine wanaeleza kuwa tatizo hilo litatuliwa iwapo Serikali itawekeza vilivyo katika kuongeza walimu wenye ubora katika masomo ya sayansi na hesabu.
Mhadhiri wa Uhandisi wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) Aviti Mushi anasema licha ya kwamba idadi ya walimu wa masomo ya sayansi kuwa si ya kuridhisha bado baadhi yao uwezo wao si wa kuaminika.
“Serikali inapaswa kuongeza idadi ya walimu wa masomo ya sayansi na hesabu lakini lazima kuwe na namna ya kupima ubora wa walimu hawa kabla hawajakabidhiwa jukumu la kufundisha…huenda hata sasa katika walimu kumi wawili au mmoja hawana ubora unaotakiwa, “ anasema Dk Mushi ambaye pia huandika vitabu vya kufundishia shuleni vikiwemo vya fizikia.
Suluhu ya masuala ya shuleni pekee huenda isimalize tatizo. Mwalimu Veronica anashauri kuwa wazazi wanatakiwa kuwa chachu ya kuwahimiza watoto kusoma vema masomo ya sayansi na hisabati badala ya kuwaacha wakate tamaa.
Wazazi msiwakatishe tamaa watoto
Sarungi amewashauri wazazi kuwa nguzo muhimu katika kuwatia moyo wanafunzi na kuwawezesha kwa vifaa na vitabu pale inapobidi na sio kuwapa kauli zinazowafanya wayachukie masomo ya sayansi na hesabu au kuyaona magumu zaidi.
“Mzazi anamwambia mtoto, umefeli hesabu usijari hata mimi nilifeli, mtoto anaona kumbe ni sawa tu kufeli. Hilo jambo sio sawa. Mzazi anatakiwa kumtia moyo kuwa leo umefeli kesho utafaulu ila ongeza bidii, hivyo ndivyo inavyotakiwa,” amesema Sarungi.
Tangazo: