Wamachinga Mwanza waitenga Machi 26 kuwa ‘Magufuli Day’

March 24, 2021 10:11 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Hatua hiyo ya Wamachinga imefuatia baada ya Hayati Magufuli wakati wa uhai wake kuwazuia viongozi wa Serikali kuwabugudhi wafanyabiashara wadogo
  • Awali walipanga kuadhimisha ‘Machinga Day’ kila Aprili lakini wamebadili baada ya kifo cha Rais John Magufuli.

Mwanza. Wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama machinga mkoani Mwanza wamekusudia kuifanya siku ya maziko ya Hayati Rais John Magufuli Machi 26 kila mwaka kuwa ni siku ya ‘Magufuli Day’ ili kuuenzi mchango wa kiongozi huyo katika kuboresha biashara zao.

Hatua hiyo ya Wamachinga mkoani humo imefuatia baada ya Hayati Magufuli wakati wa uhai wake kutoa maagizo kwa viongozi wa Serikali kutowabugudhi wafanyabiashara hao katika maeneo waliyokuwa wakiyafanyia biashara kwa kuwa ni wapiga kura wake.

Hayati Dk Magufuli alifariki juma lililopita jijini Dar es Salaam alikokuwa akipatiwa matibabu katika hospitali ya Mzena. 

Mwenyekiti wa Shirikisho la wafanyabiashara wadogo Machinga, mkoani Mwanza Matondo Masanja ameiambia Nukta Habari leo Machi 24 kuwa wamekusudia kuifanya siku ya mazishi ya hayati Magufuli kuwa Magufuli Day badala ya ‘Machinga Day’ waliyokuwa wameipanga.

Masanja amesema awali walipanga maadhimisho ya wamachinga yawe yanafanyika Aprili kila mwaka kumshukuru Rais Magufuli kwa kuwapatia fursa za kufanya shughuli zao kwa amani na kuwapatia vitambulisho ambavyo wanalipia fedha ndogo kwa mwaka mzima.  

“Lakini baada tu ya kupata taarifa za kifo chake tumeamua kubadilisha na sasa tutakuwa tunafanya kila ifikapo Machi 26 ili kumuenzi kwa yale aliyotutendea,” amesema Masanja.



Baadhi ya wafanyabiashara wengine wadogo wamesema kuwa kiongozi huyo, atakayezikwa Ijumaa hii wilayani Chato mkoani Geita, aliwaletea miradi mingi ya maendeleo na wanahofu iwapo watakuja kupata tena fursa hiyo siku zijazo.

“Amekuwa mwema, amekemea viongozi wabadhirifu, ametuletea miradi mingi sijui ni nani atavaa viatu vya kiongozi huyu mtetezi wa wanyonge,” amesema Amina Rashid, mfanyabiashara mdogo katika jiji hili huku akibubujikwa na machozi.

Baadhi ya akina mama wajasiriamali jijini Mwanza wamesema mikopo kwa wanawake inayotolewa na Serikali imewasaidia kuwainua kiuchumi jambo linalowafanya kumkumbuka Hayati Dk Magufuli mara kwa mara. 

Mwenyekiti wa kikundi cha Upendo, Martha Mlata amesema awali hawakuwa na uwezo  wa kuiendesha biashara zao kutokana na benki kutoza asilimia kubwa za riba iliyowafanya washindwe kupata mikopo hiyo.

“Baada tu ya uongozi wa awamu ya tano kuingia madarakani, Rais Magufuli  aliona ni vema na sisi watu wa chini  tupate mikopo hii ili itusaidie kukuza uchumi wetu,” amesema Martha na kueleza kuwa watamkumbuka kwa “mikopo ya asilimia tano”.

Martha pamoja na wanakikundi wenzake wamesema katika awamu hiyo wameweza kukopa zaidi ya Sh20 milioni ambazo wanazitumia katika uzalishaji mali.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW