Mwanza yazuia watoto, wazee kumuaga Magufuli uwanjani
- Mkuu wa mkoa asema wanaweza kukaa nyumbani na kufuatilia kwenye runinga.
- Hatua hiyo huenda ikaepusha wakazi hao na madhara ya msongamano mkubwa.
Mwanza. Zikiwa zimesalia chini ya Saa 24 ili wakazi wa Mwanza wamuage mpendwa wao hayati Rais John Magufuli, Serikali imewazuia wazee na watoto kwenda uwanja wa CCM Kirumba kutoa heshima za mwisho kuwaepusha na madhara yanayoweza kutokea kutokana na msongamano mkubwa.
Wakazi wa Mwanza wanatarajia kuuga mwili wa hayati Rais Magufuli mapema Machi 24 mwaka huu baada ya wenzao wa Zanzibar kufanya hivyo leo.
Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Mwanza John Mongella aliiambia kamati ya maandalizi Machi 22 jioni kuwa shughuli za kuaga mwili wa Rais Magufuli aliyefariki Machi 17 mwaka huu zitafanyika kwa amani na utulivu.
Hatua hiyo huenda ikasaidia kuepusha vifo na majeruhi katika msongamano mkubwa kama vilivyotokea wakati wa kuaga mwili wa kiongozi huyo jijini Dar es Salaam ambapo familia moja imeripotiwa kupoteza ndugu watano wakiwemo watoto wanne.
- Mkalimani kuagwa Hayati Magufuli azua gumzo mtandaoni
- Jinsi vijana wanavyoweza kuepuka presha ya kupata mafanikio
“Idara zote za ulinzi na usalama zimejipanga kuhakikisha ulinzi na usalama unaimarika, na nitoe ombi kwa wazazi na walezi kuhakikisha watoto wanabaki nyumbani wakitazama kwenye runinga kwa kuwa matangazo yanarushwa kwenye channel (idhaa) zote za ndani,” amesema Mongella ambaye ni mwenyekiti wa maandalizi hayo.
Mongella, ambaye alifika katika viwanja hivyo kushuhudia maandalizi ya uwanja huo, amesema anajua kuwa Rais Magufuli ni kipenzi cha watu wa Mwanza na Kanda ya Ziwa hivyo wanategemea idadi kubwa ya watu.
Kuhusu ratiba ya kuaga, amesema mageti ya kuingilia uwanjani yatafunguliwa kuanzia saa 10 usiku na mwili utapokelewa uwanja wa ndege saa 1 asubuhi ukitokea Zanzibar.
Baada ya kupokea uwanja wa ndege, mwili huo wa Rais Magufuli utapelekwa uwanjani moja kwa moja kisha sala, dua na maombezi yatafanyika.
Baadae viongozi mbalimbali wa kitaifa na mkoa watatoa heshima zao za mwisho kisha mwili kuruhusiwa kupitishwa kwenye barabara mbalimbali za mkoa wa Mwanza.
Kwa mujibu wa Mongella, barabraba ambazo mwili huo utapitishwa ni makongoro, Pasiansi, musumbiji, Mwontensori, Loreto, Buzuruga, Babati, na Mjinj kati. barabara nyingine ni CCM mkoa, Igogo, Nyegezi, mkolani, Buhongwa, Usagara, Kigongo kisha utavuka maji kwenda Sengerema.
Amewaomba wananchi kujitokeza na kuweka na staha kwenye msafara ili kuhakisha mtu yeyote hadhuriki.
Latest