Vita ya Iran yapaisha bei ya petroli, dizeli kwa wastani wa Sh953 Tanzania

April 1, 2026 3:50 am · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Petroli inayopitia Bandari ya Dar es Salaam inauzwa kwa bei ya reja reja ya Sh 3,820 na dizeli ShSh3,806.

Arusha. Vita ya Mashariki ya Kati inayoendelea kati Marekani na Israel dhidi ya Iran imepaisha bei  ya mafuta ya petroli na dizeli kwa wastani wa Sh953 kwa mwezi Aprili nchini Tanzania na kuacha maumivu kwa watumiaji wa vyombo vya moto.

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) leo Aprili Mosi, 2026 imetangaza ongezeko la bei ya mafuta  ya  petroli kwa Sh958  na dizeli kwa Sh948.

Kwa ongezeko hilo petroli inayopitia Bandari ya Dar es Salaam itauzwa kwa bei ya reja reja ya Sh 3,820 kutoka ShSh2,864 kwa lita iliyokuwa ikitumika mwezi Machi huku dizeli ikinunuliwa kwa Sh3,806.

Ongezeko hilo pia limewafikia wanaotumia mafuta kupitia Bandari ya Tanga ambapo dizeli imepanda hadi  Sh3,881 kutoka Sh2,925 mwezi Machi na dizeli imeuzwa kwa Sh3,867 kutoka Sh2,919 kwa lita.

Hata katika Bandari ya Mtwara bei hiyo imeongezeka kufikia Sh3,912 kwa petroli kutoka Sh2,956 na dizeli imefikia Sh3,898 kutoka Sh2,951 iliyokuwa ikitumika Machi.

Hili ni ongezeko la kwanza kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Tanzania ikichangiwa zaidi na athari za vita ya Marekani na Israeli dhidi  ya Irani iliyoanza Februari 28, 2026 na kuacha athari katika maghala na visima vya  mafuta.

“…Kushambuliwa kwa visima vya mafuta, maghala ya kuhifadhi mafuta na viwanda vya kusafisha mafuta (refineries) pamoja na Irani kufunga Lengo la Hormuz linalopitisha takriban asilimia 20 ya mafuta yanayosafirishwa kwenda kwenye masoko mbalimbali duniani, imeathiri hali ya uzalishaji mafuta kwenye nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza kwa kiasi kikubwa.

…Imeongeza gharama za usafirishaji kutokana na kukosekana kwa mali za kusafirisha mizigo na imeongeza gharama za bima za mali za mizigo kutokana na vita,” imesema Ewura.

Mapema mwezi Machi Rais Samia Suluhu Hassan alidokeza kuwa vita hiyo imesababisha mafuta kupaa kwa asilimia 13 akiitaka Wizara ya Nishati na Ewura kujipanga kuweka akiba.

“Niwatake wizara kuimarisha akiba ya  kimkakati ya mafuta lli kuongeza uwezo wa nchi kujilinda dhidiya  misukosuko ya kimataifa ya nishati ikiwemo mabadiliko ya bei katika soko la dunia.

…Kama tunavyoona misukosuko iliyotokea imepandisha bei  kwa asilimia 13 mpaka jana (Machi 2. 2026),” alisema Rais Samia katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi mradi wa ujenzi wa matanki ya kupokea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam Machi 3 mwaka huu.

Bei ya bidhaa, huduma kupaa

Katika mahojiano na Nukta Habari hivi karibuni Profesa wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Abel Kinyondo alisema kuwa bidhaa zinaweza kupanda bei kutokana na kuongezeka kwa gharama za uzalishaji na usafirishaji katika katika shughuli muhimu za kiuchumi kama vile viwanda na usafirishaji.

“Mafuta ni bidhaa muhimu sana kwenye uchumi…mafuta yakipanda bei karibu kila kitu kingine kinapanda bei,” amesema Prof Kinyondo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks