Ahueni bei ya mafuta ikishuka kiduchu
- Bei ya petroli imepungua kwa Sh92 kwa lita, dizeli kwa Sh204 kwa lita, huku mafuta ya taa yakishuka kwa Sh440 kwa lita ikilinganishwa na viwango vya mwezi uliopita.
Dar es Salaam.Huenda watumiaji wa vyombo vya moto nchini Tanzania wakaendelea kushuhudia ahueni ya gharama za mafuta baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) kutangaza kushuka kwa bei kikomo za petroli, dizeli na mafuta ya taa kuanzia leo, Jumatano Agosti 5, 2026.
Taarifa ya Ewura imeeleza kuwa mabadiliko hayo yametokana na mwenendo wa bei katika soko la dunia, ambalo limeendelea kushuhudia mabadiliko yanayoathiri gharama za uagizaji wa mafuta kutokana na vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati.
“Katika mwezi Agosti bei za mafuta hapa nchini zimepungua kwa Sh92 kwa lita ya petroli, Sh204 kwa lita ya dizeli na Sh440 kwa lita ya mafuta ya taa,” imesema sehemu ya taarifa hiyo.
Kwa viwango vipya, lita moja ya petroli inayopitia Bandari ya Dar es Salaam itauzwa kwa bei kikomo ya Sh3,898 kutoka Sh3,990 mwezi Julai, huku dizeli ikishuka hadi Sh3,978 kutoka Sh4,182. Mafuta ya taa nayo yatakuwa yanauzwa kwa Sh4,003 kutoka Sh4,443 mwezi uliopita.
Kwa upande wa Bandari ya Tanga, bei ya petroli ni Sh3,959 kwa lita, dizeli Sh4,039 na mafuta ya taa Sh4,065. Mkoani Mtwara, petroli itauzwa kwa Sh3,990 kwa lita, dizeli Sh4,070 na mafuta ya taa Sh4,096.
Mwezi wa pili wa nafuu
Huu ni mwezi wa pili mfululizo kwa bei za mafuta kushuka nchini baada ya Ewura pia kupunguza bei mwezi Julai, hali inayotoa nafuu kwa watumiaji na wafanyabiashara wanaotegemea mafuta katika shughuli zao za kila siku.
Kwa bei hizo mpya, Sh10,000 itanunua takribani lita 2.57 za petroli ikilinganishwa na lita 2.51 zilizopatikana mwezi Julai. Kwa watumiaji wa dizeli, kiasi hicho kitanunua takribani lita 2.51 kutoka lita 2.39 zilizokuwa zinapatikana mwezi uliopita.
Wafanyabiashara waonywa
Mamlaka hiyo imeeleza kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Mafuta ya mwaka 2015, bei za bidhaa za mafuta zitaendelea kuamuliwa na ushindani wa soko, huku Ewura ikiendelea kutangaza bei kikomo ili kulinda ushindani na maslahi ya watumiaji.
Aidha, kampuni za mafuta zinaruhusiwa kuuza mafuta kwa bei ya ushindani, mradi zisizidi bei kikomo iliyowekwa au kushuka chini ya bei ya chini inayoruhusiwa kwa mujibu wa Kanuni za Ewura za Kupanga Bei za Mafuta za mwaka 2022 pamoja na marekebisho yake.
Ewura pia imezitaka vituo vyote vya mafuta kuweka mabango yanayoonyesha wazi bei za bidhaa, punguzo na vivutio vya kibiashara vinavyotolewa. Mamlaka hiyo imesema ni kosa kuuza mafuta bila kuonyesha bei inayoonekana kwa wateja na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka masharti hayo.
Ewura imeonya kuwa itachukua hatua kali za kisheria dhidi ya mfanyabiashara yeyote atakayekiuka bei kikomo au masharti mengine yaliyowekwa katika kanuni za biashara ya mafuta.