Uzushi: Hakuna mabadiliko ya uwasilishaji nyaraka za vibali vya kazi Tanzania
- Ni uzushi unaosema kuwa kutokana na Corona utaratibu kuwasilisha nyaraka hizo umebadilika.
- Ofisi ya Waziri Mkuu yasema hakuna mabadiliko yoyote.
Dar es Salaam. Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu imeeleza kuwa hakuna mabadiliko yoyote ya utaratibu wa uwasilishaji wa maombi ya vibali vya kazi, rufaa na msamaha ili kujikinga na janga la Corona.
Tamko la ofisi hiyo limekuja wakati kukiwa na taarifa za mtandaoni zinazoeleza kuwa kutokana na kuwepo kwa COVID-19, nyaraka hizo zinatakiwa ziwasilishwe makao makuu ya Idara ya Kazi zikiwa zimethibitishwa na wanasheria wa Serikali na risiti ya malipo.
Taarifa hiyo inaeleza zaidi kuwa mabadiliko hayo yatasaidia kujikinga na maambukizi ya COVID-19 wakati uwasilishaji wa nyaraka hizo.

Hata hivyo, taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu Februari 1, 2020 imeeleza kuwa habari hizo si za kweli na ni potofu zenye lengo la kuleta taharuki katika jamii.
“Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu inapenda kuujulisha umma kwamba hakuna mabadiliko yaliyofanyika kwa tarehe tajwa kuhusiana na uwasilishwaji wa maombi ya vibali vya kazi, rufaa na msamaha,” anaeleza taarifa hiyo.
Zinazohusiana:
- Tahadhari: Mashine za kukaushia mikono haziui virusi vya Corona
- MSD yasambaza vitakasa mikono lita 350,000 mahitaji yakizidi kuongezeka Tanzania
Imesema maombi hayo yanaendelea kuwasilishwa na kushughulikiwa kwa utaratibu wa kawaida ulizoeleka wa kujaza fomu mtandaoni na kuziwasilisha kwa njia ya barua au kuzifikisha ofisini.
“Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu inawataka watu wanaoeneza taarifa hizo za uongo kuacha upotoshaji huo mara moja. Hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao endapo watakaidi maelekezo haya,” imesisitiza taarifa hiyo.
Latest