Hapana: Serikali haiwarudishi kazini watumishi waliosimamishwa kazi kwa kukosa vyeti
- Tamisemi yawataka wananchi kupuuzia taarifa hiyo.
- Kitakachorejeshwa ni sehemu ya michango yao waliochangia kwenye hifadhi za jamii pekee.
- Makosa ya kisarufi kwenye barua hiyo yanathibitisha kuwa taarifa hiyo ni ya uzushi.
Dar es Salaam. Ofisi ya Rais Tawala za mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imewataka wananchi kupuuzia taarifa inayoenea mtandaoni inayohusu kuwarudisha kazini watumishi waliosimamishwa kazi kwa kughushi vyeti mwaka 2017 na 2019.
Taarifa hiyo ya uzushi inayosambazwa kupitia barua inayofanana na barua rasmi zinazotolewa na Tamisemi inaeleza kuwa watumishi hao waliosimamishwa kazi miaka mitano iliyopita watalipwa na kurudishwa kazini jambo ambalo si kweli

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu,Profesa Joyce Ndalichako, imeeleza kuwa watumishi walioondolewa kazini kwa kugushi vyeti watarudishiwa michango yao na sio kurudishwa kazini kama taarifa hiyo inavyosema.
“Kinachorejeshwa ni asilimia tano kwa watumishi ambao michango yao ilikatwa kwenye mshahara yao kwenda PSSSF na asilimia 10 kwa watumishi waliokuwa wanakatwa kupitia NSSF… wala si malipo mengine yoyote ya ziada,” amesema Prof Ndalichako Oktoba 26, 2022.
Utekelezaji wa agizo hilo ulianza Novemba 9, 2022 na kufanyika ndani ya siku tisa, hivyo taarifa inayosambaa ya zoezi hilo kuanza Disemba 12, 2022 siyo ya kweli.
Soma zaidi
-
Hapana: Marekani haibadilishi noti za fedha zake
-
Serikali ya Uganda haijatangaza fidia kwa majeruhi wa ajali iliyosababishwa na msafara wa Rais
Tulichobaini
Huenda taarifa hiyo ya uzushi ikawa imetengenezwa na watu wenye nia ya upotoshaji au kuwatapeli watumishi hao waliondolewa kazini miaka mitano iliyopita.
Aina ya mwandiko iliyotumika kwenye barua hiyo haifanani kabisa na mwandiko halisi unaotumika kwenye barua rasmi za Tamisemi.
Makosa ya kisarufi yaliyopo kwenye barua hiyo ni ushahidi tosha kuwa huenda barua hiyo imeandikwa na mtu mwenye taaluma ndogo au asiyefahamu itifaki za mawasiliano.
Latest