Uzushi: Rais Samia hajasema kuvaa barakoa ni lazima

June 23, 2021 8:55 am · TULINAGWE ALSON
Share
Tweet
Copy Link
  • Rais Samia amezushiwa kuwa ameagiza kuwa uvaaji barakoa siyo hiari bali ni lazima.
  • Wananchi watakiwa kuipuza habari hiyo ya uzushi.
  • Watakiwa kuendelea kuchukua tahadhari na kupata taarifa za Corona katika vyanzo vya uhakika. 

Dar es Salaam. Habari za uzushi kuhusu Corona zinaendelea kusambaa kwa kasi duniani, na sasa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amezushiwa kuwa ameagiza uvaaji wa barakoa ni wa lazima na siyo suala ya hiari ili kujikinga na janga hilo. 

Hata hivyo, Rais Samia hajatoa maagizo kama hayo na habari zinazosambaa mtandaoni kuhusu suala hilo hazina ukweli wowote, ni uzushi.

Katika mitandao ya kijamii hasa WhatsApp, linasambazwa tangazo linalodaiwa limetolewa na Idara ya Elimu ya Afya ya Wizara ya Afya ya Tanzania kuwa Rais Samia amesema kuvaa barakoa ni lazima na siyo hiari. 

Moja ya maandishi yaliyopo katika habari picha hiyo yamasema  “Kuanzia sasa, unapoingia kwenye msongamano ni lazima uvae barakoa. Hii sio hiari tena, ni lazima. Nikinge nikukinge.”

                 

Ukweli ni huu

Ni kweli, Rais Samia tangu aingie madarakani Machi 2021 amekua akihimiza Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya COVID-19 ikiwemo kuvaa barakoa hasa kwenye mikusanyiko ya watu. 

“Na mkusanyiko huu iliopo hapa ni mkubwa. Kwa hiyo ili tuwakinge wazee wetu tumeamua leo tuvae barakoa kwa sababu mkusanyiko huu ni mkubwa na tumeshindwa kuwaweka mbalimbali mmekaa pamoja,” alisema Rais Samia wakati akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam Mei 7 mwaka huu.

Licha ya kiongozi huyo mkuu wa nchi kuhimiza uvaaji wa barakoa, pia katika ziara na matukio ya kiserikali ameonekana akiwa amevaa barakoa pamoja na watendaji wake.  

Ni lazima kuvaa barakoa?

Katika kuhimiza kuvaa barakoa, Samia ambaye ni rais wa sita wa Tanzania hajawahi kusema uvaaji wa barakoa ni lazima na siyo hiari kwa watu wote hasa wanapokuwa katika mikusanyiko ya watu wengi. 

Kuthibitisha suala hilo, timu ya #NuktaFakti kwa kutumia zana za kidijitali ikiwemo ya Google Image haijafanikiwa kupata ujumbe wowote mtandaoni wenye habari picha ambayo Rais amesema uvaaji wa barakoa ni lazima.

Hivyo, habari hiyo inayotembea mtandaoni siyo ya kweli bali imetengenezwa na watu wenye nia mbaya ya kuletea taharuki na kuwagombanisha viongozi wa Serikali na wananchi. 

Ni muhimu kufahamu kuwa uvaaji wa barakoa ni njia mojawapo ya kujikinga COVID-19. 

Na njia mojawapo ya kuhakikisha habari hiyo haiendelei kuleta madhara kwa watu ni kutokuisambaza na bali kupata taarifa katika vyanzo sahihi ikiwemo Wizara ya Afya ya Tanzania na Shirika la Afya Duniani (WHO).

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW