Serikali yasema haiakiki taarifa za waliondolewa kazini kwa kughushi vyeti
- Ni baada ya wazushi kudai imeendaa utaratibu wa kuhakiki taarifa zao.
Dar es Salaam. Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imesema haijatangaza kuwarudisha kazini watumishi wa umma waliondolewa katika majukumu yao katika ya 2016 na 2021 kinyume na utaratibu.
Tamko la wizara hiyo limekuja baada ya kuwepo kwa barua inayosambazwa mtandaoni inayodaiwa kutoka katika kitengo cha mawasiliano cha wizara hiyo ikielezea utaratibu unaotakiwa kufuata kwa watumishi hao kurudi kazini.
Barua hiyo imeorodhesha namba za simu ambazo hazihusiani na wizara hiyo ikiwataka wazitumie kuhakikisha taarifa zao huku wakitakiwa kuwa na nakala ya barua ya ajira, kitambulisho cha Taifa na nakala ya hati ya mshahara ya mwisho kabla ya kusimamishwa kazi.
TAARIFA YA UONGO pic.twitter.com/nbE92PEDsp
— Ofisi ya Rais – Utumishi (@utumishitz) April 16, 2023
Hata hivyo, wizara hiyo imesema barua hiyo haina kweli wowote na haijatoa tamko lolote kuhusu suala hilo siku za hivi karibuni.
“Taarifa ya uongo,” imeeleza wizara hiyo katika mtandao wake wa Twitter dhidi ya barua hiyo.
Hiyo siyo mara ya kwanza kwa watu wenye nia mbaya kusambaza barua kama hiyo ili kuzua taharuki na kuwatapeli watu. Desemba 20, 2022 waliitumia Wizara ya Tamisemi kudai kuwa Serikali inawarudisha kazini wafanyakazi waliondolewa kazini kwa makosa ya kughushi vyeti.
Watumishi hao ni wale walioondolewa katika utumishi wa umma wakati wa zoezi la uhakiki wa vyeti lililoendeshwa katika kipindi cha kuanzia Oktoba 2016 hadi Aprili mwaka 2017.
Uhakiki huo uliowatoa katika mfumo wa utumishi wa umma watumishi wasiopungua 14,516 waliobainika kuwa na vyeti vya kughushi.