Mwanza kuwaondoa wanafunzi katika madarasa chakavu
Mwonekano wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi Mabatini B ambavyo vimechaa. Jiji la Mwanza imeanza mkakati wa kujenga vyumba vipya kwenye shule hizo ambapo tayari kiasi cha Sh80 milioni kimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vinne shuleni hapo. Picha |Mariam John.
- Ni baada ya madarasa yaliyopo kuchakaa na kuhatarisha usalama wa wanafunzi.
- Imeanza ukarabati huo katika shule ya msingi Mabatini B.
Mwanza. Halmashauri ya jiji la Mwanza imeanza mikakati ya kujenga vyumba vya madarasa katika shule za msingi kongwe ambazo vyumba vyake vimekuwa chakavu hali inayotishia usalama wa wanafunzi.
Tayari halmashauri hiyo imetenga kiasi cha Sh80 milioni kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vinne katika shule ya msingi Mabatini B na kati ya fedha hizo, Sh31 milioni zimeshaingizwa kwenye akaunti ya shule.
Akizungumza baada ya kutembelea shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 1,141, Meya wa Jiji la Mwanza, Sima Costantine amesema kabla ya kuamua kuanza kwa ujenzi huo kiasi hicho cha Sh31 milioni kiliwekwa kwa ajili ya ukarabati wa vyumba hivyo.
“Wakati zoezi la ukarabati likiendelea, ukuta wa moja ya chumba cha darasa ulianguka hivyo tukabaini kuwa madarasa yote katika shule hiyo ni mabovu kwa kuwa yamejengwa kipindi kirefu hivyo ili kutohatarisha maisha ya wanafunzi tumeamua kuanza ujenzi wa vyumba vipya vya madarasa na hii itakuwa mwendelezo kwa shule zote kongwe za msingi,” amesema Sima.
Amesema baada ya kukamilika kwa majengo 13 ya vyumba vya madarasa vya gorofa watawekeza nguvu kwenye vyumba vya madarasa ya shule ya msingi ili kuhakikisha madarasa yote chakavu yanaondolewa.
Awali, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Samson Lukas amesema vyumba vya madarasa katika shule hiyo vimekuwa vikibomoka na kundondoka katokana na ubovu.
Zinazohusiana:
- Mbinu zitakazowasaidia watahiniwa darasa la saba kufanya vizuri.
- Necta yafuta matokeo ya watahiniwa 909 darasa la saba
- Kanda ya ziwa yatikisa matokeo darasa la saba 2019
Shule hiyo ina vyumba vya madarasa nane na kati ya hivyo vinne ni vibovu hali inayohatarisha usalama wa wanafunzi wawapo darasani.
“Kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa wanafunzi wa darasa la kwanza na la pili wanasoma kwa shifti na ili kuondoa changamoto hiyo kuna hitajika vyumba vya madarasa 20,” amesema Mwalimu Lukas.
Diwani wa Kata ya Mabatini, Ntobi Ntobi amesema shule hiyo imekuwa ya muda mrefu na ujenzi wake ulikuwa wa kiwango cha chini.
“Nimesoma hapa nimeanza darasa la kwanza mwaka 1980 na wakati kulikuwa na madarasa yaliyojengwa kwa matofali ya udongo lakini pia hata yalipokuja kujengwa haya nayo hayakuwekewa lenta hivyo ni rahisi kubomoka,” amesema Ntobi.
Amesema karibia vyumba vyote vya madarasa katika shule hiyo ni chakavu na kuiomba Serikali kutenga fungu la kutosha kwa ajili ya kuyajenga upya na kwamba wananchi katika kata hiyo wapo tayari kushiriki kwenye ujenzi wa vyumba hivyo.
Latest
