Karibu robo ya wanafunzi hawajaripoti kidato cha kwanza Tanzania
- Hadi Februari 10, wanafunzi 915,919 kati ya milioni 1.07 walikuwa wameripoti shuleni.
- Serikali yawataka wazazi kuwapeleka shuleni watoto ambao hawajaripoti bado kabla haijachukua hatua.
Mwanza. Karibu robo ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza Tanzania bado hawajaripoti shuleni huku Serikali ikiwataka wazazi kuwapeleka mara moja kabla hatua zingine hazijachukuliwa.
Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza Februari 12, 2023, amesema wanafunzi milioni 1.07 walichaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka huu lakini hadi kufikia Februari 10 ni wanafunzi 915,919 walikuwa wameripoti shule.
Hiyo ni asilimia 85.34 ya wanafunzi wote waliochaguliwa au sawa na kusema wanafunzi nane kati ya 10.
“Kwenye kidato cha kwanza kulikuwa na shida kidogo wakati tunaanza walioriopoti walikuwa wachache lakini sasa angalau wanaendelea kuripoti, nitoe wito kwa wanafunzi ambao hawajaripoti kuhakikisha wanaenda kwa kuwa Serikali imeboresha miundombinu ya kujifunzia,” amesema Msigwa.
Amesema Serikali imejenga vyumba vya madarasa na kuweka madawati kwa shule zote za sekondari nchini, ingawa kuna changamoto ya upungufu wa walimu lakini inajitahidi kuhakikisha suala hilo linatafutiwa ufumbuzi.
Amesema wameweka mfumo wa kufuatilia wanafunzi wote waliofaulu na kupangiwa kwenye shule zao. Iwapo mwanafunzi hatakuwa ameonekana katika shule aliyopangiwa kwa muda wa siku 21 atahesabika kuwa ni mtoro au ameacha shule na mfumo utamuondoa.
Soma zaidi:
Amesema kwa wanafunzi wanaopelekwa shule za binafsi, serikali pia imetoa maelekezo kwa shule hizo kuhakikisha zinapeleka taarifa hizo kwenye mfumo ndani ya siku 90 iwapo hazitafanya hivyo mwanafunzi ataondolewa kwenye mfumo na kuhesabika kuwa ni mtoro.
“Hivyo tunawaomba wazazi wote kuhakikisha wanawapeleka watoto wao shule na wale waliowapeleka shule binafsi tupate taarifa zao ili ziweze kujumuishwa,” amesema Msigwa.
Tunaboresha elimu
Amesema kupitia fedha za mradi wa Uviko-19, jumla ya vyumba vya madarasa 15, 000 vilijengwa lakini pia serikali ilitoa zaidi ya Sh160 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 8,000.
Msigwa amesema mwaka huu Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 9,000 kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la awali na msingi.
“Tunataka watoto wanapoingia madarasa ya awali na msingi wasipate shida ya sehemu ya kujifunzia kwa kuwa Serikali inaendelea kutoa fedha ili kuboresha miundombinu ya kusomea,” amesema Msigwa.
Latest