Michezo, burudani vyachangia kupaisha mfumuko wa bei Tanzania
- Mfumuko wa bei umeongezeka hadi asilimia 3.5 mwaka ulioshia Januari 2021 kutoka 3.2 Desemba, 2020.
- Bidhaa za chakula zashuka bei huku huduma za burudani, michezo na utamaduni zikipanda.
- Huduma zingine zilizopanda bei ni pamoja na huduma za makazi, maji, umeme na gesi.
Dar es Salaam. Mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwaka ulioishia Januari 2021 umeongezeka kidogo hadi kufikia asilimia 3.5 kutoka asilimia 3.2 iliyorekodiwa mwaka ulioishia Desemba mwaka jana ukichagizwa zaidi na kupaa kwa bei za baadhi ya bidhaa na huduma za usafiri na afya.
Taarifa ya mfumuko wa bei iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Februari 8, 2021 inaeleza bei za huduma za burudani, michezo na utamaduni zimeongezeka kwa asilimia 3.2 huku gharama za samani za nyumbani na ukarabati zikiongezeka kwa asilimia 2.2 zikiwa sawa sawa na bidhaa za usafi binafsi na wa kijamii.
Soma zaidi:
- Kushuka kwa bei ya mahindi kulivyowapunguzia maumivu walaji mwaka 2020
- Hivi ndivyo unavyoweza kupata simu mpya kwa bei rahisi
- Vilio, vicheko bei ya mahindi ikipaa Tanzania
Bidhaa nyingine na huduma zilizopanda katika kipindi hicho ni huduma za makazi, maji, umeme, gesi na mafuta mengine kwa asilimia 1.1 na huduma za usafiri kwa asilimia 1.5.
NBS imeeleza kuwa bidhaa nyingine zilizopanda bei ni mavazi na viatu ambavyo vimepanda kwa asilimia 1.9 huku pombe na bidhaa za tumbaku zikipanda kwa asilimia 0.6
Hata hivyo, kasi ya mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji baridi ulishuka kidogo katika katika kipindi hicho.
“Mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji baridi umeshuka kutoka asilimia 3 mwezi Desemba, 2020 hadi asilimia 2.8 mwezi Januari 2021,” inasomeka sehemu ya taarifa iliyotolewa na NBS.

Latest