Mfumuko wa bei wapaa baada ya kudumaa kwa miezi miwili
- Umepanda hadi asilimia 4 mwaka ulioishia Septemba 2021 kutoka asilimia 3.8 mwaka unaoishia Agosti mwaka huu.
- Kumechangiwa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na zisizo za vyakula.
Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia Septemba 2021 imepanda hadi asilimia 4 baada ya kubaki katika kiwango kimoja kwa miezi miwili mfululizo.
Mfumuko wa bei wa Taifa hupima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na zinazotumiwa na kaya binafsi nchini.
Mfumuko wa bei umeongezeka kutoka asilimia 3.8 iliyorekodiwa katika mwaka unaoishia Julai na Agosti mwaka huu hadi asilimia 4 mwaka unaoishia Septemba.
Kuongezeka kwa mfumuko huo kumechangiwa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na zisizo za vyakula.
Kaimu Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu, Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Ruth Minja, amesema baadhi ya bidhaa za vyakula zilichangia kuongezeka kwa mfumuko wa bei ni pamoja na unga wa ngano kwa asilimia 6.8, Nyama ya Ng’ombe (asilimia 3.4), maziwa ya unga kwa (asilimia 9.2), mayai kwa (asilimia 5) na viazi mviringo kwa asilimia 4.7
Baadhi ya bidhaa zisizo za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa mfumuko wa bei ni gesi ya kupikia kwa asilimia 5.7, mkaa (asilimia 3.5) na Huduma ya malazi kwenye nyumba za kulala wageni kwa asilimia 5.7
“Mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia Septemba, 2021 umeongezeka hadi kufikia asilimia 4.0 kutoka asilimia 3.6 kwa mwaka ulioishia Agosti 2021,” amesema Minja.
Mfumuko wa bei ambao haujumuishi bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa Septemba 2021 umeongezeka pia hadi kufikia asilimia 4.1 kutoka asilimia 4 ilivyokuwa kwa mwaka ulioishia mwezi Agosti 2021.
Latest
