Ugonjwa wa kipindupindu, kuharisha ulivyowatesa Watanzania mwaka 2025
- Ugonjwa wa kuharisha ulikuwa ni ugonjwa ama hali iliyoripotiwa zaidi mwaka 2025 katika mikoa yote ya Tanzania
Dar es Salaam. Huenda Watanzania wakatakiwa kuchukua tahadhari za kiafya zaidi ili kujikinga na magonjwa ya kipindupindu na kuharisha ambayo takwimu za hivi karibuni za Wizara ya Afya zinayataja kuwasumbua zaidi wananchi mwaka 2025.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kuharisha ni hali ya kiafya inayohusisha kujisaidia choo chepesi zaidi kuliko kiwango cha kawaida kwa zaidi ya mara tatu kwa siku, hali ambayo huchangiwa zaidi na maambukizi ya bakteria na virusi vinavyoathiri mfumo wa mmeng’enyo wa chakula.
Wakati mwingine kuharisha, hutajwa kuwa miongoni mwa dalili za ugonjwa wa kipindupindu unaosababishwa na bakteria aitwaye Vibrio cholerae, ambao kwa miaka ya nyuma ulitajwa kuchangia idadi kubwa ya vifo.
Takwimu za Mfumo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Udhibiti wa Magonjwa (IDSR), zilizotolewa Februari 2, 2026 na Wizara ya Afya zinabainisha kuwa karibu nusu ya visa vyote 369,864 vya magonjwa yanayoripotiwa nchini vinatokana na ugonjwa wa kuharisha.
Visa 176,797 vilihusishwa na magonjwa ya kuharisha, sawa na asilimia 47.8 ya visa vyote vilivyoripotiwa katika robo ya kwanza na ya pili ya mwaka 2025.

Kila mtu hupata kuhara mara kwa mara, lakini inapodumu zaidi ya wiki nne, huchukuliwa kuwa kuhara sugu. Picha/ Gastro florida.
Takwimu hizo zinaonesha kuwa karibu mgonjwa mmoja kati ya wawili waliokwenda katika vituo vya afya alikuwa anakabiliwa na tatizo la kuharisha kutoka mikoa yote 26 ya Tanzania Bara.
Miongoni mwa mikoa iliyoongoza kwa visa vingi vya kuharisha ni Dodoma yenye visa 13,770 (asilimia 7.8), ikifuatiwa na Mara visa 13,622 (asilimia 7.7), Morogoro visa 11,879 (asilimia 6.7) na Rukwa visa 11,494 (asilimia 6.5).

Mwezi wa Mei uliongoza kwa idadi kubwa ya visa, ambapo viliripotiwa visa 78,496 sawa na asilimia 21.2 ya visa vyote ikichangia vifo 33.
Mbali na Kuharisha kipindupindu pia kiliwatesa Watanzania mwaka 2025, visa 3,433 na vifo 26, sawa na asilimia 78.8 ya vifo vyote vikiripotiwa.
Nimonia, ‘typhoid’ pasua kichwa
Ripoti ya Wizara ya Afya inayataja magonjwa mengine yaliwasumbua Watanza ndani ya mwaka 2025 kuwa ni ugonjwa wa nimonia ambapo visa 133,310 vilirekodiwa ikifuatiwa na homa ya matumbo (typhoid) uliokuwa na visa 31,760.

Pneumonia ni maambukizi ya papo hapo ya njia ya hewa yanayohusisha alveoli na njia za hewa za mbali. Picha/ Dr J Suri.
Pia, kulikuwa na visa 12,062 vya kung’atwa na wanyama na visa 6,183 vya kung’atwa na nyoka, maambukizi makali ya njia ya hewa (SARI) yalishika nafasi ya sita kwa visa 4,213 pamoja na vifo saba vilivyoripotiwa.
Homa ya dengue pia yenye visa 84 na kichaa cha mbwa (rabies) kilichokuwa na visa 25 kiliingia katika orodha hiyo ya magonjwa 10 yaliyowatesa Watanzania suala linaloacha mzigo mkubwa wa udhaifu wa mwili kwa wananchi.
WHO yatoa mwongozo mpya wa lishe mashuleni kudhibiti unene uliopitiliza
- Takribani watoto na vijana milioni 188 wa umri wa kwenda shule waliishi na unene uliopitiliza 2025.
- Ni nchi 48 pekee kati ya 408 zilizo na sera zinazozuia matangazo ya vyakula visivyofaa kwa watoto.
Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO) limetoa mwongozo mpya wa kimataifa wa lishe mashuleni, unaoziitaka nchi wanachama kuimarisha mazingira ya lishe shuleni ili kudhibiti ongezeko la unene uliopitiliza na kukabiliana na changamoto ya utapiamlo kwa watoto.
Uzito au unene uliopitiliza hufafanuliwa kama mkusanyiko usio wa kawaida au wa kupita kiasi wa mafuta mwilini ambao unaweza kuweka afya hatarini ikichangiwa zaidi na mtindo mbovu wa maisha, ulaji usiozingatia kanuni za afya na tabia bwete.
Takwimu za WHO zinakadiria kuwa mwaka 2024 takribani watoto milioni 35 walio chini ya umri wa miaka mitano duniani kote walikuwa na uzito uliopitiliza suala linaloweka afya zao rehani.
Hali ni mbaya zaidi kwa watoto na vijana milioni 188 wenye umri wa kwenda shule ambao waliripotiwa na WHO kuwa na unene uliopitiliza, sawa na mtoto mmoja kati ya 10, idadi iliyozidi kwa mara ya kwanza watoto wenye uzito pungufu.

Kutokana na uwepo wa changamoto hiyo, January 27, 2026, WHO ilitoa mwongozo wa lishe mashuleni utakaohakikisha vyakula na vinywaji vinavyotolewa shuleni, pamoja na vinavyopatikana katika mazingira yanayozunguka shule, ni vyenye afya na lishe bora.
“Uzito kupita kiasi na unene uliokithiri kwa watoto vinaendelea kuongezeka duniani, huku utapiamlo bado ukiwa changamoto ya kudumu. Shule ziko mstari wa mbele katika kukabiliana na mzigo huu maradufu wa utapiamlo,” inaeleza sehemu ya taarifa ya WHO.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dk Tedros Adhanom Ghebreyesus aliyekuwa akizunngumza alisema kuwa lishe shuleni ina athari ya moja kwa moja katika afya na maendeleo ya watoto.
“Chakula ambacho watoto hula shuleni kinaweza kuathiri uwezo wao wa kujifunza na kuwa na madhara ya muda mrefu kwa afya na ustawi wao. Lishe sahihi shuleni ni msingi wa kuzuia magonjwa baadaye maishani,” alisema.

Katika muktadha wa kitaifa, baadhi ya nchi ikiwemo Tanzania, tayari zina miongozo ya chakula cha shule inayolenga kuboresha lishe kwa wanafunzi kupitia Mpango wa Taifa wa Chakula Shuleni (NSFG).
Mpango huo unazingatia Sera ya Afya ya mwaka 2007, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na Mpango wa Taifa wa Sekta Jumuishi wa Miaka Mitano wa Utekelezaji wa Lishe 2016/17 hadi 2020/2.
Kwa mujibu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, utoaji wa huduma za chakula shuleni huchangia kuboresha afya ya wanafunzi, kupunguza utoro, kuongeza usikivu darasani na kuinua kiwango cha ufaulu.
WHO inakadiria kuwa zaidi ya watoto milioni 466 duniani hupata chakula kupitia programu za chakula shuleni jambo linaloimarisha afya ya akili na kuimarisha uwezo wao wa kimasomo.

Hata hivyo, shirika hilo linaonya kuwa bado kuna upungufu wa taarifa kuhusu ubora wa lishe ya chakula hicho, hali inayoweza kusababisha changamoto za kiafya.
Katika mwongozo wake mpya, WHO inapendekeza shule ziweke kanuni za lazima zitakazohamasisha upatikanaji wa vyakula vyenye afya na kupunguza matumizi ya vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi na mafuta yasiyo na afya, pamoja na kudhibiti mbinu za kibiashara zinazowalenga watoto.
Kwa sasa, nchi 104 zina sera za chakula chenye afya mashuleni huku karibu robo tatu zikiwa na vigezo vya lazima vya kuongoza muundo wa chakula cha shule huku nchi 48 pekee zikizuia matangazo ya vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi au mafuta yasiyo na afya.
Fahamu mahitaji ya usingizi kwa watoto wachanga
- Usingizi ni muhimu sana kwa ukuaji wa mwili na akili ya mtoto.

Dar es Salaam. Usingizi ni miongoni mwa mahitaji muhimu kwa binadamu, hususan watoto wachanga katika miaka miwili ya mwanzo ya maisha yao.
Tofauti na watu wazima, watoto huhitaji muda mwingi zaidi wa kulala ili kuwawezesha kukua vizuri na kuimarisha uwezo wa ubongo kufanya kazi kwa ufanisi.
Kwa mujibu wa tovuti ya masuala ya afya ya Stanford Medicine Children’s Health, watoto wachanga huhitaji hadi saa 17 za usingizi kwa siku, ambazo hugawanyika katika vipindi mbalimbali.
“Ratiba ya usingizi wa mtoto ni muhimu sana kwa ukuaji wake wa mwili, maendeleo ya akili (kumbukumbu, kujifunza na umakini), udhibiti wa hisia, pamoja na ujuzi wa mwendo wa mwili,” inaeleza tovuti hiyo.
Tovuti hiyo inabainisha kuwa watoto wenye umri wa kuanzia siku moja hadi miezi mitatu ya mwanzo wanahitaji kulala wastani wa saa 16 hadi 17 kwa siku, lakini mara nyingi hawalali zaidi ya saa 1 hadi 2 kwa wakati mmoja.
Aidha, watoto wenye umri wa miezi minne hadi 12 wanahitaji kulala wastani wa saa 12 hadi 16 kwa siku, huku wale wenye umri wa mwaka mmoja hadi miaka miwili wakihitaji kulala kati ya saa 11 hadi 14 kwa siku.
Nchi 10 Afrika zilizopokea msaada mkubwa sekta ya afya kutoka USAID 2023

Kwa miaka mingi, Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) limekuwa msaada wa huduma za afya barani Afrika, likifadhili mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko, na kuboresha mifumo ya afya.
Kwa mujibu wa Shirika la Misaada la Serikali la Marekani (Foreign Assistant Government) nchi 10 zilizonufaika zaidi kwa mwaka 2023 ni Kenya, Nigeria, Tanzania, Uganda, Ethiopia, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Malawi, na DRC, ambapo misaada hii imewezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, lishe bora, na huduma za afya ya uzazi.
Tanzania ni nchi iliyoongoza kwa kupokea msaada mkubwa katika sekta ya afya kutoka USAID ikipokea takriban Dola milioni 512.8 za Marekani, sawa na Sh1.32 trilioni.
Hata hivyo, kusitishwa kwa misaada hii kunaweza kuwa na athari kubwa katika nchi hizi kwa kukabiliwa na uhaba wa dawa za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI), lishe, kifua kikuu, magonjwa ya mlipuko na vitisho vipya vya kiafya, vifaa vya afya, uzazi wa mpango na afya ya uzazi, usafi wa maji, pamoja na miradi mingine ya afya.
Bila ufadhili wa USAID, nchi hizi zinapaswa kutafuta vyanzo mbadala vya rasilimali ili kuzuia madhara kwa mamilioni ya watu wanaotegemea huduma hizi. Lakini je, mataifa haya yana uwezo wa kuziba pengo hili haraka? Ikiwa suluhisho halitapatikana, mustakabali wa afya barani Afrika unaweza kuwa hatarini.
Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania

Dar es Salaam. Miongoni mwa masuala yanayogusa zaidi vijana wengi waliopo kwenye ndoa na wasio kwenye ndoa kwa sasa ni suala la kuwa na watoto.
Miongoni mwa maswali makubwa huwa ni lini wapate watoto, idadi ya watoto lakini ni njia gani sahihi itakayomfanya wanawake vijana wasipate ujauzito bila kutarajia. Wataalamu wanasisitiza kuwa ni vema wazazi vijana wakapanga mipango yao vema ya kijamii na kiuchumi kabla ya kupata watoto.
Hata hivyo, si watu wote wanapanga ipasavyo juu ya kupata watoto. Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa mwaka 2022 unabainisha kuwa nchini Tanzania takriban wanawake wanne kati ya 10 au asilimia 38 ya waliolewa wenye umri wa miaka 15 hadi 49 wanatumia njia ya aina yeyote ya uzazi wa mpango.
Ripoti ya utafiti huo uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa ushirikiano na taasisi nyingine iwepo Wizara ya Afya inabainisha ipo baadhi ya mikoa yenye kiwango kikubwa cha wanawake wenye wanaotumia ipasavyo njia za uzazi wa mpango ikiongozwa na Njombe huku mingine ikitumia kwa kiwango kidogo sana kama Simiyu.
Je, waifahamu mikoa inayoongoza kwa matumizi ya njia za uzazi wa mpango Tanzania?
Ulaji milo mitatu ya chakula bado kitendawili Tanzania
- Idadi ya wanaokula milo mitatu yashuka kwa asilimia 8.2.
- Mtanzania mmoja kati ya 10, anakula mlo mmoja wa chakula.
- Uviko -19, uhaba wa chakula baadhi ya maeneo vyatajwa kama sababu.
Dar es Salaam. Wakati wataalamu wa afya wakihimiza kula milo mitatu ya chakula kwa siku au zaidi ili kuwa na afya bora, hali ni tofauti nchini Tanzania kwani idadi ya watu wanaokula milo mitatu kwa siku imeshuka kwa asilimia 8.2.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Kufuatilia Hali ya Kaya Tanzania (NPS) ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), idadi ya Watanzania wanaokula milo mitatu imeshuka kutoka asilimia 71.2 mwaka 2014/15 mpaka asilimia 63 mwaka 2020/21.
Hii ni kumaanisha kuwa kati ya Watanzania kumi ni sita ndio wanaokula milo mitatu ya chakula au zaidi kwa siku.
Wakati idadi ya wanaokula milo mitatu au zaidi ikishuka, idadi ya wanaokula milo miwili hadi mmoja imeongezeka. Mathalani wanaokula mlo mmoja wameongezeka kutoka asilimia 0.6 mpaka 1.6 huku wanaokula milo miwili wakiongezeka kutoka 28.2 mpaka 35.4.
Uchambuzi wa takwimu uliofanywa na Nukta habari umebaini kuwa kwa mujjbu wa ripoti hiyo katika kila Watanzania kumi basi mmoja hula mlo mmoja tu wa chakula huku watatu kati ya 10 wakila milo miwili ya chakula.
Hata hivyo, hali ya ulaji wa chakula imeonekana mbaya zaidi katika maeneo ya vijijini kuliko mjini kwani, Watanzania waishio mjini wana wastani mzuri zaidi wa kula milo mitatu kwa asilimia 74.8 huku vijijini wakiwa na asilimia 57.3.
Vivyo hivyo, idadi ya wanaokula mlo mmoja vijijini ni kubwa zaidi ambao ni asilimia 1.8 wakati mjini ni 1.2 huku asilimia ya wanaokula milo miwili vijijini ikiwa ni mara mbili zaidi ya wale waishio mjini.
Huenda hali hiyo imechangiwa na kuwepo kwa upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo hapa nchini hali iliyosababishwa na mtawanyiko wa mvua pamoja na visumbufu.
Soma zaidi
- Vyakula vinavyoimarisha kumbukumbu, uelewa wa kimasomo kwa watoto
- Mwaka 2022 umekuwa mgumu familia kuweka mlo mezani: UNCTAD
Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Chakula nchini ya mwaka 2020/21 imeeleeza kuwa pamoja na kuwa na ziada ya chakula halmashauri 17 kutoka mikoa nane nchini ilitarajiwa kukutana na uhaba wa chakula mwaka juzi.
“Upungufu huo umechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo mtawanyiko mbaya wa mvua, visumbufu vya mimea kama vile wanyamapori, ndege aina ya kwelea kwelea na viwavijeshi vamizi, ” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.
Aidha uwepo wa ugonjwa wa Uviko-19 uliathiri shughuli za kilimo kwani ulisababisha changamoto katika upatikanaji wa pembejeo muhimu za kilimo kama vile mbegu, mbolea, viuatilifu na zana za kilimo.
Janga hilo lilichangia watu kupoteza ajira na biashara, na hivyo kukosa kipato kwa ajili ya kukidhi ya mahitaji ya kila siku ya chakula.
Tangazo:




