Bunge lapitisha Bajeti Kuu ya Serikali 2023-24

June 26, 2023 3:11 pm · admin
Share
Tweet
Copy Link
  • Wabunge 354 wapiga kura za ndio 20 wasita kutoa maamuzi.
  • Bajeti kuleta ahueni, maumivu kwa Watanzania.

Dar es Salaam. Bunge la Tanzania limepitisha bajeti ya Sh44.39 trilioni iliyopangwa kutumika na Serikali kwa mwaka 2023/24 huku zaidi ya theluthi mbili ya bajeti hiyo zikipangwa kutumika kwenye matumizi ya kawaida.

Hata hivyo, bajeti hiyo inaweza kusababisha maumivu kwa watumiaji wa vyombo vya moto baada ya mapendekezo ya ongezeko la Sh100 katika kila lita ya mafuta pamoja na ushuru wa bidhaa kwa asilimia 10 katika magari yanayozidi umri wa miaka mitano yanayoingizwa nchini kupita.

Jumla ya wabunge 354 sawa na asilimia 95  wamepiga kura za ndio huku wabunge 20 akiwemo Halima Mdee na Conchester Rwamlaza wakipiga kura za kutotoa maamuzi yaani kwa kimombo ‘abstain’.

Spika wa Bunge la Tanzania Dk Tulia Ackson aliyekuwa akitangaza matokeo ya kura leo Juni 26, 2023 amebainisha kuwa bajeti ya Serikali imepitishwa rasmi mara baada ya wabunge 354 walioshiriki zoezi hilo kupiga kura za ndio.

“Nitangaze rasmi kwamba bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/24 imepitishwa rasmi na bunge,” amesema Dk Tulia.


Soma zaidi


Mchakato wa kuidhinisha bajeti hiyo ulianza mapema asubuhi ya leo Juni 26, 2023 mara baada ya kipindi cha maswali na majibu ambapo Spika wa Bunge Dk Tulia Ackson alimkaribisha Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba kutolea ufafanuzi wa hoja za wabunge zilizoibuliwa kuhusiana na bajeti.

Mara baada ya Mwigulu kumaliza ufafanuzi wa hoja zake ambapo alijikita katika kuhamasisha wabunge kuipitisha bajeti hiyo, makatibu wa Bunge walianza kuwahoji wabunge ambao walitakiwa kujibu ndio au hapana.

Baadhi ya mambo yanayotarajiwa kuleta ahueni kutoka kwenye bajeti ya iliyoidhinishwa ni pamoja na mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya kati watakaosoma kada za kipaumbele pamoja na Serikali kuwalipia ada wahitimu wa kidato cha nne watakao chaguliwa kujiunga na vyuo vya DIT, ATC, pamoja na MUST.

Enable Notifications OK No thanks