Bunge lapitisha bajeti ya Serikali 2026/27 kwa asilimia 97.66
- Ni baada ya wabunge 385 kati ya 393 waliokuwepo bungeni kupiga kura ya ndiyo.
Dar es Salaam. Bunge la Tanzania limepitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndiyo kuunga mkono bajeti hiyo licha ya kuwepo mapendekezo kwa baadhi ya wadau ikiwemo Serikali kupunguza matumizi yasio ya lazima
Akitangaza matokeo ya kura ya wazi iliyopigwa bungeni, leo Juni 23, 2026 Spika wa Bunge la Tanzania Mussa Zungu amesema jumla ya kura zilizopigwa ni 393, ambapo wabunge nane wamepiga kura za hapana.
“Kura za ndio 385, kura za hapana nane, kura za sipigi kura sifuri, bajeti ya Serikali imepitishwa kwa kura 385 sawa na asilimia 97.66,” ameeleza Spika Zungu huku akitaka bajeti kutumika kwa maslahi ya wananchi na siyo vinginevyo.
Bajeti hiyo ya Sh 62.3 trilioni iliyopitishwa leo iliwasilishwa bungeni Juni 11, 2026 na Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Omar na kisha kujadiliwa kwa takriban wiki mbili na wabunge hao wa Bunge la Tanzania kabla ya kuipitishwa.
Kiwango hicho cha bajeti ni sawa na ongezeko la asilimia 10.3 kutoka Sh56.49 trilioni iliyoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya mwaka wa fedha 2025/26 unaohitimishwa Juni mwaka huu.
Fedha hiyo iliyoombwa inatarajiwa kukamilisha maeneo matano ya vipaumbele ikiwemo kuimarisha uwezo wa watu na maendeleo ya jamii na kuimarisha uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu kwa mabadiliko ya tabianchi.
Vile vile, kusimamia utekelezaji wa vichocheo vya mageuzi pamoja na kuimarisha utawala bora, demokrasia, amani, na utulivu.
Mbali na kupitishwa kwa bajeti hiyo, Bunge pia limeidhinisha mswada wa Sheria ya Fedha mwaka 2026 na Sheria ya kuidhinisha matumizi ya Serikali kwa mwaka 2026.
Sheria hiyo inairuhusu Serikali kukusanya na kutumia kiasi cha Sh62.3 trilioni kwa matumizi ya Serikali kutoka katika mfuko mkuu wa hazina kwa mwaka unaoishia Juni 30, 2027.
Kupitishwa kwa bajeti hiyo kunamaanisha kuwa baadhi ya marekebisho ya sheria yataanza kutekelezwa kuanzia Julai 2026.