Bunge laahirishwa baada ya waziri na naibu wake kutoonekana
- Ni Waziri wa Nishati, January Makamba na naibu wake, Stephen Byabato.
Dar es Salaam. Bunge limeahirisha shughuli zake kwa muda wa dakika 30 kwa sababu Waziri wa Nishati, January Makamba na naibu wake, Stephen Byabato hawakuwepo katika ukumbi wa Bunge kabla ya mjadala wa hotuba ya wizara hiyo kuanza.
Uamuzi huo umefikiwa leo asubuhi Juni 2, 2022 na Mwenyekiti wa Bunge, David Kihenzile wakati mjadala wa hotuba ya bajeti ya wizara hiyo ulipoanza kwa Mbunge wa Viti Maalum Catherine Magige kutoa mchango wake.
Kihenzile alimkatisha Mbunge Magige kuendelea kutoa mchango wake kwa sababu mawaziri wa wizara hiyo hawapo bungeni na wanahusika kupokea maoni ya Wabunge kabla hawajafanya majumuisho ya bajeti yao leo.
“Mheshimiwa Catherine Magige hebu keti kwanza, waheshimiwa Wabunge tunaahirisha shughuli za Bunge kwa nusu saa mpaka Mheshimiwa naibu waziri na waziri watakuwa wamefika Bungeni,” amesema.
Muda mfupi wakati Wabunge wakitoka nje ya ukumbi wa Bunge, Waziri Makamba aliingia na kuketi kwenye kiti chake. Hata hivyo, Wabunge walilazimika kusubiri muda wa nusu saa uliotangazwa kisha wakarejea bungeni kuendelea na mjadala.
Waziri Makamba jana aliwasilisha bungeni bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 ambayo imepanga kutumia Sh2.9 trilioni ambapo moja ya vipaumbele ni kuimarisha mfumo wa uagizaji na uingizaji wa mafuta nchini.
Mjadala wa bajeti ya wizara hiyo huo mkali miongoni mwa Wabunge kwa sababu unagusa eneo muhimu la umeme na mafuta, nishati muhimu kwa ajili shughuli mbalimbali za maendeleo.
Hata hivyo, Waziri Makamba katika hotuba yake jana alisema Serikali imeandaa mpango kabambe unakaosaidia kumaliza tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara na uhaba wa petroli na dizeli nchini.
Latest