Bunge la Tanzania lapunguza matumizi ya karatasi, lageukia mitandao ya kijamii

September 3, 2019 12:06 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link

Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema hatua hiyo itasaidia katika kuachana kabisa na matumizi ya karatasi na kutumia mifumo ya kielektroniki kuwasiliana. Picha|Mtandao.


  •  Limesema kuanzia kesho Wabunge watapatiwa taarifa za orodha ya shughuli za Bunge kwa kutumia simu, mitandao ya kijamii na barua pepe.
  • Lengo ni kupunguza matumizi ya karatasi na kuongeza usafi katika dawati la Mbunge awapo bungeni. 

Dar es Salaam. Bunge la Tanzania limeanza kuchukua hatua mbalimbali za kupunguza matumizi ya karatasi katika shughuli zake ikiwemo kutumia mitandao ya kijamii na barua pepe kuwapatia Wabunge orodha ya shughuli za vikao vya Bunge kwa siku husika. 

Katika Bunge la Tanzania, kila Mbunge amekuwa akipatiwa karatasi ya pinki (order paper) yenye orodha ya shughuli zinazofanyika bungeni kwa siku husika. 

Spika wa Bunge, Job Ndugai aliyekuwa akizungumza leo (Septemba 3, 2019) wakati akiwa bungeni, amesema leo ndiyo itakuwa mwisho kutumia karatasi ya orodha ya shughuli za muhimili huo, badala yake Wabunge watakuwa wanatumiwa taarifa katika simu zao na mitandao ya kijamii kama WhatsApp. 

“Niwatangazie Wabunge kwamba hizi karatasi za pinki za maswali, “order paper” kwa ujumla wake, orodha ya shughuli hii itakuwa karatasi ya mwisho kuingia bungeni leo. 

“Kuanzia kesho tutakutumia hii kwenye mawasiliano yako ya kimtandao, kwa hiyo naomba kila mmoja uthibitishe namba ya simu, ya WhatsApp, email address (barua pepe) hapa,” amesema Ndugai.


Soma zaidi:


Amesema Bunge la Tanzania ndiyo Bunge pekee Afrika Mashariki ambalo bado linaendekeza matumizi ya karatasi katika shughuli zake, jambo linalofanya dawati la Mbunge kuwa na karatasi nyingi ambazo wakati mwingine zinaleta usumbufu. 

“Sisi ndiyo bunge pekee Afrika Mashariki ambalo bado tunaendekeza masuala ya makaratasi mengi, wenzetu wote ni paperless (hawatumii makaratasi). Tutaanza na jambo moja hili peke yake ya  hii “order paper” halafu tutaona kidogo kidogo kadiri tunavyoenda dawati la Mheshimiwa Mbunge litakuwa safi,” amesema Spika Ndugai. 

Amesema hatua hiyo itasaidia katika kuachana kabisa na matumizi ya karatasi na kutumia mifumo ya kielektroniki kuwasiliana. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW