Google kulipa faini ya Sh390 bilioni kwa kuingilia faragha ya watoto Youtube
Google imepewa onyo na kutakiwa kuzingatia sheria na kanuni zinazosimamia maudhui ya mtandaoni. Picha|Mtandao.
- Inadaiwa kuwa Youtube ilifanya kosa la kuingilia jumbe zinazohusu watoto ambao ni moja ya wateja na wenye haki ya kuwa na faragha katika maudhui wanayoangalia.
- Pia ilitumia maudhui ya watoto kujipatia matangazo kutoka kampuni mbalimbali.
- Kwa sasa faini hiyo ndiyo faini ya kiwango cha juu kwa kampuni ya teknolojia kutozwa duniani.
Dar es Salaam. Tume ya Shirikisho la Biashara ya Marekani (FTC) ya imeitoza faini ya dola za Marekani milioni 170 sawa na Sh390 bilioni kampuni ya Google baada ya mtandao wake wa Youtube kukiuka sheria ya faragha kwa watoto (Child privacy).
FTC imesema Youtube walifanya kosa la kuingilia jumbe zinazohusu watoto ambao ni moja ya wateja na wenye haki ya kuwa na faragha katika maudhui wanayoangalia.
Katika taarifa ya FTC iliyowekwa kwenye tovuti yake inaeleza kuwa wamebaini kuwa Google iliuza jukwaa lake la video la YouTube, kwa watangazaji ikijua kuwa chaneli nyingi za mtandao zilikuwa zinatazamwa na watoto na hakupaswa kuona baadhi ya maudhui.
Pia inadaiwa kuwa kampuni hiyo ilifuatilia historia ya kutazama video ya watoto ili kuitumia kupata takwimu za matangazo, na kukiuka Sheria ya Ulinzi wa Usiri wa Siri za Watoto (COPPA).
Faini hiyo imegawanywa katika makundi mawili; dola milioni 136 zitalipwa katika tume ya FTC kiasi kilichobaki cha dola milioni 34 kitalipwa kwa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa New York ambayo ilihusika kuichunguza Youtube.
Zinazohusiana:
- Youtube yaleta mbinu mpya ya kudhibiti maudhui ya watoto mtandaoni
- Youtube yajipanga kuzuia matangazo ya biashara kwenye video za watoto.
Inaelezwa kuwa kwa sasa faini ya Dola za Marekani milioni 170, ndiyo faini ya kiwango cha juu kwa kampuni ya teknolojia kutozwa ukilinganishwa na ambayo kampuni ya TikTok ilitozwa Februari mwaka huu.
Faini hio ya bilioni 390 iliyotozwa Google mpaka sasa ndio faini ya juu kuliko zilizowahi kutolewa nyuma kwa baadhi ya kampuni zilizoenda kinyume na sheria za kimtandao au maudhui.
Google imepewa onyo na kutakiwa kuzingatia sheria na kanuni zinazosimamia maudhui ya mtandaoni.
Agosti, 2019 Mtandao wa YouTube uliweka wazi nia yake ya kuondoa matangazo ya biashara yanayomlenga mtumiaji wa simu ya mkononi anayeangalia video zote zenye maudhui ya watoto.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya kimataifa maamuzi hayo yalifikiwa na YouTube baada ya mashirika mbalimbali kulalamika juu ya mtandao huo kushindwa kuwalinda watoto hasa pale wanapokuwa wanatumia simu za wazazi wao.
Latest
