Kimbunga Jobo kutua Dar, mikoa mengine kuathirika
- Mikoa hiyo ni Mtwara, Lindi, Tanga, Mafia, Dar es Salaam, Pwani na Zanzibar.
- Kinatarajiwa kuleta athari za upepo mkali, mawimbi makubwa baharini na mvua kubwa.
- Wananchi watakiwa kuchukua tahadhari ikiwemo kusitisha kwa muda shughuli za baharini.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema kuwa kimbunga Jobo kinachozidi kusogea ukanda wa Pwani wa Tanzania kinatarajiwa kutua Dar es Salaam Aprili 25 huku kikitarajiwa kuleta athari za upepo mkali, mawimbi makubwa baharini na mvua kubwa.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dk Agness Kijazi amewaambia wanahabari jijini Dar es Salaam kuwa kimbunga kama hicho hakijawahi kutokea tangu mwaka 1952 na kuwasihi Watanzania hasa wanaofanya shughuli zao baharini kuchukua tahadhari zikiwemo kusitisha shughuli zao kwa muda kutazamia mwelekeo wake.
“Kimbunga kitakachotua Dar es Salaam kitakuwa kimepungua nguvu kitakuwa na kilomota 60 kwa saa. Lakini tufahamu kuwa kasi ya kilomita 60 kwa saa japo kuwa ni nguvu iliyopungua ikilinganishwa na jinsi upepo ulivyo sasa bado ni mkubwa unaweza kuleta athari,” amesema Dk Kijazi.
Amewataka wakazi wa mikoa ya ukanda wote wa Pwani kuanzia Mtwara, Lindi, Tanga, Mafia, Dar es Salaam, Pwani na Zanzibar kuchukua tahadhari ya upepo mkali unaotarajiwa wa kimbunga kitakachokuwa Jumapili hii.
Dk Kijazi amewasihi wanaotumia bahari hususan wavuvi na wengineo kuchukua tahadhari ikiwemo kusubiri kwanza kutazamia mwenendo wa kimbunga hicho.
Kimbunga Jobo kutua Dar Aprili 25 mwaka huu kikitokea kaskazini mwa kisiwa cha Madagascar, wananchi hasa wanaotumia bahari ya hindi watakiwa kuchukua tahadhari.
Kinaweza kusababisha ongezeko la Kasi ya upepo, mawimbi na mvua kubwa.#NuktaVideoYaSIku
pic.twitter.com/zqcJJvBvR2— Nukta Tanzania (@NuktaTanzania) April 23, 2021
“Kwa sasa hivi wananchi wachukue tahadahari wale wanaotumia bahari ambako kimbunga hiki kipo kuna upepo mkali baharini pamoja na mawimbi makubwa. Mtu aangalie chombo chake katika usawa baharini kama kinaweza kustahimiri.
“Kwa wavuvi katika ukanda wa Pwani ni bora wakasubiri kwanza hali ya kimbunga kiweze kupita weweze kuendelea sasa na shughuli zao,” amesema.
Soma zaidi:
- Kimbunga Kenneth kuikumba Mtwara, Lindi
- Tahadhari: Kimbunga Jobo pwani ya Lindi, Mtwara
- Taarifa muhimu ya muendelezo wa Kimbunga Kenneth Tanzania
Dk Kijazi amesema kuwa mamlaka mbalimbali za Serikali zitatoa matamko kwa wananchi juu ya hatua ya kuzitekeleza na maeneo ambayo shughuli zinaweza kusitishwa.
Mbali na ukanda wa Pwani, Dk Kijazi amesema kimbunga hicho kinaweza kuathiri hadi ukanda wa Magharibi kwa kuleta mvua kubwa.
“Vimbunga kama hivi si kawaida kutokea katika maeneo yaliyo karibu na Ikweta. Tuna muda mrefu haikijawahi kutokea. Mwaka 1872 kulikuwa na kimbunga kilitua Dar es Salaam. Lakini 1952 kilikuwepo kimbunga Lindi kiliweza kuleta athari.
TMA imewataka wananchi kuendelea kufuatilia na kuzingatia taarifa za utabiri kutoka TMA pamoja na kupata ushauri na miongozo ya wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.
Latest
