TMA: Kimbunga ‘Freddy’ hakina madhara kwa sasa
- Yasema sehemu zote za nchi zipo salama
- Wananchi watakiwa kuzingatia taarifa na tahadhari za hali mbaya ya hewa zinazotolewa
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa ufafanuzi kuhusu uwepo wa kimbunga ‘Freddy’ kilichopo kusini magharibi mwa bahari ya Hindi karibu na pwani ya Madagascar, kilichotarajiwa kuikumba pwani ya afrika mashariki mwanzoni mwa wiki hii.
Kwa mujibu wa ufafanuzi huo uliotolewa leo February 20,2023, TMA imesema kimbunga hicho hakina madhara ya moja kwa moja kwenye maeneno mengi yaliyopo nchini tofauti na upotoshaji unaoendelea kwenye kwenye mitandao ya kijamii.
“TMA inaendelea kufuatilia kwa kina mwenendo wa kimbunga hiki na itatoa taarifa punde tu kutakapokuwa na haja ya kufanya hivyo”, inasema taarifa hiyo.
Kwa takribani kipindi cha wiki moja iliyopita kulizuka taarifa ya ujio wa kimbunga hicho ikiripotiwa na vyombo vya habari mbalimbali vya kitaifa na mamlaka za hali ya hewa za kimataifa ikiwemo Taasisi ya Hali ya Hewa Duniani (WMO).
Hii si mara ya kwanza kwa tahadhari za vimbunga kutangazwa ukanda wa Afrika Mashariki na nchini Tanzania,.
Mwaka 2021 mamlaka hiyo ilitangaza ujio wa kimbunga ‘Jobo’ kilichotarajiwa kuathiri maeneo ya pwani ya Tanzania mnamo April 25,2 2021.
Kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kuibuka kwa upepo kinzani kwenye ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi kimbunga hicho kilizidiwa nguvu na kushindwa kuathiri maeneo yalyliyokusudiwa.
Soma zaidi
-
Haya ndiyo maeneo utakayokutana na uzushi mwingi mtandaoni
-
Tanzania yaunga mkono azimio la chanjo kwa watoto Afrika
Wananchi zingatieni taarifa za tahadhari
Kupitia taarifa hiyo TMA imewata ka wananchi na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania pamoja na kutafuta, kupata na kufuata ushauri wa wataalamu katika sekta husika ili kupunguza athari zinazotokana na hali mbaya ya hewa.
Pamoja na hayo imewakumbusha wananchi wanaojihusisha na kusambaza taarifa zisizo na ukweli kuhusu hali ya hewa nchini kuacha mara moja kwani ni kinyumme na sheria na taratibu.
“Mamlaka inapenda kuikumbusha jamii na umma kwa ujumla kuwa kwa mujibu wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya 2019, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ndiyo pekee yenye mamlaka ya kutoa taarifa za tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa na ni kosa kisheria mtu mwingine kufanya hivyo,” imesema TMA .