Ahueni: Kimbunga Jobo chapungua nguvu ghafla, kutua Dar kesho
- Kimbunga Jobo kilichopo bahari ya Hindi kwa sasa kipo umbali wa kilomita 200 mashariki mwa kisiwa cha Mafia.
- Kimbunga hicho kimepungua nguvu kwa haraka baada ya kuingia katika mazingira yenye mzunguko wa upepo kinzani.
- Kitatua Dar es Salaam kesho, wananchi watakiwa kuchukua tahadhari.
Dar es Salaam. Licha ya kasi ya kimbunga Jobo kinachozidi kusogea katika mikoa pwani ya Tanzania kupungua nguvu, wananchi wa mikoa hiyo wametakiwa kuendelea kuchukua tahadhari kutokana na kuwepo kwa vipindi vya mvua kubwa, upepo mkali na mawimbi.
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema kwa kimbunga Jobo kilichopo bahari ya Hindi kwa sasa kipo umbali wa kilomita 200 mashariki mwa kisiwa cha Mafia.
Kimbunga hicho kimepungua nguvu kwa haraka baada ya kuingia katika mazingira yenye mzunguko wa upepo kinzani.
“Hivyo Jobo kwa sasa ni kimbunga hafifu kinachosafiri kwa kasi ya kilometa 18 kwa saa baharini,” imesema taarifa ya TMA iliyotolewa leo mchana Aprili 24, 2021.
Hata hivyo, kimbunga hicho kinatarajiwa kusababisha vipindi vya mvua kubwa katika maeneo machache hususan ya ukanda wa Pwani kadiri kinavyosogea nchi kavu kwa siku ya leo na kesho.
Soma zaidi:
- Kimbunga Kenneth kuikumba Mtwara, Lindi
- Tahadhari: Kimbunga Jobo pwani ya Lindi, Mtwara
- Taarifa muhimu ya muendelezo wa Kimbunga Kenneth Tanzania
Izingatiwe kuwa uwepo wa kimbunga hafifu baharini, unatarajiwa kusababisha mawimbi makubwa na upepo ambao unaweza kuathiri shughuli za uvuvi.
Maeneo yanayotarajiwa kupata athari za moja kwa moja ni pamoja na mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani (ikiwemo kisiwa cha Mafia), Dar es Salaam pamoja na kisiwa cha Unguja.
Kimbunga kama hicho hakijawahi kutokea tangu mwaka 1952 ambapo TMA imewasihi Watanzania hasa wanaofanya shughuli zao baharini kuchukua tahadhari zikiwemo kusitisha shughuli zao kwa muda kutazamia mwelekeo wake.
“Kwa sasa hivi wananchi wachukue tahadahari wale wanaotumia bahari ambako kimbunga hiki kipo kuna upepo mkali baharini pamoja na mawimbi makubwa. Mtu aangalie chombo chake katika usawa baharini kama kinaweza kustahimiri.
“Kwa wavuvi katika ukanda wa Pwani ni bora wakasubiri kwanza hali ya kimbunga kiweze kupita weweze kuendelea sasa na shughuli zao,” alisema Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi Aprili 23 mwaka huu.
Latest
