Mbowe: Kutoka gerezani hadi Ikulu

March 5, 2022 12:45 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link

Rais Samia Suluhu Hassan, akizungumza na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe alipowasili Ikulu Jijini Dar es Salaam leo March 4, 2022. Picha| Ikulu.

Akutana na Rais Samia saa chache baada ya kutoka gerezani.

  • Ni baada ya ufutiwa mashtaka ya ugaidi.
  • Wawili hao wateta kuhusu maridhiano, haki na maendeleo ya Tanzania.

Dar es Salaam.  Hatimaye Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Samia Suluhu Hassan saa chache baada ya kufutiwa mashtaka ya ugaidi yaliyokuwa yakimkabili na wenzake watatu.

Tangu Rais Samia alipoingia  madarakani Machi mwaka jana, Mbowe amekuwa akitafuta fursa ya kuonana na Rais ili kuzungumzia mstakabali wa chi lakini hakufanikiwa mambo mbalimbali ikiwemo kesi iliyokuwa ikimkabili ambayo leo Mwendesha Mashtaka (DPP) ameonyesha nia ya kutokuendelea nayo.

Rais Samia na Mbowe wamekutana leo Machi 4, 2022 Ikulu jijini Dar es Salaam ambapo mazungumzo yao yalijikita katika ujenzi wa nchi hasa kuzingatia misingi ya kufanya kazi kwa pamoja na maridhiano.

“Rais Samia amesisitiza kuwa kuna umuhimu wa kushirikiana ili kuijenga Tanzania kwa kuaminiana na kuheshimiana kwa misingi ya haki,” imeeleza taarifa ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Zuhura Yunus.

Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa Mbowe amemshukuru Rais Samia kwa kuonyesha kujali huku akikubali kuwa msingi mkubwa wa kujenga Taifa la Tanzania ni kusimama katika haki.

Amesema wamekubaliana kufanya siasa za kistaarabu na za kiungwana na kuwa yuko tayari kushirikiana na Serikali katika kuleta maendeleo ili nao pia waweze kutekeleza majukumu yao ipaswavyo.

Mbowe na wenzake watatu Khalfani Bwire, Adam Kasekwa na Mohammed Ling’wenya katika kesi hiyo, iliyovuta hisia tofauti za watu wengi tangu ianzwe kusikilizwa, walikuwa wanakabiliwa na mashtaka sita yakiwemo ya kufadhili vitendo vya ugaidi na kukusanya pesa kwa ajili ya kufanya vitendo vya kigaidi. 

Mashtaka mengine ni kushiriki kula njama kutenda vitendo vya kigaidi, kukutwa na silaha aina ya bastola na kukutwa na sare za jeshi kinyume cha sheria.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW