Sekta binafsi inavyoweza kushiriki katika uhifadhi wa wanyamapori Tanzania
- Kutoa rasimali watu na fedha kwa kuendeleza wanyamapori.
- Kushiriki katika mafunzo na uboreshaji wa sera za uhifadhi.
- Waandishi wa habari nao wahimizwa kuwa sehemu ya safari hiyo.
Dar es Salaam. Wadau wa masuala ya uhifadhi wamesema sekta ya wanyamapori inaweza kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania ikiwa sekta binafsi itashirikishwa kikamilifu katika shughuli za uhifadhi endelevu.
Wanyamapori wanaopatikana katika hifadhi za Taifa na maeneo mengine tengufu wamekuwa wakitumika katika shughuli za utalii na uwindaji na hivyo kuipatia nchi mapato ambayo yanatumika katika kuboresha huduma za kijamii.
Hata hivyo, sekta hiyo ndogo inaweza kuendelea kuwa na mchango katika pato la Taifa, ikiwa wadau wote ikiwemo sekta binafsi watashiriki katika uhifadhi endelevu wa wanyamapori ambao kwa sasa unatishiwa na mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la watu katika maeneo ya uhifadhi na ukosefu wa rasilimali watu na fedha.
Afisa Miradi kutoka Jumuiya ya Uhifadhi ya Chem Chem (CCA), Walter Pallangyo amesema sekta binafsi inaweza kushiriki katika uhifadhi wa wanyamapori kwa namna mbalimbali ikiwemo kutoa fedha kufadhili shughuli za uhifadhi.
Walter aliyekuwa akizungumza katika mdahalo wa uhifadhi wa wanyamapori ulioandaliwa na Chama cha Waandishi wa habari za Mazingira Tanzania (JET) wiki hii amesema Serikali peke yake haiwezi kutimiza jukumu la uhifadhi kwa sababu haina fedha za kutosha.
Mdau huyo kutoka Che Chem inayoendesha shughuli za uhifadhi katika ushoroba wa Kwakuchija ambao ni mapitio ya wanyamapori kati ya hifadhi za Taifa za Manyara na Tarangire amesema fedha kutoka kwa wadau wa sekta binafsi zinasaidia kununua vifaa, kufanya doria dhidi ya majangili, matengenezo ya magari na mafunzo kwa jamii kuhusu uhifadhi.
“Sekta binafsi inaweza kushirikiana na jamii zinazozunguka hifadhi katika shughuli za kiuchumi na kijamii zinazochochea uhifadhi na mapitio ya wanyamapori,” amesema Pallangyo.
Amesema, taasisi yake imekuwa ikizisaidia jamii zinazoishi karibu na hifadhi kwa kuzipatia huduma za kijamii ikiwemo shule na misaada ya kifedha ili kuanzisha miradi ya kiuchumi, jambo linalosaidia jamii hizo kutoshiriki katika vitendo vya ujangili.
Soma zaidi:
- Mbinu zilizotumika kukomesha ujangili wa tembo Rufiji
- Botswana yapoteza zaidi ya tembo 300 ndani ya miezi mitatu
- Mvutano wa tembo, binadamu unavyoacha maumivu Tanzania – 1
Sekta binafsi inaweza kuchangia katika kutafuta masoko ya bidhaa za utalii zilizopo nchini kwa kuvutia watalii wa kimataifa kuja katika hifadhi za wanyamapori ili kutengeza ajira kwa watoa huduma za utalii na kuongeza mapato kwa Serikali.
“Ni wajibu wa sekta binafsi kuchagiza utekelezaji wa sera nzuri za uhifadhi,” amesema Pallangyo huku akibainisha kuwa taasisi yake imekuwa ikishiriki katika mikutano, majadiliano na kampeni mbalimbali zinazolenga kuweka mazingira rafiki kwa wanyamapori.
Eneo lingine ambalo ni muhimu, ni sekta binafsi kuendelea kushiriki katika tafiti za wayamapori nchini ambazo zinasaidia kufahamu hali halisi ya uhifadhi wa viumbe hao, changamoto zilizopo na suluhu za kudumu za kukabiliana tishio la kutoweka kwao.
“Tunapaswa kuzuia usafirishaji wa wanyamapori na vitendo vingine haramu ikiwemo ujangili, uharibifu wa makazi ya wanyamapori na kuimarisha mtandao wa uchunguzi na watoa habari kuhusu uharifu wa wanyamapori,” amesema Pallangyo katika mdahalo huo ambao uliwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari za mazingira Tanzania.
Licha ya sekta binafsi kuwa mshirika muhimu wa uhifadhi, kibaruau walichonacho wadau hao ni kuongeza kasi ya kudhibiti ujangili unaohusishwa na nyamapori, ongezeko la watu katika maeneo ya hifadhi, ufugaji na uvuvi haramu, migogoro ya binadamu na wanyamapori na vifo vya wanyamapori vinavyotokana na ajali za barabarani.
Askari wanyamapori wakishirikiana na wataalam kutoka WWF Tanzania kufunga vitambaa vyenye oili na pilipili kwenye uzio wa waya ili kuzuia tembo kuingia kwenye mashamba ya wakulima katika kijiji cha Ngarambe wilayani Rufiji. Picha|WWF Tanzania.
Victoria Michael, Mchambuzi wa Sera kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) amesema taasisi hiyo ni mwamvuli wa shughuli za uhifadhi zinazoratibiwa na sekta binafsi.
Amesema kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la Misaada la Marekani linalotekeleza mradi wa Tuhifadhi Maliasili (USAID PROTECT), wameweza kutetea ushirikishwaji wa sekta binafsi katika uhifadhi wa mazingira na kupambana na uhalifu wa wanyamapori.
“Baadhi ya mipango na hatua muhimu zilizofikiwa ni pamoja na uundaji wa Kamati ya Sekta Binafsi ya uhifadhi wa mazingira,” amesema Michael.
Pia TPSF imefanikiwa kuendesha mafunzo kwa zaidi ya makampuni 190 ya sekta binafsi katika sekta zote za uchumi kuhusu uhifadhi Tanzania.
Amesema wanaendelea kuhimiza sekta binafsi kusaidia shughuli za uhifadhi na mnyororo wa thamani katika maeneo ya uwekezaji ili kutengeneza ajira na mapato.
Awali, akifungua mdahalo huo, Mwenyekiti wa JET, Dk Hellen Otaru amewataka waandishi wa habari kuwa sehemu ya safari hiyo ya uhifadhi kwa kuibua masuala mbalimbali ili kuhakikisha mchango wa sekta hiyo unawanufaisha wananchi na Taifa.