TMA yatahadharisha mvua kubwa katika mikoa 8
- Mikoa hiyo ni pamoja na Lindi, Mtwara, Morogoro, Iringa, Ruvuma, Songwe, Mbeya na Njombe.
- TMA yawataka wananchi kuchukua tahadhari.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa angalizo la halimbaya ya hewa na mvua kubwa inayoweza kunyesha katika mikoa nane nchini ikiwemo mkoa wa Morogoro.
Angalizo hilo litahusisha mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro, Iringa, Ruvuma, Songwe, Mbeya na Njombe, ambapo itadumu kwa siku tano kuanzia Januari 30, hadi Februari 2 mwaka huu.
Soma zaidi:Rais Samia awataka wanaoishi mabondeni kuhama kuepuka maafa
Taarifa iliyotolewa na TMA leo Januari 29, 2024 inabainisha kuwa uwezekano wa kutokea kwa mvua hizo ni wa wastani na hata kiwango cha athari zinazoweza kutokea ni cha wastani pia.
“Athari zinazoweza kujitokeza baadhi ya makazi kuzingirwa na maji pamoja na kuathirika kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi, zingatia jiandae,” imesema TMA.
Mbali na angalizo hilo la TMA, viongozi mbalimbali wa Serikali wamekuwa wakiotoa rai kwa wananchi kuchukua hatua za mapema ili kuepuka athari zitokanazo na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha nchini.
Januari 21, 2023 Rais Samia aliyekuwa akizungumza katika hafla ya kumuingiza kazini Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT, Dk. Alex Malasusa aliwataka wananchi kuchukua tahadhari ili “kuiepusha nchi na misiba mikubwa”.
“Tunawataka wananchi wawe na hadhari, wale wanaohisi wanaishi maeneo ya hatari, waondoke wasogee juu…hatuwezi kudhibiti kiwango cha mvua kinachonyesha…
…Niombe sana wananchi tuchukue tahadhari na kuliepusha taifa na misiba mikubwa au hatari kubwa zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi,” alisisitiza Rais Samia.
Hata hivyo, TMA imebainisha kuwa upepo wa pwani unatarajiwa kuvuma kwa kasi ya Km 20 kwa saa kutoka kaskazini kwa pwani ya kusini na kwa kasi ya Km 30 kwa saa kutoka kaskazini mashariki kwa pwani ya kaskazini huku bahari ikitarajiwa kuwa na mawimbi madogo hadi makubwa kiasi.