Tahadhari ya mvua kubwa mikoa 11 yatolewa
- Ni pamoja na mikoa ya Mbeya, Iringa, Njombe na Dar es Salaam.
- Athari zinazotarajiwa kutokea ni za wastani.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa tahadhari ya kuwapo kwa mvua kubwa katika mikoa 11 nchini ikiwamo mikoa ya Mbeya, Iringa, na Njombe.
Taarifa ya mamlaka hiyo iliyotolewa leo Januari 11, 2024 katika mitandao yao ya kijamii imebainisha kuwa mvua kubwa itanyesha ndani yaa saa 24 zijazo kuanzia saa tatu kamili usiku.
“Vipindi vifupi vya mvua kubwa vinatarajiwa katika maeneo machache ya mikoa ya Mbeya, Iringa, Njombe, Songwe, Rukwa, Ruvuma, Mtwara, Lindi, Morogoro, Dar es salaam na Pwani,” imebainisha taarifa hiyo.
Awali Januari 9, 2024 TMA walitoa tahadhari ya mvua kubwa kwa siku nne mfululizo katika maeneo mbalimbali, wakitabiri kutokea kwa athari za wastani kutokana na mvua hizo.
UTABIRI WA HALI YA HEWA 11.01.2023 pic.twitter.com/vsVnRztr0X
— Tanzania Meteorological Authority (@tma_services) January 11, 2024
Miongoni mwa athari zilizobainishwa ni pamoja na makazi kuzingirwa na maji, na kuathirika kwa shughuli za kiuchumi.
Hivi karibuni nyumba zaidi ya 30 ziliathirika kutokana na maporomoko ya udongo uliochanganyika na mawe yaliyoyasababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika kata ya Kilomeni,Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro.
Agosti 26, 2023 TMA ilitoa taarifa ya uwezekano wa kuwapo kwa mvua kubwa za El-Nino ambazo huenda zikasababisha vifo, magonjwa ya mlipuko na uharibifu wa miundombinu kuanzia Oktoba hadi Desemba 2023.
TMA ilisema mvua hizo zitasababisha mafuriko na maporomoko ya ardhi, upotevu wa mali na madhara kwa binadamu na mazingira.
Madhara makubwa zaidi yanayokumbukwa ni mafuriko ya matope yaliyotokea Disemba 3, 2023 wilayani Hanang, ambapo watu 89 walipoteza maisha huku wengine zaidi ya 130 wakijeruhiwa.
Latest
