Sekta binafsi kuwabeba wamachinga Tanzania
- Yatakiwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya biashara wamachinga.
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Innocent Bashungwa, ameitaka sekta binafsi na washirika wa maendeleo kushirikiana na Serikali kuwatengenezea mazingira wezeshi wafanyabiashara ndogo (Wamachinga) ili waweze kukuza biashara zao na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Bashungwa aliyekuwa akizungumza Mei 20, 2022 jijini Dodoma wakati akifungua warsha ya wamachinga iliyoandaliwa na Wizara ya Fedha na Mipango kwa ushirikiano na Mfuko wa Uendelezaji wa Sekta ya Fedha nchini (FSDT) amesema kundi hilo linahitaji kupewa kipaumbele nchini.
“Wamachinga wakijenjengewa mazingira mazuri yatakayowawezesha kukuza mitaji yao, ni fursa nzuri kwa mabenki kwa kuwa yatakuwa na wateja wa kuwakopesha,” amesema Bashungwa.
Wadau waliohudhuria warsha hiyo wametakiwa kufanya uchambuzi wa maeneo yanayofanya vizuri kwa wamachinga, changamoto na fursa ili kujua wajibu wa kila mmoja katika kuhakikisha wafanyabiashara hao wanakua na kuleta tija stahiki kwa Taifa.
Kwa sasa, Serikali iko mbioni kutunga sheria itakayosimamia shughuli na maslahi ya wamachinga nchini ili kuwasaidia Watanzania waliojiajiri katika sekta hiyo isiyo rasmi kuboresha maisha yao.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mwanaidi Ali Khamis amesema kuwa shughuli za machinga zimesaidia kutatua changamoto za ajira kwa vijana kwa kujiajiri na kuwa sehemu ya ukuaji wa uchumi wa nchi.
Kutokana na umuhimu huo, amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa kundi la wamachinga linahudumiwa kwa upekee kwa kuratibu shughuli wanazozifanya ili ziweze kuwanufaisha na kuwaletea maendeleo.
Zinazohusiana:
- Flyover ya Tazara ilivyoleta maumivu, faida kwa wafanyabiashara ndogondogo
- Serikali kuwalipa wafanyabiashara marejesho ya VAT
- Rais Magufuli atoa vitambulisho maalum kwa wafanyabiashara wadogo
Bajeti ya 2022/23 kuwajumuisha wamachinga
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Lawrence Mafuru, amesema kuwa wizara yake ipo katika hatua za kutengeneza Bajeti Kuu ya Serikali ambapo itawajumuisha wamachinga katika utekelezaji wake.
Amesema kuwa warsha ya wamachinga itasaidia kutoa fursa ya kujifunza lakini pia kuwa na sera itakayoelekeza rasilimali fedha kutoka kwa wadau mbalimbali inapatikanaje kwa ajili ya eneo hilo.
Eneo la wamachinga linahudumiwa na wizara nyingi ikiwemo Tamisemi, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum pia katika maeneo ya kiutawala kama Mikoa na Wilaya.
Mafuru ameshauri kuwa na muelekeo mmoja kama Serikali badala ya kulishugulikia suala hilo kwa uelewa wa mtu mmoja mmoja, hivyo warsha hiyo ni muhimu katika kupata maoni ya wadau.
Mwenyekiti wa Wamachinga Taifa, Ernest Masanja,amesema kuwa kundi la wamachinga lilitengwa lakini sasa linashirikiana vizuri na Serikali hivyo akaahidi wamachinga kuiunga mkono Serikali katika jitihada zake za maendeleo.
Warsha hiyo imewakutanisha makatibu wakuu wa kisekta, wakuu wa mikoa, makatibu tawala wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakuu wa idara, viongozi wa wamachinga na wadau wengine.
Latest