Rais Samia aagiza wamachinga kupangwa upya

September 13, 2021 12:54 pm · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link

                         


  • Ameagiza wafanyabiashara hao kuwekewa maeneo ya biashara.
  • Amesema itapunguza usumbufu kwa wafanyabiashara wengine.
  • Aagiza zoezi lifanyike kwa kufuata sheria na kwa utulivu. 

Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan, amewataka Wakuu wa Mikoa nchini kuwapanga upya Wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama Wamachinga, bila kutumia nguvu ili wafanye biashara kwa kufuata taratibu zilizowekwa.

Rais Samia ametoa maagizo hayo leo Septemba 13, 2021 jijini Dodoma wakati akiwaapisha mawaziri wanne na Mwanasheria Mkuu, Dk Eliezer Feleshi walioteuliwa jana.

Mkuu huyo wa nchi amesema Serikali iliwapa uhuru wamachinga kufanya biashara ili wapate kipato na kupunguza utegemezi lakini uhuru wao hautakiwi kuvuka mipaka kiasi cha kuwaletea changamoto wafanyabiashara wengine.

“Watu hawa sasa wameenea kila pahali. Kila pahali mpaka kwenye maduka wao wanaziba maduka hayauzi wanauza wao mbele. Mpaka sasa wenye maduka baadhi yao wamepata na wenyewe mtindo wa kutoa bidhaa ndani na kuwapa wamachinga kuuza kwa sababu watu hawaingii ndani,” amesema Rais Samia.

Amesema kitendo hicho kinaikosesha Serikali kodi kwa sababau pale wenye maduka wanapowapa wamachinga mzigo wauze, wanakuwa hawatoi kodi kwani machinga hawalipi kodi.

Baadhi ya machinga huweka bidhaa zaombele ya mdaka. Picha| Rodgers George.

Kufuatia hali hiyo, Rais Samia amewaagiza wakuu wa mikoa kuweka utaratibu mzuri wa kuwapangia maeneo wafanyabiashara hao pasipo kuwaonea.

“Sitaki kuona yale ninayoyaona kwenye TV (televisheni) ngumi, kupigana, kufukuzana, kuchafuliana, vitu kumwagwa ah ah! Mnaweza kuchukua hatua vizuri na kuwapanga vyema bila kuudhi wenye maduka bila kuudhi wamachinga na maisha yakaendelea,” amesema Rais.

Aidha, Rais Samia amewaagiza wamachinga kufuata sheria na kanuni zilizopo na kuwasikiliza wakuu wa mikoa na wa wilaya wanapowapanga katika maeneo ya biashara.

Tayari Mkoa wa Dar es Salaam umeanza kuchukua hatua ya kuwapanga upya wafanyabiashara wadogo hasa wale wanaofanya biashara kandokando ya barabara ili kupunguza usumbufu kwa watumiaji. 

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makala ambaye siku nne  zilizopita alipotembelea mtaa wa kibiashara wa Kariakoo na alitangaza kuwa njia zote za wapita kwa miguu kweye mkoani hapo ziwe wazi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW