Watalii wa kimataifa waongezeka zaidi ya mara tatu 2022

September 28, 2022 12:41 pm · Abdushakur
Share
Tweet
Copy Link
  • Hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 172 kati ya Januari hadi Julai 2022.
  • Sekta ya utalii yaimarika kwa asilimia 60 mwaka huu.
  • UN yaonya hatua zichukuliwe kulinda mazingira.

Dar es Salaam. Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii UNWTO limesema sekta ya utalii duniani imeimarika kwa asilimia 60 huku idadi ya watalii wa kimataifa ikiongezeka zaidi ya mara tatu mwaka huu.

UNWTO imesema kuimarika kwa sekta ya utalii duniani kumechangiwa na hatua kubwa iliyopigwa na dunia katika mapambano dhidi ya Uviko-19. 

Kwa mujibu wa UNWTO sekta ya utalii inazidi kuimarika na taarifa za kuanzia Januari mpaka Julai 2022 zinaonesha idadi ya watalii kimataifa iliongezeka kwa asilimia 172 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka jana.

Ongezeko la idadi hii ya watalii inamaanisha kuwa sekta hii ya utalii imeimarika kwa asilimia 60 ikilinganishwa na kipindi cha kabla ya janga la Uviko-19.  

Hatua ya nchi mbalimbali duniani kupunguza vizuizi vya usafiri, ni miongoni mwa sababu muhimu zzilizochangia kuwepo kwa ongezeko hili ambalo halikutarajiwa hapo awali kutokana na uwepo wa janga la Uviko-19.

Hadi kufikia Septemba 19, 2022 nchi 86 ulimwenguni zimeondoa kabisa vikwazo vya usafiri vinavyolenga kuzuia kusambaa kwa virusi vya Corona.


Soma zaidi


Hata hivyo, Katibu Mkuu wa UNWTO Zurab Pololikashvili katika taarifa yake iliyotolewa jana Septemba 28,2022 ameonya juu ya mabadiliko hasi ndani ya sekta hiyo kwa siku za usoni endapo changamoto kadhaa zisipofanyiwa kazi. 

“Kutoka kwenye siasa za kijiografia hadi za kiuchumi. Sekta ya utalii inarudisha matumaini na fursa kwa watu kila mahali. Sasa ni wakati wa kufikiria upya utalii, unakokwenda na jinsi unavyoathiri watu na sayari,” amesema Pololikashvili.

Akiweka msisitizo juu ya shughuli za utalii duniani Katibu Mkuu wa Umoja Wa Mataifa Antonio Guterres  katika ujumbe wake wa Siku ya Utalii Duniani ameikumbusha dunia kuwa utalii unapaswa kufanyika kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira, sayari, kulinda asili pamoja na kukuza uelewa wa kitamaduni.

“Utalii ni kichocheo kikubwa cha maendeleo endelevu. Unachangia elimu na uwezeshaji wa wanawake na vijana na kuendeleza maendeleo ya jamii na utamaduni ya zao. 

“Utalii unachukua sehemu muhimu katika mifumo ya ulinzi wa kijamii ambayo inaunda msingi wa uthabiti na ustawi.” amesema Guterres.

Guterres amesema kuwa  wakati utalii ukizidi kuimarika ulimwenguni , ni wakati mwafaka kwa Serikali na wafanyabiashara kuzidi kuwekeza kwenye utalii safi na endelevu, pasi kusahau kupunguza matumizi ya nishati,  uchafuzi wa hewa na kulinda bayoanuwai.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW