Ukweli kuhusu idadi ya watu waliopata chanjo ya Uviko-19
- Baadhi ya watu wanasema ni milioni 22 lakini WHO inasema ni idadi ya dozi zilizosambazwa.
Dar es Salaam. Kumekuwa na habari zinazosambaa mtandaoni zikionyesha Watanzania milioni 22 tayari wamechanjwa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Corona (Uviko-19), jambo ambalo siyo kweli kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).
WHO imesema hadi kufikia Agosti 20, 2022 Watanzania milioni 16.4 ndiyo walikuwa wamepata dozi kamili ya ugonjwa huo.
Shirika hilo limeeleza pia kuwa Watanzania milioni 18.2 wamepata angalau dozi moja wapo kati ya zile zinazotolewa nchini. Chanjo zinazotolewa nchini ni pamoja na Sinopharm, Jonhson&Johnson, Pfzier na Sinovac.
Taarifa hizo kutoka WHO ni tofauti na taarifa zinazosambaa mtandaoni kuwa waliopata chanjo kamili ya ugonjwa wa Uviko-19 ni milioni 22.
Ukweli uko wapi?
Kwa mujibu wa WHO, milioni 22 siyo idadi ya watu waliochanja bali ni idadi ya dozi ya chanjo zilizotolewa kwa Tanzania ambazo baadhi tayari wamechanjwa watu.
“Hadi kufikia Agosti 20, 2022 jumla ya chanjo za Corona milioni 22 zimetolewa (administered) nchini Tanzania,” limeeleza shirika hilo.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya nchini Tanzania, hadi kufikia Julai 29, 2022, Watanzania milioni 4.2 walikuwa wamepata dozi kamili ya chanjo ya Uviko-19.
Serikali ya Tanzania ina mpango kuchanja watu milioni 21.5 ifikapo Desemba 2022.
Chukueni tahadhari
WHO na Wizara ya Afya bado inasisitiza watu kuchukua tahadhari kukabiliana na kusambaa kwa virusi vya Corona ikiwemo kunawa mikono kwa maji tiririka, kutumia vitakasa mikono kuvaa barakoa pamoja na kupunguza misongamano.
Ili kupata habari sahihi kuhusu chanjo ya Uviko-19 na ugonjwa wa corona tembelea vyanzo rasmi vya habari kama Shirika la Afya Duniani (WHO) na Wizara ya Afya nchini Tanzania.
Latest
