Ufanisi ukusanyaji kodi waongezeka, Serikali akianika bajeti ya 2020-2021

March 12, 2020 7:08 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango wakati alipowasilisha  Mapendekezo kuhusu  mpango na kiwango cha Ukomo  wa Bajeti ya Serikali 2020/2021 katika mkutano wa wabunge uliofanyika kwenye ukumbi wa Msekwa, bungeni jijini Dodoma, Machi 11, 2020. Picha|Ofisi ya Waziri Mkuu.


  • Serikali imesema mapato ya yatakonayo na kodi katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita umeongezeka kwa asilimia 16.6.
  • Katika kipindi cha Julai 2019 hadi Januari 2020, ufanisi wa kukusanya mapato ya kodi umeimarika na kufikia asilimia 96.9 ya lengo ikilinganishwa na ufanisi wa asilimia 88.6 katika kipindi cha Julai 2018 hadi Januari 2019.
  • Waziri wa Fedha, Dk Mpango asema sababu kubwa ni kuzibwa kwa mianya ya ulipaji kodi.

Dar es Salaam. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amesema ufanisi wa kukusanya mapato ya Serikali yatakonayo na kodi katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita umeongezeka kwa asilimia 16.6 ukichagizwa na kuzibwa kwa mianya ya ulipaji kodi. 

Dk Mpango alikuwa akizungumza jana (Machi 11, 2020) jijini Dodoma wakati akiwasilisha mapendekezo ya kiwango na ukomo wa bajeti ya mwaka 2020/21 ambapo Serikali inatarajia kukusanya na kutumia Sh34.88 trilioni.

Kati ya fedha hizo, Sh21.98 trilioni zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh12.90 trilioni za matumizi ya maendeleo sawa na asilimia 37 ya bajeti yote. 

Bajeti ya matumizi ya maendeleo inajumuisha Sh10.16 trilioni ni fedha za ndani, sawa na asilimia 78.8 na Sh2.74 trilioni fedha za nje ambapo matumizi hayo yanajumuisha gharama za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Dk Mpango amesema katika kipindi cha Julai 2019 hadi Januari 2020, ufanisi wa kukusanya mapato ya kodi umeimarika na kufikia asilimia 96.9 ya lengo ikilinganishwa na ufanisi wa asilimia 88.6 katika kipindi cha Julai 2018 hadi Januari 2019, sawa na ukuaji wa asilimia 16.6. 

Amebainisha kuwa katika kipindi cha Julai 2019 hadi Januari 2020, Serikali ilikusanya mapato ya kodi ya Sh10.62 trilioni sawa na asilimia 96.9 ya makadirio ya Sh10.96 trilioni.

“Sababu za ongezeko la mapato yaliyokusanywa na TRA ni pamoja na: kuongezeka kwa utoaji wa elimu ya walipakodi; wananchi kuhamasika kulipa kodi kutokana na kuimarika kwa utoaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ikijumuisha maji, elimu, afya, miundombinu wezeshi ya barabara na umeme,” ameeleza Dk Mpango katika hotuba yake.

 


Zinazohusiana: 


Sababu nyingine ni kuendelea kuongezeka kwa uwazi katika usimamizi wa sheria za kodi, maboresho ya huduma kwa mlipakodi, usimamizi wa matumizi ya mashine za kutolea risiti za kielektroniki hususan kwenye sekta ya usafirishaji wa bidhaa mbalimbali, 

Pia kuendelea kuziba mianya ya ukwepaji kodi kwa kuwashirikisha kikamilifu na kuwaelimisha ipasavyo wale wote ambao wamekuwa wakibainika kukwepa kodi kumesaidia kuimarisha ufanisi wa ukusanyaji kodi. 

Hata hivyo, Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuongeza makusanyo zaidi ikiwemo kusimamia utekelezaji wa sheria, kanuni na taratibu za kodi; kuhakikisha mfumo wa usimamizi wa mashine za kielektroniki za kutolea risiti unatumika ipasavyo.

“Tutaendelea kupitia nyaraka za walipa kodi kwa lengo la kufanya usuluhishi wa kodi walizolipa kwa kujikadiria wao wenyewe ikilinganishwa kiasi halisi walichopaswa kulipa kwa mujibu wa sheria,” amesema Waziri huyo.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...