Udumavu, mimba za utotoni, kuwaweka wakuu wa mikoa kikaangoni
- Ni baada ya kuripotiwa ongezeko la mimba za utotoni katika mikoa ya Dar es Salaam na Njombe.
- Rais Samia awataka wajitafakari na kuja na njia za kukabiliana na hali hiyo.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewataka wakuu wa mikoa nchini kuongeza jitihada za kukabiliana na ongezeko la mimba za utotoni pamoja na udumavu katika maeneo yao ili kujenga jamii bora, yenye afya na kuwa na Taifa lenye maendeleo.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti ya Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa Mwaka 2022 (DHS-MIS 2022) amewaambia wakuu wa mikoa yenye kiwango kikubwa cha udumavu na mimba za utotoni kujitathimini na kutafuta suluhu.
“Wakuu wote wa mikoa ambao mikoa yao iko nyuma katika kuzuia mimba za utotoni, na ile yenye kiwango kikubwa cha udumavu, wajitathimini na kuweka mikakati ya kurekebisha hali hiyo,” amesema Rais Samia.
Kwa mujibu wa Rais Samia kiwango cha mimba za utotoni kwa Mkoa wa Dar es Salaam kimeongezeka kutoka asilimia 11.9 hadi 18.1, Njombe kutoka asilimia 19.7 hadi 25.5 na Ruvuma kutoka asilimia 32 hadi 37.2.
“Kulingana na ripoti hii mikoa inayoongoza kwa kuwa na kiwango kikubwa cha mimba za utotoni ni Songwe 25%, Ruvuma 37%, Katavi 34%, Mara 31% na Rukwa 30% kajiangalieni sababu ni zipi mrudi mlipokuwa,” amesisitiza Rais Samia.
Soma zaidi : Spika Tulia ashinda urais Umoja wa Mabunge Duniani.
Miongoni mwa athari za mimba za utotoni ni pamoja na kukatisha masomo, vifo wakati wa kujifungua, kuongeza utegemezi katika jamii na kupunguza kasi ya maendeleo.
Akizungumzia suala la udumavu Rais Samia amesema ni aibu kuwa na taifa ambalo theluthi ya watoto wanakabiliwa na udumavu kwa kuwa itasababisha kuwa na watu watakaoshindwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za ujenzi wa Taifa.
Mapema mwezi huu alipokuwa akizungumza katika hafla ya kuzima Mwenge wa Uhuru Mkoani Manyara Rais Samia alibainisha kuwa kiwango cha udumavu cha asilimia 30 kilichopo nchini Tanzania ni kiashiria cha hali mbaya ya lishe kwa mujibu wa viwango vya lishe vya Shirika la Afya Duniani (WHO).
Rais Samia aliitaja baadhi ya mikoa inayoongoza kuwa na kiwango kikubwa cha udumavu ukiwemo mkoa wa Iringa, unaoongoza ukiwa na asilimia 56.9 ukifuatiwa na Njombe wenye asilimia 50.4, Rukwa asilimia 49.5, Geita asilimia 38.6 na Ruvuma wenye asilimia 35.6.
Latest
