Alichokisema Rais Samia baada ya Tanzania kufikisha watu milioni 61.7
- Amesema lazima iwepo mikakati madhubuti ya kuwahudumia watu.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amesema ongezeko la idadi ya watu Tanzania ni mzigo kwa Taifa, hivyo lazima iwepo mipango madhubuti ya kuwahudumia watu milioni 61.7.
Hilo ni sawa na ongezeko la asilimia 3.2 ikilinganishwa na idadi ya watu milioni 44.9 waliokuwepo mwaka 2012. Kati ya watu hao, milioni 59.8 wako Tanzania Bara.
Idadi hiyo ya Watanzania imetangazwa leo Oktoba 31, 2022 jijini Dodoma na Rais Samia wakati akizindua Chapisho la Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi la 2022 na Mwongozo wa Kitaifa wa Matumizi ya Sensa ya Watu na Makazi wa mwaka 2022.
“Inawezekana idadi hiyo isiwe tatizo la kuhumiza kichwa kwa nchi kama yetu lakini ni mzigo mkubwa kwa Taifa, jamii na uchumi kwa ajili ya kuwahudumia.
“Kuanzia sasa lazima pawepo na mikakati madhubuti katika mpango wa maendeleo ya jinsi ya kuwahudumia watu hao milioni 61.7,” amesema Rais Samia.
Ifikapo mwaka 2025, Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni 67.9 na ifikapo mwaka 2050 itakuwa na watu milioni151.3.
Amewataka Watanzania kutumia takwimu za sensa kwa madhumuni yaliyokusudiwa ambayo ni kuboresha maisha ya kila Mtanzania.
“Motokeo ya sensa ya idadi ya watu, majengo na anuani za makazi yaanze kutumika katika kupanga miradi ya wananchi, bajeti, sekta binafsi na wawekezaji wote wa mipango jumuishi na maendeleo endelevu kwa Taifa letu,” amesema Rais Samia.
Mwongozo waandaliwa
Serikali imeandaa Mwongozo wa Kitaifa wa Matumizi ya Sensa ya Watu na Makazi wa 2022 ili kuhakikisha matokeo ya sensa yanatumika kutunga na kutekeleza sera za maendeleo ya kisekta na kiutawala.
Mwongozo huo ni wa kwanza tangu Tanzania ipate uhuru na Afrika.
Lengo kuu ya mwongozo ni kuongeza wigo wa uelewa na matumizi ya matokeo ya sensa kwa mwaka huu kwa wadau wote hususani Serikali kupanga mipango jumuishi ya kijamii, kiuchumi na kimazingira kwa maendeleo endelevu.
Utatekelezwa kwa kipindi cha miaka 10 kuanzia Novemba 2022
Amesema elimu ya matumizi ya matokeo ya sensa itatolewa kwa wananchi wote kupitia njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari.
“Mwongozo huo unaeleza kuwa kuna wajibu wa kila mdau kutumia matokeo ya Sensa kuanzia watendaji wote wa Serikali, sekta binafsi na wadau wote pamoja na makundi maalum katika jamii,” amesisitiza Rais Samia.
Mwongozo huo utasaidia kufuatilia na kutathmini malengo yaliyowekwa kitaifa katika maendeleo kwa pande zote za muungano lakini vilevile mipango ya kimataifa ambayo Tanzania imeridhia.
Latest
