TLS, wadau wa maendeleo waomba kukutana na Rais Samia
- Wasema majadiliano na Rais ni muhimu kulinda amani, haki na mshikamano wa kitaifa.
Dar es Salaam. Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kimeomba kukutana na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ili kuwasilisha maoni ya wadau mbalimbali kuhusu changamoto zinazopaswa kutatuliwa kabla ya uchaguzi mkuu wa 2025.
Hatua hiyo huenda ikasaidia kuongeza ushiriki wa makundi mbalimbali ambayo yamekuwa yakilalamikia baadhi ya vitu ikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo Chadema.
Rais wa TLS, Wakili Boniface Mwabukusi aliyekuwa akizungumza leo Agosti 26, 2025 na wanahabari jijini Dar es Salaam amesema tayari wamewasiliana na Ofisi ya Rais kwa ajili ya kuwasilisha maazimio hayo.
“Lengo letu TLS kwenda kwa Rais hatuendi ‘kudictate’ tunaenda kwa unyenyekevu kumwambia Rais wewe ni Rais wa Tanzania, sio wa Chama cha Mapinduzi (CCM), sio wa wabunge, sio wa vyombo vya ulinzi na usalama…
…Huyo ni Rais wetu sote. Tunapokuwa na hoja kama hizi tunawasilisha kwake tupate ‘forum’ ya kukaa naye atusikilize,” ameeleza Mwabukusi.

Hata hivyo, Mwabukusi amebainisha kuwa changamoto zinazojitokeza wakati wa uchaguzi zinapaswa kuwa za kimsingi na siyo zinazotokana na wale wanaohusika na uratibu wa uchaguzi.
Kwa mujibu wake, TLS imekuwa mstari wa mbele kuratibu mazungumzo ya amani yaliyojumuisha taasisi za dini, vyama vya siasa, watu mashuhuri pamoja na asasi za kiraia, ili kujadili haki, amani na utulivu kabla na baada ya uchaguzi.
“TLS imeratibu mazungumzo ya amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu (2025)… Lengo kuu lilikuwa ni kujadili masuala ya haki, amani na utulivu kabla, wakati na baada ya uchaguzi kwa kuzingatia changamoto na fursa zilizopo kwenye mifumo ya kisheria, kitaasisi na kijamii,” ameongeza Rais wa TLS.
Aidha, TLS imesisitiza kuwa itaendelea kuwa daraja la haki kwa njia ya mazungumzo na maelewano bila kumlazimisha au kumpendelea mtu na kwamba mazungumzo na Rais yanalenga kurejesha imani ya wananchi na kuhakikisha uchaguzi unakuwa shirikishi, huru na wa haki.
Latest