Ofisi za TLS zazingirwa na polisi, wadau wa haki watoa neno
- Wadau wa haki walitaka Jeshi la Polisi kuheshimu misingi ya sheria, pamoja na kanuni na miongozo ya kimataifa.
Arusha. Mvutano wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na Jeshi la Polisi Tanzania umechukua sura mpya baada ya TLS kudai ofisi zao kuzingirwa na polisi kuanzia asubuhi ya leo huku baadhi ya wadau wa haki wakikemea vitendo hivyo.
Taarifa ya Boniface Mwabukusi rais wa TLS, iliyotolewa leo Septemba 22, 2025 imewataka mawakili wanaofika katika ofisi za chama hicho kuendelea kuwa watulivu wakati wakiendelea na mazungumzo katika mamlaka zinazohusika.
“Tunawasihi mawakili wote kubaki na tahadhari na kutochokozeka kwa uchokozi huu wa makusudi unaofanywa dhidi yao na Jeshi la Polisi na kutii maelekezo ya baraza la uongozi tuliyowasilisha kwenu kwa maandishi kuhusu umuhimu wa kutoa nafasi kwa mazungumzo yaliyokwisha anza…
…Ni jukumu letu sisi viongozi kushughulikia jambo hili kwa haraka na kwa wakati na kutoa mrejesho kwenu kwa wakati,” imesema taarifa ya Mwabukusi.
Itakumbukwa kuwa Septemba 18 mwaka huu baraza la uongozi la TLS lilitangaza kuandaa maandamano ya amani nchi nzima, ikiwa ni ishara ya kulaani kitendo cha kushambuliwa kwa wakili Deogratius Mahinyila na askari wa Jeshi la Polisi, Septemba 15, 2025, katika viwanja vya Mahakama Kuu, Masijala Ndogo ya Dar es Salaam.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi lilizuia maandamano hayo likidai barua yao ya maombi ya maandamano haijakidhi vigezo ikiwemo kukosekana kibali cha Jaji Mkuu.
Pamoja na hayo jeshi hilo pia lilidai maandamano hayo yamezuiwa kutokana na shughuli za kampeni zinazoendelea kufanyika na askari watakuwa kwenye ulinzi wa kampeni.
Baadhi ya wadau wa haki ikiwemo Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) wamepinga kitendo cha Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kuzingira ofisi za makao makuu ya TLS.
LHRC imesema Jeshi la Polisi linapaswa kuheshimu misingi ya sheria, pamoja na kanuni na miongozo ya kimataifa na kikanda inayolinda uhuru wa vyama vya wanasheria katika kutekeleza majukumu yao kwa uhuru na bila hofu.
“Tunatoa wito kwa Polisi kuchukua hatua za haraka kuwaondoa askari walioko katika ofisi za TLS ili kuruhusu mawakili na wateja wao kuendelea na shughuli zao kwa amani na utulivu,” imesema taarifa ya LHRC.
Latest