Tanzania yaimarisha diplomasia ya uchumi katika tasnia ya utalii kimataifa
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro akiwa katika picha pamoja na Kiongozi wa Vyama vya Wasafirishaji Watalii wa nchini Marekani, Rumit Mehta wakiwa wameshika picha ya twiga katika ofisi za Ubalozi za Tanzania nchini Marekani mara baada ya kumaliza kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano kwenye sekta ya utalii. Picha| Wizara ya Maliasili na Utalii.
- Yawataka mabolozi wake kuhubiri diplomasia hiyo kila kona ya dunia.
- Hiyo itasaidia kuvutia watalii na kuongeza mapato ya nchi.
Dar es Salaam. Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro amewataka watumishi wa ubalozi wa Tanzania nchini Marekani kuweka nguvu za kutosha katika kutekeleza diplomasia ya uchumi ikiwemo kuwavutia watalii kutoka nje ya nchi kuja nchini.
Dk Ndumbaro ametoa kauli hiyo Januari 28, 2022 mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea ofisi ya ubalozi huo ikiwa ni muendelezo wa kuzungumza na watumishi na wawekezaji mara baada ya kumalizika kufanyika kwa mkutano wa 50 wa mwaka wa uwindaji wa kitalii uliofanyika katika Jiji la Las Vegas nchini Marekani.
Akizungumza na timu ya watumishi hao, Dk Ndumbaro amempongeza Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Dk Elsie Kanza kwa kazi kubwa anayoifanya ya diplomasia katika tasnia ya biashara na utalii.
“Nimevutiwa mno kwa jinsi unavyoitendea haki diplomasia ya uchumi natamani mabalozi wengine wanaoziwakilisha nchi zetu nchi za nje wajifunze kutoka kwako,” amesisitiza Dk Ndumbaro.
Amewataka wanadiplomasia hao kuwa daraja katika kuwawezesha watalii kuja nchini Tanzania
Zinazohusiana:
- Serikali kuwabana wanaopangisha nyumba kwa watalii bila leseni.
- Tamasha la Urithi Festival kufanyika mikoani kila mwaka.
Amesema diplomasia ya uchumi katika tasnia ya utalii inapaswa kutangaza na kujibu maswali ya watu mbalimbali wanaotaka kutalii Tanzania kuhusu namna ya kufika nchini na katika kila kivutio cha utalii.
“Kutokana na kasi kubwa ya maendeleo ya kiuchumi, mabalozi wanaoziwakilisha nchi, diplomasia ya kiuchumi ndio injini ya maendeleo haikwepiki, ongezeni ujuzi katika eneo hili,” amesisitiza Dk Ndumbaro.
Aidha, amewahimiza watumishi hao kuwa mstari wa mbele katika kujua masuala ya uwekezaji na biashara pamoja na mambo yote muhimu kuhusu utalii nchini ili waweze kuwaelezea wananchi wanaowahudumia.
Vilevile amewataka wanadiplomasia hao kuwa kichocheo cha watalii kutoka katika nchi waliyopo kuhudhuria katika mikutano, makongamano na maonyesho ya utalii ya ndani ya Tanzania ikiwemo matamasha ya kiutamaduni.