Msimamo wa Tanzania kuhusu diplomasia ya uchumi kimataifa
- Ni kuendelea kushirikiana na nchi mbalimbali duniani.
- Kuweka mazingira bora ya uwekezaji na biashara.
- Kuitangaza Tanzania katika majukwaa ya kimataifa.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano na mataifa mbalimbali duniani ikiwemo Marekani katika sekta zote za maendeleo ili kusaidia kuongeza fursa za uwekezaji na biashara.
Kiongozi huyo mkuu wa shughuli za Serikali amesema Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuendelea kuifungua Tanzania kimataifa katika maeneo mbalimbali ili kuongeza fursa kwa Watanzania.
“Mheshimiwa Rais ameelekeza tufanye mapitio na maboresho ya uwekezaji na biashara, kwa kupitia sheria zetu na kuondoa maeneo ambayo yanakwaza wafanyabishara na kujenga uwezo kwa Watanzania kufanya biashara nje ya nchi, lengo ni kuinua uchumi na kufungua fursa za ajira kwa vijana wetu,” amesema Majaliwa.
Majaliwa ametoa msimamo huo leo Februari 23, 2022 alipozungumza na wabunge wa Bunge la Marekani Katika ofisi ndogo ya Waziri Mkuu, Magogoni Jijini Dar es Salaam ambao wako nchi ikiwa ni sehemu ya kuendeleza uhusiano wa nchi hizo mbili.
Waziri Mkuu amesema kuwa wabunge hao wamefurahi kuona mahusiano kati ya nchi hizi mbili yanakua na kuimarika.
“Mahusiano yetu kiuchumi yanaendelea kuimarika, wanatambua mchango wa Tanzania katika kutoa fursa za uwekezaji hapa Tanzania na sisi kufanya nao biashara, tutaendelea kuimarisha kwa kuwa na forum (majukwaa) mbalimbali za wafanyabishara wa ndani ya nchi na Wamarekani,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi:
- Rais Samia ataja virusi vitatu vinavyotafuna maendeleo ya Mara
- Tanzania itakavyofaidika ziara ya Rais Samia nchini Ufaransa, Ubelgiji
Amesema kuwa wabunge hao wameahidi kushirikiana na Tanzania katika mpango wa kuinua uchumi kupitia miradi na programu mbalimbali za taasisi za Marekani.
“Wameahidi kuendelea kuwa nasi na sisi tumeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano wetu, tutaendelea kumpa ushirikiano balozi wa Marekani ili tuweze kuongeza fursa za mashirikiano katika maeneo mengi zaidi na misaada yote tutaitumia katika malengo yaliyokusudiwa,” amesema.
Amewataka wabunge hao kuwa mabalozi wa kuhamasisha utalii kati ya Tanzania na Marekani kwa kuwa Tanzania imebarikiwa vivutio vingi
“Eneo la utalii tumewahamasisha ndugu zetu waje kuona vivutio vingi tulivyonavyo,” amesisitiza.
Wabunge walioshiriki mkutano huo ni Gregory Meeks, Ami Bera, Ilhan Omar, Joyce Beatty, G.K Butter, Brenda Lawrence na Troy Carter.
Wabunge hao waliambatana na Balozi wa Marekani Nchini Tanzania Dk Donald Wright.