Tanzania ilivyojipanga kudhibiti wimbi la tano la Uviko-19
- Unalenga kuchanja watu 59,000 kwa siku.
- Watanzania wahimizwa kuendelea kuchukua tahadhari kwani korona ipo.
Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Serikali na wadau wa maendeleo wataongeza kasi ya utoaji chanjo ili kukabiliana na tishio la wimbi la tano la ugonjwa wa Corona (Uviko-19).
Utoaji wa chanjo ya Uviko-19 utaenda sambamba na kampeni mpya yenye lengo la kuongeza kasi ya kuhamasisha jamii kupata chanjo pamoja na kufuatilia wale ambao hawakukamilisha chanjo yenye dozi mbili.
Waziri Ummy amesema kuwa kutokana na mataifa jirani ya Kenya na Afrika Kusini kuripoti ongezeko la wagonjwa wa Uviko-19, wizara yake na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) wanaongeza jitihada katika afua za kukabiliana na ugonjwa huo.
“Ugonjwa wa Uviko-19 bado upo na kwa sababu ipo hatari au tupo katika tishio la kupata wimbi la tano la mlipuko wa Uviko-19 ndiyo maana pia leo tunazindua mpango huu wa Global Vax ili kuwatayarisha Watanzania kuweza kupambana na wimbi linalokuja la Uviko-19,” amesema Ummy jana Juni 2, 2022 wakati wa uzinduzi wa mkakati huo unaofahamika kama Global Vax.
Kasi ya kuchanja kuongezeka
“Ninapenda kuwakumbusha kwamba ili tufikie kinga jamii (herd immunity), hapa nchini tumejiwekea malengo ya kutoa chanjo ya Uviko-19 kwa walengwa milioni 21.5 ifikapo Desemba, 2022. Idadi hii ni sawa na asilimia 70 ya wananchi wenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea,” amesema Ummy.

Latest
