Tanzania ilivyojipanga kudhibiti uvujaji mitihani ya utabibu
- Kuboresha mifumo ya usimamizi wa mitihani.
- Kuunda mamlaka kamili ya kusimamia mafunzo ya vyuo vya afya.
Dar es Salaam. Baada ya Serikali ya Tanzania kukiri kuvuja kwa mitihani ya utabibu ngazi ya stashahada, imesema itaimarisha mifumo yake ya usimamizi katika ngazi zote ili kuhakikisha vitendo hivyo havijirudii tena.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Omary Kipanga ametoa kauli hiyo leo Mei 31, 2022 jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Husna Sekiboko aliyetaka kujua kauli ya Serikali kuhusu kuvuja kwa mitihani hiyo.
“Nini ni kauli ya Serikali juu ya kuvuja kwa inayosimamiwa na vyuo vya afya 2021,” ameuliza Sekiboko.
Akijibu swali hilo, Kipanga amesema kuwa Serikali itaboresha mifumo ya uchapishaji na ufungaji wa mitihani, kufanya mapitio ya miongozo ya mitihani iliyo chini ya Wizara ya Afya ili kuendana na mahitaji ya ulinzi na kiusalama.
Pia itaanzishwa mamlaka itakayayosimamia mafunzo ya vyuo vya afya ngazi ya kati pamoja na uendeshaji wa mitihani.
Oktoba mwaka jana, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) lilizuia matokeo ya mitihani ya utabibu ngazi ya stashahada ikisubiri uchunguzi unaofanywa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto kutokana na kuvuja kwa mitihani hiyo.
Mitihani hiyo iliyofanywa kati ya Agosti 12 na Septemba 11 mwaka jana katika vyuo 147 nchini, ilivuja kwa baadhi ya vyuo kuinunua.
Baadhi ya wabunge wamesema Serikali inapaswa kutoa adhabu kali kwa maafisa wote wa Wizara ya Afya waliohusika na uvujaji wa mitiani hiyo kama ambavyo imekuwa ikifanya kwa shule za msingi na sekondari.
Latest