Magari ya umeme, gesi kupata ahueni zaidi bajeti 2026/27
- Ni baada ya Serikali kupendekeza punguzo la kodi kwenye bidhaa na vifaa vinavyohusiana na nishati hizo.
Dar es Salaam. Watumiaji wa vyombo vya moto vinavyotumia umeme na gesi ni miongoni mwa watu watakaonufaika na bajeti kuu ya Serikali ya 2026/27 baada ya Serikali kupendekeza punguzo la kodi kwa viwango mbalimbali.
Hatua hizo za kikodi zinalenga kubadilisha muundo wa usafiri na matumizi ya nishati nchini huku ikiashiria mwelekeo mpya wa uchumi chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, aliyekuwa akiwasilisha bajeti hiyo kwa mara ya kwanza bungeni, amesema mapendekezo hayo ni pamoja na kusamehe Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye vifaa vitakavyotumika katika vituo vya kuchaji magari yanayotumia umeme vinavyoingizwa nchini.
Mbali na kusamehe VAT, amesema Serikali inapendekeza kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10 kwa baadhi ya aina za magari yanayotumia nishati ya umeme, hatua inayotarajiwa kushusha gharama za uagizaji na kuongeza upatikanaji wa magari hayo nchini.
Ndani ya miaka miaka miwili kumekuwa na mwamko mkubwa miongoni mwa Watanzania wa kutumia vyombo vya moto vya umeme yakiwemo magari na pikipiki yakiwemo maguta ya kubebea mizigo.
“Serikali inaendelea kufanya majadiliano na viwanda vya kuunganisha magari vilivyopo nchini ili kutoa unafuu wa kodi kwa waunganishaji wa magari ya umeme nchini,” amesema Omar.
Mapendekezo hayo yamewasilishwa kupitia hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27, na yanatarajiwa kuanza kutekelezwa mwezi Julai mwaka huu endapo yatapata idhini ya Bunge.
Serikali pia imependekeza kusamehe VAT kwenye mita janja za gesi ya kupikia (LPG smart meter) zinazoingizwa nchini, huku msamaha huo ukielekezwa kwa wasambazaji wa gesi ya kupikia pekee.
Kutatua changamoto ya mafuta?
Punguzo hili la kodi linakuja wakati ambapo Watanzania wanaugulia maumivu ya kupanda kwa bei ya mafuta iliyoongezeka kwa mfumuko wa bei ambao kufikia Mei mwaka huu umekua kwa asilimia 4.2.
Huenda kupunguza ushuru wa magari ya umeme kunalenga kupunguza utegemezi wa mafuta kupitia bajeti hii ya kwanza tangu Rais Samia Suluhu Hassan aanze muhula wake wa pili wa uongozi na bajeti ya kwanza kutekelezwa chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Aidha pia, kupunguza ushuru wa magari ya umeme kunatarajiwa kupunguza bei za magari hayo sokoni na kuongeza kasi ya kutoka kwenye matumizi ya mafuta kwenda kwenye nishati mbadala.
Hata hivyo, mafanikio ya hatua hiyo yatategemea upatikanaji wa miundombinu ya kutosha ya kufanikisha mwelekeo huo mpya.
Ikiwa hatua hizi zitatekelezwa sambamba na uwekezaji katika miundombinu, ushirikiano na sekta binafsi na utoaji wa elimu kwa umma, Tanzania inaweza kujijengea msingi imara wa uchumi wenye ushindani, unaojali mazingira na unaoendana na mabadiliko ya teknolojia duniani.
Katika miaka ya hivi karibuni, serikali tayari imeanza kuweka mazingira ya mpito huo kupitia msamaha wa ushuru wa bidhaa kwa magari ya umeme na yale yanayotumia gesi kulingana na uwezo wa injini, kuondoa VAT kwenye gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) na vifaa vyake vya usambazaji, pamoja na msamaha wa kodi kwenye mnyororo mzima wa uzalishaji wa CNG.
Vilevile, imepunguza ushuru wa forodha kwa betri za magari na pikipiki za umeme, pamoja na vifaa vya kubadilisha magari kutoka mafuta kwenda nishati mbadala hatua zinazolenga kupunguza gharama za uwekezaji na kuharakisha matumizi ya nishati safi nchini.