TNMC yafuta matokeo ya watahiniwa 1,330 wa uuguzi na ukunga ngazi ya diploma
- Ni baada ya kubainika kuvuja kwa mitihani ya stashahada.
- Watahiniwa kurudia mitihani yao Februali 16, 2024 jijini Dodoma.
Dar es Salaam. Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC) limefuta matokeo ya mitihani ya usajili na leseni kwa wauguzi na wakunga tarajali 1,330 baada ya kubainika kuvuja kwa mitihani hiyo kabla haijafanyika.
TNMC ambayo ipo chini ya Wizara ya Afya, ina jukumu la kusimamia taaluma za wauguzi na wakunga nchini kupitia Sheria ya Uuguzi na Ukunga ya Mwaka 2010.
Pamoja na majukumu mengine, TNMC imepewa jukumu la kusajili, kuorodhesha, na kutoa leseni kwa wauguzi na wakunga wa ngazi zote, kwa kuendesha Mitihani ya Usajili na Leseni kwa Mujibu wa Kifungu cha 15(a) (b) cha Sheria ya Uuguzi na Ukunga ya mwaka 2010.
Soma zaidi : Mwanza na mapambano dhidi ya ugonjwa wa kipindupindu
Englibert Kayombo, ambaye ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini amebainisha katika taarifa aliyoitoa leo Januari 16, 2024 kuwa wizara ilipata taarifa za kuvuja kwa mtihani iliyofanyika Setemba 7, 2023 ambapo baada ya uchunguzi ilithibitika mitihani imevuja na kusambaa kwa watahiniwa wa stashahada.
“Wizara inautangazia umma kuwa matokeo yote ya mtihani wa usajili na leseni wa wauguzi na wakunga kwa watahiniwa wa Stashahada yamefutwa kwa mujibu wa Sheria ya Uuguzi na Ukunga ya Mwaka 2010, Kanuni ya mafunzo ya Mwaka 2010, Kifungu cha 22(3),” amebainisha Kayombo.
TAARIFA KWA UMMA
KUHUSU KUFUTWA KWA MATOKEO YA MTIHANI WA USAJILI NA LESENI YA BARAZA LA UUGUZI NA UKUNGA TANZANIA KWA WATAHINIWA 1,330 WA STASHAHADA pic.twitter.com/Z9Q9sDIil8
— Wizara ya Afya Tanzania ?? (@wizara_afyatz) January 16, 2024
Kayombo ameongeza kuwa, mtuhumiwa aliyehusika katika uvujishaji wa mtihani tayari amebainika na kusimamishwa kazi huku taratibu za kinidhamu na kisheria zikiendelea kutekelezwa.
Kwa mujibu wa Kayombo, Hatua hizo zimechukuliwa kwa lengo la kuhakikisha baraza linathibitisha wataalam wenye sifa stahiki kulingana na taaluma zao kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa pamoja na kuzingatia usalama wa mteja anayetegemea kupata huduma za uuguzi na ukunga.
Soma zaidi : Waziri Ummy: Kuna changamoto utekelezaji wa Sera ya matibabu bure
Hata hivyo, siku za hivi karibuni yameripotiwa matukio kadhaa yaliyolitia doa kada ya afya nchini, ikiwemo vifo vya wajawazito mfululizo, huku sababu ikitajwa kuwa ni uzembe wa wahudumu wa afya, wakiwemo wakunga, na madaktari.
Nini hatma ya watahiniwa?
Kutokana na kufutwa kwa matokeo yao TNMC imebainisha kuwa, watahiniwa wote wa stashahada watapewa nafasi ya kufanya mtihani mwingine bila malipo yoyote na hawatahitajika kujisajili tena Februali 16, 2024 jijini Dodoma.
Matokeo ya mitihani ya usajili na leseni kwa wauguzi na wakunga yaliyofutwa ni ya ule uliofanyika Septemba 7, 2023 kwa wauguzi na wakunga 1,434 wa ngazi zote.
Kwa watahiniwa wengine Kayombo amesema matokeo yao yameshatoka na wameshayapata.
Latest